Image
Image

SAKATA la uchunguzi wa mkataba tata wa LUGUMI ngoma nzito

SAKATA la uchunguzi wa mkataba tata kati ya Kampuni ya Lugumi Enterprises na Jeshi la Polisi, bado ni kitendawili baada ya kamati ndogo iliyoundwa kulichunguza, kushindwa kukabidhi ripoti juzi kutokana na masuala kadhaa kutokamilika.
Awali, Mwenyekiti wa kamati ndogo hiyo iliyoundwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuchunguza utekelezaji wa mkataba huo, Japhet Hasunga, aliiambia Nipashe kuwa ripoti hiyo ilitarajiwa kukabidhiwa kwenye ofisi ya Spika mjini Dodoma juzi Jumamosi, lakini "imeshindikana."
Kampuni hiyo ilikuwa inatekeleza mradi wenye thamani ya Sh. bilioni 37 wa kusimika mfumo wa utambuzi wa alama za vidole kwenye vituo vya polisi nchini.
Aprili 23, mwaka huu, PAC iliunda kamati ndogo ya watu tisa kuchunguza utekelezaji wa mradi huo na taarifa yake kuwasilishwa bungeni.
PAC ililazimika kuunda kamati hiyo ndogo baada ya kushindwa kupata ufafanuzi wa kina kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Meja Jenerali Projest Rwegasira na maofisa wengine wa Jeshi la Polisi iliyowahoji kwenye ofisi za Bunge Aprili 20, mwaka huu kuhusu sakata hilo.
Baada ya kumaliza uchunguzi wake, kamati ndogo ya PAC yenye wajumbe (wabunge) watano wa CCM na wanne kutoka upinzani (CUF na Chadema vikitoa wajumbe wawili kila kimoja), ilirejea bungeni mjini hapa Mei 24, mwaka huu,
huku ikiahidi kukabidhi ripoti ya uchunguzi, Jumamosi iliyopita.

Hata hivyo, katika mahojiano maalum na Nipashe jana mchana, mwenyekiti wa kamati hiyo (Hasunga) alisema walishindwa kuikabidhi ripoti yao kwenye ofisi za Spika kutokana na changamoto kadhaa zilizojitokeza wakati wakiiandika.
"Tulipanga tuikabidhi jana (juzi), lakini tulishindwa baada ya kuibuka mambo kadhaa," alisema Hasunga.
Aliongeza kuwa: “Kama unakumbuka vizuri, tulikuwa tumegawanyika katika makundi matatu wakati wa uchunguzi, tulipokutana kuna vitu vilijitokeza, tukaona tusiikabidhi, tuvute subira kidogo ili vitu hivyo tuviandike kwa kina zaidi.

“Ni matarajio yetu mwishoni mwa wiki lijalo, tutakuwa tumeshaifikisha mbele ya meza ya Spika kwa kushirikiana na wajumbe wengine wa PAC ili iwasilishwe bungeni na
kuanikwa kwa maslahi ya umma.”

Aidha, Hasunga, ambaye hakuwa tayari kuweka wazi waliyoyabaini katika uchunguzi wao, alisema kamati yake ilipata ushirikiano mkubwa wakati wa uchunguzi wa utekelezaji wa mradi huo ambao umekuwa ukidaiwa kuwagusa baadhi ya ‘vigogo’ wa serikali akiwamo aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga.
Kitwanga ambaye uteuzi wake ulitenguliwa na Rais John Magufuli, Mei 20, mwaka huu kutokana na ulevi, anahusishwa na mkataba wa utekelezaji wa mradi huo kupitia kampuni yake ya Infosy ambayo ilipewa zabuni ya kusambaza vifaa na Kampuni ya Lugumi.
Mwanzoni mwa mwezi uliopita, PAC ilieleza kuwa Kampuni ya Lugumi ililipwa Sh. bilioni 34 na Jeshi la Polisi ili kufunga vifaa hivyo katika vituo 138 vya polisi nchini, lakini ni vituo 14 tu ndivyo vilivyokuwa vilivyokuwa vimefungiwa, licha ya kulipwa fedha hizo ambazo ni sawa na asilimia 90 ya malipo yote ya kazi hiyo.
    Share on Google Plus

    Kuhusu TAMBARARE HALISI

    This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

    0 comments:

    Post a Comment