AbdulQader Muhammad Mkuu wa Wilaya ya Lower Shabelle nchini Somalia
amesema kuwa, kwa akali wanamgambo 20 wa al Shabab wameuawa kwenye
shambulio lililofanywa na ndege za kivita karibu na mji wa Marga kusini
mwa Somalia. Abdulqader Muhammad ameongeza kuwa, shambulio hilo
lililofanywa na ndege ya kigeni kwenye kambi ya al Shabab, limeharibu
magari na boti kadhaa za wanamgambo hao.
Wakati huohuo, kundi la
kigaidi la al Shabab nchini Somalia limetekeleza shambulio dhidi ya
uwanja wa ndege wa Mogadishu na kuwauwa wafanyakazi wanne na kuwajeruhi
wengine kadhaa. Polisi ya Mogadishu imeeleza kuwa, watekelezaji wa
shambulio hilo wakiwa garini walilifyatulia risasi kadhaa kundi la
wafanyakazi waliokuwamo uwanjani hapo. Taarifa iliyotolewa na Polisi ya
Mogadishu inaeleza kuwa, msaidizi wa mkuu wa uwanja wa ndege wa
Mogadishu ni miongoni mwa watu waliouawa kwenye shambulio hilo.
Mwaka
2011, majeshi ya Somalia yakisaidiwa na Kikosi cha Kulinda Amani cha
Umoja wa Afrika nchini Somalia AMISOM yalifanikiwa kuwafurusha
wanamgambo wa al Shabab kutoka mji mkuu wa nchi hiyo. Kundi la al Shabab
licha ya kutekeleza operesheni mbalimbali za kigaidi ndani ya Somalia,
limekuwa likitekeleza operesheni kadhaa nje ya nchi hiyo na hasa nchini
Kenya.
0 comments:
Post a Comment