Image
Image

Rais Kikwete asema hajapokea wala kuletewa majina ya watu 16 waliohukumiwa kifo kutokana na mauaji ya Albino.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa hajaletewa majina ya watu 16 waliohukumiwa kifo kutokana na mauaji ya maalbino nchini kwa sababu safari ya kisheria ya majina hayo kufikishwa kwake ni ndefu.

Rais Kikwete aliyasema hayo jana, Jumapili, Aprili 12, 2015  wakati alipozungumza katika ibada maalum ya kuwekwa wakfu na kusimikwa kwa Askofu Liberatus Sangu kuwa Mhashamu Baba Askofu wa Jimbo la Kanisa Katoliki la Shinyanga. 
Akizungumza katika ibada hiyo iliyofanyika kwenye Kanisa Kuu la Mama Mwenye Huruma, Ngokolo, mjini Shinyanga na mbele ya viongozi wengi wa Kanisa hilo wakiwemo maaskofu wakuu, maaskofu na maaskofu wasaidizi 38, Rais Kikwete alitumia nafasi hiyo kujibu madai kuwa Serikali yake haichukui hatua za kutosha kukabiliana na mauaji ya albino na pia kufafanua juu ya shinikizo ambalo linatolewa na baadhi ya mashirika yasiyokuwa ya serikali (ngo’s) yakimtaka Rais kutia saini ya kuruhusu watu hao wanyongwe. 
Rais Kikwete aliwaambia viongozi hao wa dini: “Ninayo maombi maalum kwenu viongozi wa dini. Naomba mtusaidie kuielimisha jamii ili iachane na imani za kishirikina. Vikongwe wanauawa kwa sababu tu ya kuwa na macho mekundu na ujinga uliokithiri unaosababisha Watanzania wenzetu wenye ulemavu wa ngozi  (albino) kusakwa na kuuawa kikatili kabisa.” 
“Nawaombeni sana viongozi wa dini tusaidiane katika kukomesha ujinga huu mkubwa kwa kutoa elimu kwa waumini wenu, ili wajue kuwa vikongwe wana macho mekundu kwa sababu ya kutumia samadi ya ng’ombe kupikia kwa muda mrefu na kuwa kiungo cha albino hakiweza kuleta utajiri wowote,” Rais aliwaambia viongozi hao wa dini. 
Kuhusu madai kuwa Serikali yake haichukui hatua za kutosha kukabiliana na mauaji ya albino, Rais Kikwete aliwaambia viongozi hao: “Tumewatia mbaroni watuhumiwa wengi wa mauaji ya albino. Watu 16 tayari wamehukumiwa kifo na wengine wanasubiri…kesi zao zinaendelea kusikilizwa. Yapo maneno maneno, lakini binafsi kama Rais sijaletewa majina ya watu hao.” 
Aliongeza: “Ni lazima tuelewe jinsi mfumo wetu wa kutoa haki unavyofanya kazi hasa katika eneo hilo la kunyonga ama kutokunyonga. Ni mlolongo mrefu. Katika kesi za watu kuhukumiwa kifo, kwanza kukata rufani ni lazima na wala siyo jambo la hiari ama matakwa ya aliyehukumiwa.  Pili, tukimalizana na rufani ni lazima Kamati ya Msamaha (Committee on Prerogative of Mercy) nayo ifanye kazi. Kwa hiyo ni utaratibu mrefu kidogo.” 
Mhashamu Baba Askofu Sangu ambaye aliteuliwa na Baba Mtakatifu Francesco kuwa Askofu Februari 2, mwaka huu, 2015, amechukua nafasi ya hayati Baba Askofu Aloysius Balina ambaye alifariki dunia Novemba 6, 2012. 
Wakati wa uteuzi wake, Mosinyori Sangu alikuwa anafanya kazi kwenye Idara ya Uenezaji Injili Ulimwenguni katika makao makuu ya Kanisa Katoliki, Vatican ambako alifanya kazi kwa miaka minane. 
Mwisho. 
Imetolewa na;

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu – Dar es Salaam.

13 Aprili,2015
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment