Hotuba
ya mhe. Dkt. Jakaya mrisho kikwete, rais wa jamhuri ya muungano wa tanzania kwenye
maadhimisho ya siku ya mwalimu nyerere (nyerere day) na uzinduzi wa program
maalumu ya uongozi na maadili ya chuo cha kumbukumbu ya mwalimu nyerere,
jumatatu tarehe 13 aprili, 2015 kivukoni-dar es salaam.
Mheshimiwa Dkt. Shukuru
Kawambwa, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi;
Mhe. Meck Said Sadick,
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam;
Mhe. Bi Sophia Mjema, Mkuu wa Wilaya ya Temeke;
Mheshimiwa Dkt. Terezya
Huvisa, Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo;
Prof. Shadrack S.
Mwakalila, Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere;
Mheshimiwa Pius Msekwa,
Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano;
Waheshimiwa Mabalozi;
Ndugu Wanataaluma na
Wafanyakazi Waendeshaji wa Chuo;
Ndugu Wanafunzi;
Ndugu Wanajumuiya ya
Chuo;
Ndugu Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana.
Mheshimiwa
Waziri wa Elimu,
Ninakushukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi na
pamoja na Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Kivukoni kwa kunialika
Chuoni hapa siku ya leo. Nawapongeza kwa
uamuzi wenu wa busara wa kuanzisha Programu Maalum ya Mafunzo ya Uongozi na
kuizindua leo tarehe 13 Aprili, 2015 siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa Hayati Baba
wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere
miaka 93 iliyopita.
Pongezi kwa Chuo cha
Kumbukumbu ya
Mwalimu Nyerere
Ndugu Wageni Waalikwa;
Nakupongeza sana Kaimu Mwenyekiti
wa Bodi ya Chuo, Mkuu wa Chuo, wakufunzi na wafanyakakazi wote kwa kazi nzuri
mnayoifanya na kwa mafanikio yanayoendelea kupatikana hapa Chuoni. Katika miaka 10 ya uhai wake Chuo kimekua
sana. Kama alivyoeleza Mkuu wa Chuo, mmefungua
tawi kule Zanzibar na sasa mnadahili wanafunzi 4,000 hapa Kivukoni na 2,400
kule Zanzibar. Aidha mnaendesha mafunzo ya ngazi za awali (foundation), cheti,
stashahada na shahada hapa Kivukoni na katika Tawi la Zanzibar. Nawapongeza
sana kwa upanuzi huu mkubwa.
Programu ya Uongozi na
Maadili
Ndugu Mkuu wa Chuo;
Nakosa maneno mazuri ya kuelezea
furaha yangu kwa uamuzi wenu wa kuanzisha Programu Maalum ya Uongozi na
Maadili. Nafurahi kuwa mnafanya moja ya mambo muhimu yaliyokuwa yanafanywa na
Chuo cha Kivukoni wakati ule kabla ya kuwa Chuo cha Sayansi ya Jamii cha
Kivukoni na sasa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere.
Napenda mjue kwamba hapa palikuwa
hoteli iliyoitwa Ghana Hotel. Mwaka 1961,
hoteli hiyo ilinunuliwa na kuanzishwa Chuo cha Kivukoni ambacho madhumuni yake
ni kuwaendeleza kwa elimu na mafunzo vijana wa kiafrika ambao hawakupata elimu
nzuri. Walengwa hasa walikuwa vijana
waliojiunga na harakati za kudai uhuru ili waweze kujiendeleza maishani. Miongoni mwa wanufaikaji ni pamoja na hayati
Kighoma Malima ambaye aliacha shule darasa la 10 na kushiriki harakati za kudai
Uhuru. Alikuja Chuoni hapo akaendelezwa
na baadaye kwenda Marekani kusoma zaidi na hata kufikia kuwa mchumi bingwa
aliyetambulika kimataifa.
Chuo kilianza kwa kufundisha masomo
ya sayansi ya jamii na walimu wake walikuwa wa kutoka nje hususan Uingereza,
Canada na Marekani. Ilikuwa hivyo kwa
sababu wasomi wazalendo walikuwa wachache sana.
Baadaye ndipo walipoajiriwa kidogo kidogo mpaka hatimaye wazungu walipoondoka.
Baada ya Azimio la Arusha, Mwalimu
Nyerere aliagiza Chuo kifundishe Azimio hilo kwa viongozi wa Chama na Serikali. Mwaka 1972
Chuo kikabadilika kabisa na kuwa cha mafunzo ya siasa na uongozi. Kwa ajili hiyo, viongozi wa ngazi mbalimbali
wa Chama wakati ule, Serikali na taasisi zake wakiwemo wa vyombo vya ulinzi na
usalama na mashirika ya umma walipitia Kivukoni. Walipatiwa mafunzo ya siasa, ya uongozi maadili. Mimi ni mmoja wa wanafunzi waliopitia na
kuhitimu katika Chuo hiki. Lengo lilikuwa
ni kuwawezesha kuwa viongozi wanaoweza kutimiza ipasavyo majukumu yao uongozi
katika taifa linalojitegemea na la kijamaa.
Viongozi pia ambao ni waadilifu wanaotambua na kuheshimu miiko ya
uongozi. Katika mafunzo yale miiko ya
uongozi kwa mujibu wa Azimio la Arusha yalikuwa yanafundishwa.
Baada ya mageuzi ya kiuchumi na ya
kisiasa, na Chama cha Mapinduzi kuachana na vyuo vya siasa, kukatokea ombwe
kubwa kwa upande wa mafunzo ya uongozi. Si
vyema kuhoji busara ya uamuzi wa Chama lakini athari zake sote tunaziona. Kumekuwepo na kilio na manung’uniko kuhusu maadili
na mienendo ya viongozi. Tumeshuhudia viongozi wakifanya matendo ya utovu wa
maadili na hata kutumia lugha zisizofanana na uongozi ulio adilifu. Hivyo,
uamuzi wenu huu umekuja wakati mwafaka sana.
Ni uamuzi uliokuja wakati unahitajika sana.
Mkuu
wa Chuo;
Mabibi
na Mabwana;
Wanazuoni wamekuwa na mjadala kwa
karne nyingi kuhusu uongozi na hayajakamilika.
Moja ya mambo yanayowashughulisha wanazuoni ni kama viongozi huzaliwa na
vipaji vya uongozi au huandaliwa kwa mafunzo kuwa viongozi. Huu ni mjadala unaoendelea hata
sasa katika fani ya sayansi ya siasa. Tafiti nyingi zimeonyesha kuwa pamoja na
kuwepo ushahidi kuwa wako viongozi wenye kuzaliwa na vipawa na karama za
uongozi, hata hivyo, ubora wa viongozi, hata kwa wale waliozaliwa na vipawa na
karama zao hutokana na mafunzo. Inaweza
kuwa mafunzo darasani au kwa kuona na kwa kutenda. Bahati mbaya hatuna vyuo vya uongozi wa
jamii.
Mafunzo kwa viongozi ni muhimu kwa
kuwa huwapa nyenzo na ufunguo wa kuyaelewa mazingira wanayoongozea, historia na
uzoefu wa eneo wanaloliongoza, watu wanaowaongoza, matarajio yao, hulka zao,
changamoto zao na muhimu sana maadili na miiko ya uongozi wenyewe. Hali
kadhalika, uadilifu katika uongozi, hujumuisha desturi na tabia zinazokubalika
na zinazotarajiwa na jamii na wananchi kutoka kwa kiongozi. Wananchi
hawamtegemei kiongozi kuwa mla rushwa, mlevi, mhuni, mwongo au asiye na uhusiano
mzuri na watu.
Maadili na miiko ya uongozi vinapaswa
kuzingatiwa na viongozi wote katika jamii na taifa bila ya kujali vyama vya
siasa. Kiongozi asiye na uelewa huu, hupwaya
katika uongozi. Maadili na miiko ya uongozi ni tunu muhimu sana kwa kiongozi
yeyote. Kiongozi anapaswa awe mtu mwenye uadilifu usiotiliwa shaka utakaomfanya
aaminiwe na awe na mamlaka ya kimadili
(moral authority) juu ya wale anaowaongoza.
Katika miaka hii 10, tumejishughulisha
sana na masuala ya maadili katika uongozi na utendaji Serikalini. Tumefanikiwa
kuimarisha mifumo ya kusimamia maadili ya viongozi kwa kutunga Sheria, Kanuni
na Taasisi za kufuatilia mienendo ya viongozi. Tumeimarisha Sekretariati ya
Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kuipa uwezo wa kiuchunguzi, rasilimali watu na
vitendea kazi. Tumelipa meno Baraza la Maadili na tumeliona kwa mara ya kwanza
likiwaita na kuwahoji viongozi wenye tuhuma za kimaadili.
Mwaka 2009 tumetunga Sheria Mpya ya
Rushwa iliyoboreshwa na kuongeza nguvu kupambana na rushwa. Orodha ya makosa ya rushwa imeongezwe kutoka manne
hadi 24 na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imeimarishwa
kwa majengo, vifaa na rasilimali watu. Hivi sasa TAKUKURU iko katika wilaya
zote nchini na watuhumiwa wengi wa rushwa wamefikishwa katika mahakama na fedha
nyingi zimekuwa zinaokolewa.
Vilevile, tumetunga Sheria ya
Matumizi ya Fedha katika Uchaguzi ili kuhakikisha kwamba maadili ya kupata
viongozi wa kuchaguliwa katika taifa letu yanazingatiwa. Tutakapokamilisha
Sheria ya kutenganisha shughuli za siasa na biashara tutakuwa tumepiga hatua
kubwa. Tumetunga pia Sheria mpya ambayo
imeimarisha Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). Imesaidia kuimarisha nidhamu ya matumizi ya
fedha za umma na kuwabana viongozi na watumishi wa umma wanaofanya vitendo vya wizi
au ubadhilifu wa fedha na mali za umma. Yote
haya tumeyafanya ili kuimarisha mifumo ya kusimamia maadili ya viongozi na
watendaji wetu.
Bahati nzuri katika Katiba Inayopendekezwa,
Bunge Maalumu la Katiba limesisitiza na kuweka uzito unaostahili kwa maadili ya
viongozi na watendaji wa umma. Ibara 28 na 29 inazungumzia maadili ya
viongozi wa umma, na ibara 30 na 31 inazungumzia maadili ya watendaji wa
umma. Katiba Inayopendekezwa ikipitishwa
tutakuwa tumefanikiwa sana katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maadili
nchini. Ombwe lililoachwa na Azimio la
Zanzibar kuhusu miiko ya uongozi litakuwa limepata jawabu la uhakika.
Ni ukweli usiopingika kuwa pamoja na jitihada
hizo, leo hii tunayo nakisi ya maadili miongoni mwa viongozi na watendaji wa
umma. Funzo tunalolipata hapa ni kuwa
kukinga ni bora kuliko kutibu. Mifumo ya udhibiti pamoja na umuhimu wake, si
badala ya mifumo ya kuwaandaa viongozi kimaadili. Zamani kupitia Jeshi la
Kujenga Taifa (JKT) na Chuo cha Kivukoni zilikuwa sifa muhimu za kupata uteuzi
wa uongozi wa siasa. Baada ya mageuzi ya
kiuchumi na kisiasa na kuingia kwa mfumo wa soko huria na vyama vingi, mambo
hayo hayakupewa umuhimu. JKT ikadorora,
vijana wakakosa fursa ya kujengwa uzalendo.
Ukichanganya na Azimio la Zanzibar lililolegeza miiko ya uongozi ya
Azimio la Arusha, kumekuwa na mmong’onyoko mkubwa wa maadili miongoni mwa
viongozi. Kufa kwa Chuo cha Kivukoni
kumeshusha ubora wa uongozi.
Baada ya kurejesha JKT, hakika, taifa
linahitaji sana programu ya aina hii tunayozindua leo ili kutuandalia viongozi wazuri,
wenye mtazamo wa kitaifa na maadili mema. Nasema hivyo kwa kuwa sote ni mashuhuda
wa matatizo ya maadili ya uongozi nchini.
Hatuna budi kuwaandaa viongozi wetu
hasa vijana kwa mafunzo maalumu ili waje kuwa viongozi bora. Ni jambo ambalo
tulikuwa tukilifanya siku za nyuma. Uzoefu unaonyesha hata katika nchi zilizoendelea
wanafanya hivi. Viko vyuo maalum vinavyoandaa na kutoa viongozi wa kada
mbalimbali. Katika nchi za wenzetu kuna ngazi fulani za uongozi huwezi kushika
ikiwa hujafundwa katika taasisi maalumu. Kwa kuzingatia ukweli huo, ndiyo maana
tumeanzisha Chuo cha Uongozi kiitwacho Uongozi Institute. Chuo hiki kinalenga kutoa mafunzo ya uongozi
kwa viongozi wa Serikali. Wamekuwa
wakitoa mafunzo kwa Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa na viongozi wengine wa
ngazi mbalimbali.
Nimefurahishwa na taarifa yako kuwa
kutakuwa na Kada za aina tatu katika mafunzo ya program hii yaani ngazi ya juu
yenye viongozi na watendaji wa kitaifa
na mkoa;ngazi ya kati itakayohusisha viongozi wa ngazi ya wilaya; na ngazi ya
chini yenye viongozi wa ngazi za kijiji. Aidha, umesema yatakuwa ni mafunzo ya
muda mfupi. Nakubaliana nanyi kwani si vyema kuziacha nafasi hizi wazi kwa muda
mrefu. Vile vile, ni muhimu sana mafunzo haya yakaegemea pia katika vitendo na
uzoefu badala ya nadharia pekee. Hii inajumuisha kuwa na wakufunzi mchanganyiko
kutoka katika taaluma na wale kutoka katika uongozi na utendaji wa fani
mbalimbali.
Uamuzi wenu wa kuanzisha Kibweta
cha Mwalimu Nyerere kwa madhumuni ya kusimamia program ya mafunzo haya ni
mzuri. Nimefurahishwa pia na uteuzi wenu wa Mheshimiwa Pius Msekwa kuwa
Mwenyekiti wa Kibweta hiki. Chaguo hili ni muafaka kwani amesheheni historia,
uzoefu na hazina kubwa ya uongozi. Ni imani yangu kuwa chini ya uongozi wake programu
hii itafanikiwa. Sisi katika Serikali tunaahidi kuwapa kila aina ya ushirikiano
mtakaohitaji. Tuleteeni mapendekezo yenu kuhusu program hii ili ifanyiwe kazi
na tuanze kuleta viongozi kwa ajili ya mafunzo hayo.
Changamoto za Chuo
Mkuu
wa Chuo;
Kama ulivyoeleza, kukua na kupanuka
kwa Chuo hiki kumekuja na changamoto zake. Idadi ya wanafunzi inaongezeka
wakati majengo ya hosteli ni finyu. Umezungumzia ujenzi wa hosteli kusimama
kutokana na uhaba wa fedha. Nitawasaidia
kusema. Kuhusu kupewa majengo ya TAFICO
ili myabadili matumizi na kuyatumia kwa kufundishia itabidi kushauriana na
wenye majengo kujua mipango yao na mahali hapo.
Kama itawezekana tutawapeni taarifa.
Kuhusu tatizo la mmomonyoko wa fukwe unaotokana na kuongezeka kwa bahari
tutawasiliana na mamlaka husika utafiti ufanywe na ushauri wa kitaalamu utolewe.
Nikuhakikishie kuwa nimepokea
changamoto zenu na ni changamoto za msingi na tutatazama moja baada ya nyingine
tuone namna ya kujenga Chuo hiki kulingana na mahitaji yake ya sasa na ya siku
za usoni.
Hitimisho
Mabibi
na Mabwana;
Niwashukuru sana kwa kunialika
katika maadhimisho ya kumbukumbu ya kuzaliwa Mwalimu Nyerere na ufunguzi wa
Programu Maalum ya Uongozi na Maadili. Nimefurahi
sana kujumuika na nanyi wote katika eneo hili ambalo linanikumbusha nilipokuwa
nikihudhuria mafunzo katika chuo hiki. Sasa ninayo furaha kutangaza kuwa
Programu Maalum ya Mafunzo ya Uongozi na Maadili imefunguliwa rasmi.
Asanteni sana kwa kunisikiliza.
0 comments:
Post a Comment