Image
Image

TPSF; DK MENGI NDIYE MWENYE KITI HALALI WA TAASISI HII.



Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi, akipongezwa na Mwenyekiti wa Bodi anayemaliza muda wake wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Esther Mkwizu (kulia), baada ya kuibuka mshindi wa kiti hicho cha uongozi katika uchaguzi uliofanyika wakati wa Mkutano Mkuu wa 14 wa mwaka wa taasisi hiyo jijini Dar es Salaam mwishoni wa wiki. Aliyekaa ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji), Dk. Mary Nagu na Makamu Mwenyekiti mpya wa taasisi hiyo, Salum Shamte (wa pili kulia).
Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa mwaka wa 14 wa Taasisi ya Sekta Binafsi nchini (TPSF) wamemchagua Dk. Reginald Mengi kuwa Mwenyekiti mpya wa Bodi ya taasisi hiyo katika uchaguzi uliofanyika mwishoni mwa wiki.



Uchaguzi huo mkuu ulikuwa ni sehemu ya mkutano mkuu wa mwaka ambapo taasisi hiyo ilitumia fursa hiyo kufanya uchaguzi wa kupata bodi mpya baada ya bodi iliyokuwa ikiongozwa na Esther Mkwizu kumaliza muda wake.



Uchaguzi huo ulioendeshwa kwa njia ya kura ulisimamiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Joyce Mapunjo.



Wajumbe wa mkutano mkuu waliopiga kura walikuwa 73 ambapo Dk. Reginald Mengi alipata kura 39 huku mgombea mwingine, Salum Shamte akipata kura 34. 

Hapakua na kura iliyoharibika.

“Kulingana na sheria ya taasisi hii aliyepata kura nyingi anakuwa mwenyekiti mpya wa bodi  wakati aliyepata kura pungufu anakuwa Makamu Mwenyekiti wa Bodi,” alisema  Mapunjo alipokua akitangaza matokeo hayo.



Kwa maana hiyo, Salum Shamte anakua Makamu Mwenyekiti mpya.

Viongozi hao wapya watahudumu katika nafasi hizo kwa muda wa miaka miwili na baada ya kumaliza wanaweza kuingia katika uchaguzi tena kuomba ridhaa ya kuongoza katika kipindi cha pili.



Mkutano huo mkuu pia uliwachagua wajumbe 11 walioomba uongozi kupitia kongano wanazotoka ili kuwa wajumbe wa bodi hiyo.



Wajumbe wa bodi waliochaguli ni pamoja na Deodatus Mwanyika atakaewakilisha sekta ya Nishati na Madini, Felix Mosha (Uzalishaji/ Viwanda),  Enock Dondole (vikundi vya biashara mikoani),  Anna Matinde (wajasirimali wanawake), Mbarouk Omar (Taasisi ya Sekta Binafsi Zanzibar).



Wengine ni  Peter Chisawillo (Biashara),  Salum Shamte (Kilimo),  Gaudence Temu (Rasilimali na Utalii), Dk. Gideon Kaunda (Makampuni), Dk. Charles Kimei (Benki na huduma za kifedha) na Dk. Reginald Mengi (huduma).



Baada ya kutangazwa mshindi, Dk. Mengi alisema katika kipindi chake atashirikiana na bodi na sekretarieti ya TPSF kuhakikisha yale yote mazuri yaliyofanywa na uongozi uliopita yanaendelezwa.



“Tunahitaji kuzidi kuifanya sekta hii kuwa na sauti moja na yenye nguvu ili iweze kushiriki vema katika uchumi wa  nchi yetu,” alisema na kuongeza kuwa sekta hiyo ndiyo injini ya uchumi wa taifa.

Alitoa changamoto kwa serikali kutumia fursa za rasirimali zilizopo nchini kwa kuwapa kipaumbele Watanzania kwa ajili ya maslahi zaidi ya nchi kama zilivyofanya nchi za Korea kusini na Malasia.



Pia alisema mataifa yote duniani yanaweka kipaumbele zaidi kwa watu wake katika nyanja zote.



Akitoa mfano alisema kwasasa ambapo taifa linaanza kuvuna rasirimali ya gesi na rasirimali nyingine, ni vyema vitalu vitolewe kwa ajili ya kuvuna gesi baada ya kuwa sera inayoongoza uchimbaji huo kupatikana.



“Ili nchi iweze kufaidika zaidi ni vyema Watanzania wakapewa vitalu vya kuchimba gesi ili wakatafute wabia au fedha kutoka taasisi za fedha za kimataifa kwa ajili ya kuvuna ili faida kubwa ibakie nchini,” alisema.



Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF,  Godfrey Simbeye alisema taasisi hiyo imepata kwa mara nyingine viongozi mahiri katika nyanja ya masuala ya biashara na wenye ushawishi katika kuzungumza na serikali.



“Tunategemea bodi hii itazidi kuwa kichocheo na tutazidi kufanya vizuri zaidi kutokana na uzoefu wa viongozi hawa na mafanikio yatakuwa makubwa kwa faida ya taifa zima,” alisema.

TPSF ni taasisi ya sekta binafsi inayoundwa na vyama vinavyowakilisha sekta binafsi  mbalimbali nchini.



Wakati huo huo, serikali imesema itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) kama njia ya kuimarisha sekta binafsi nchini na kuifanya kuwa injini ya ukuaji wa uchumi na ustawi wa jamii.



Kauli hiyo ilitolewa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda katika mkutano mkuu wa 14 wa taasisi hiyo uliofanyika mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam na kusisitiza kuwa nia ya serikali ni kuona kuwa taasisi hiyo inashika hatamu katika uchumi wa nchi.



Alisema kuwa kwa muda wa miaka mitatu sasa jtihada za makusudi za serikali   na wadau wa sekta binafsi zimeelekezwa katika kujenga sauti moja ya sekta binafsi Tanzania.



“Ni matumaini yangu kwamba taasisi yenu itatekeleza majukumu yake ya msingi ya kutetea maslahi ya sekta binafsi na kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazoikabili sekta binafsi nchini kwa ufanisi wa hali ya juu,” alisema.



“Ninafarijika kwamba tayari matunda ya jitihada hizi yameanza kuonekana kwa kuweka mfumo madhubuti wa uongozi kwenye taasisi yenu tofauti na ilivyokua awali,” alisema.

 
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment