Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Said Meck Sadiki
akifungua moja ya bomba la maji la mradi wa Maji ya Kisima mtaa wa
Mongolandege, Ilala jijini Dar es salaam wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya
Wiki ya Maji mkoani Dar es salaam.
Bi.Martha Singano, Mkazi wa Mongolandege akipokea ndoo ya
maji kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Said Meck Sadiki mara baada
ya kuzindua mradi wa Maji ya Kisima katika mtaa huo.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe.Said Meck Sadiki akitoa
ufafanuzi kuhusu maadhimisho ya Wiki ya Maji mkoani Dar es salaam.
Tanzania inaungana na mataifa mengine duniani kuadhimisha
Wiki ya maji kuanzia tarehe 16 hadi 22, Machi 2015 chini ya Kauli Mbiu isemayo
Maji kwa Maendeleo Endelevu.
Maadhimisho ya mwaka huu yanatoa fursa kwa Mamlaka
zinazohusika na usimamizi wa Maji nchini kutathmini huduma wanayoitoa kwa
wananchi, kujenga na kuimarisha miundombinu iliyopo katika maeneo mbalimbali
nchini.
Akizindua Maadhimisho ya Wiki ya Maji kwa mwaka 2015 katika
Mkoa wa Dar es salaam, Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Said Meck Sadiki
amesema maadhimisho hayo katika jiji la Dar es salaam pamoja na mambo mengine
yataambatana na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASA) kuzindua miradi maji
katika maeneo mbalimbali ya jiji, kutoa elimu kuhusu utunzaji wa vyanzo vya
maji, utunzaji wa miundombinu ya miradi inayojengwa, upokeaji wa maoni na kero
za wananchi pamoja operesheni za kukamata baadhi ya watu wanaoiba na kuhujumu
miundominu ya maji.
Amesema maadhimisho hayo mkoani Dar es salaam yatazindua
miradi ipatayo 9 na kuweka mawe ya msingi katika miradi 2 na kuongeza kuwa
chini ya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) mkoa unatekeleza jumla ya miradi
41 ya Visima vya maji katika wilaya za Ilala, Kinondoni na Temeke.
Mhe. Saidi Meck Sadiki ameseama miradi mingine 14
iliyojengwa chini ya ufadhili wa Serikali ya Ubelgiji (BTC) imekamilika na
inaendelea kuwahudumia wananchi katika wilaya zote tatu za jiji la Dar es
Salaam.
Amefafanua kuwa jiji la Dar es salaam linaongoza nchini kwa
kuwa na mahitaji makubwa ya maji huku huduma ya Maji kwa wakazi hao ikitolewa
na Mamlaka ya Maji ya jiji la Dar es salaam (DAWASA) ambayo imekodisha shughuli
za uendeshaji huduma kwa DAWASCO. Vyanzo vikuu vya maji katika jiji la Dar es
salaam mto Ruvu, Kizinga pamoja na maji yanayopatikana chini ya ardhi.
Amesema mahitaji ya maji kwa wakazi wa jiji na baadhi ya
maeneo ya mkoa wa Pwani kwa sasa ni wastani wa lita 450 kwa siku huku uwezo wa
kuzalishaji maji kwa siku ni lita 300 ambazo ni sawa na asilimia 66.7 ya
mahitaji yote.
Ameeleza kuwa upungufu huo unaosababishwa na uwezo mdogo wa
mitambo na miundombinu ya kuzalisha maji na kuongeza kuwa Serikali kupitia
sekta 6 zilizopewa kipaumbele chini ya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa, Maji
yamepewa kipaumbele ambapo miradi ya maji 41 mkoani Dar es salaam itatekelezwa
ili kufikia lengo la Serikali la uzalishaji wa lita 710 ambazo zitakua ni zaidi
ya mahitaji mwishoni mwa mwaka 2015.
“Matarajio yangu na mkoa ninaouongoza ni kuhakikisha kuwa
tunawapatia watu milioni 3.8 ambao ni asilimia 90 ya wananchi katika jiji la
Dar es salaam huduma ya majisafi na salama mwishoni mwa mwaka 2015” Amesisitiza.
Ameleza kuwa DAWASA inatekeleza mpango maalum wa kuongeza
upatikanaji wa maji jijini Dar es salaam kwa kupanua Mitambo ya Ruvu chini
ambayo kazi yake imekamilika kwa asilimia 100, ujenzi wa bomba kuu kutoka Ruvu
chini hadi chuo kikuu cha ardhi ambao umekamilika kwa asilimia 93, kazi ya
upanuzi wa mtambo wa Ruvu juu na ujenzi wa bomba la maji hadi Kimara ambao
umefikia asilimia 55 utakaokamilika mwezi Agosti, 2015.
Aidha, amesema kazi ya uchimbaji wa visima 20 katika awamu
ya kwanza imeanza na itakamilika mwezi Agosti mwaka huu ikihusisha pia upanuzi
wa mtandao wa usambazaji wa maji katika maeneo yaliyo kandokando ya mabomba
makuu kutoka Ruvu chini na Ruvu juu na kunufaisha vitongoji vilivyopo kati ya
mji wa Bagamoyo hadi eneo la Tegeta-Mpiji na vitongoji vilivyopo kati ya mji wa
Mlandizi –Kiluvya na maeneo ya Mbezi, Kimara na Goba.
Awamu ya pili itahusisha upanuzi wa mfumo wa usambazaji wa
maji katika maeneo yote ya jiji yatakayopata maji kutoka Kimbiji na Mpera na
maeneo mengine ya jiji yasiyo na mabomba ya usambazaji.
Akitoa ufafanuzi kuhusu mradi wa visima vya dharula katika
maeneo yasiyo na maji ya bomba amesema jumla ya visima 48 vimechimbwa katika
maeneo mbalimbali ya jiji yakiwemo Kimara,Kimara, Kisukuru, Keko –Chang’ombe,
Sandali, Mburahati, Mbagala, Mtoni, Kigamboni ,Gerezani na Ukonga
Katika hatua nyingine Mhe. Saidi Meck Sadiki ameeleza kuwa
Serikali itaendelea kuchukua hatua kali za kisheria kwa baadhi ya watu
wanaorudisha nyuma juhudi za Serikali za kuwapatia wananchi maji safi kwa
kuhujumu miundombinu ya maji ya DAWASCO kwa kuendesha vitendo vya wizi wa maji,
mambomba na miundombinu mingine.
Pia ameitaka DAWASCO na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na
Maji (EWURA) kuanza kuwafuatilia na kuwadhibiti baadhi ya wafanyabiashara wanaowaibia
wananchi kwa kununua maji ya DAWASCO kwa gharama nafuu ya shilingi 1 kwa lita
na kuyauza kwa zaidi ya shilingi 50.
0 comments:
Post a Comment