Image
Image

Uchaguzi Mkuu ujao wawekewa masharti.

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) pamoja na vyama vya siasa 22 imepitisha maadili yatakayotumika katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Pia vyama vya siasa vimeshinikiza kuwa Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), awe sehemu ya maadili hayo kuepuka jeshi lake kunyanyasa viongozi na wafuasi wa vyama vya siasa.
Katika mkutano wa kujadili maadili hayo jana, Mwenyekiti wa NEC, Jaji Damian Lubuva alisema maadili hayo yatahusisha zaidi vyama vya siasa, wagombea wote, Serikali pamoja na Tume yenyewe, jambo ambalo viongozi wa vyama vya siasa walisema kwa upande wa Serikali, anayehusika zaidi ni IGP.
Maadili hayo yanavitaka vyama vya siasa na wagombea wake kuheshimu, kutekeleza sheria za uchaguzi, kanuni, maadili na sheria nyingine za nchi katika kipindi chote cha uchaguzi yaani kuanzia kampeni hadi siku ya uchaguzi.
Mawaziri, watendaji
Kwenye maadili hayo, mawaziri wametakiwa wasichanganye ziara za kikazi na shughuli za kiuchaguzi na wasitumie vyombo au watendaji wa Serikali katika shughuli za uchaguzi kwa manufaa yao.
Kuanzia kipindi cha kampeni, mawaziri na watendaji wengine wa Serikali hawatakiwi kutangaza katika vyombo vya habari au kwa namna yoyote misaada au ahadi ya aina yoyote, kutoa ahadi za shughuli za maendeleo ya jamii kwa mfano kujenga barabara, kusambaza maji na wasitumie rasilimali za umma kwa shughuli za kampeni.
Maadili hayo pia yanaeleza mambo ambayo hayatakiwi kufanywa na vyama vya siasa na wagombea, mambo yanayotakiwa kufanya au kutofanywa wakati wa upigaji kura mpaka kutangaza matokeo ya uchaguzi, wajibu wa Serikali na Tume ya Uchaguzi.
Miongoni mwa mambo ambayo yanakatazwa na maadili hayo ni wafuasi wa vyama vya siasa kufanya fujo au kusababisha vurugu ya aina yoyote katika mkutano wa chama kingine cha siasa.
Wafuasi vituoni
Pia wafuasi wa vyama vya siasa, wametakiwa kuondoka vituoni mara tu baada ya kupiga kura, ili kuepusha msongamano na vitendo vingine vinavyoweza kuchochea kuvunjika kwa amani.
Jaji Lubuva pia alisema maadili hayo yanaitaka Serikali wakati wa uchaguzi kutoa fursa sawa kwa wadau wote, ikiwemo vyama vya siasa, ili kuviwezesha kuendesha shughuli zao za kisiasa kwa kuzingatia sheria za nchi, ikiwemo kuruhusu wagombea urais kutumia vyombo vya habari vya umma katika kutangaza sera zao.
Aidha mawakala wa vyama vya siasa, wamezuiwa kutumia simu za viganjani wawapo katika kituo cha kupiga kura, kwa kuwa waliohudhuria wametamkwa kabisa katika maadili hayo.
Goli la mkono
Hata hivyo, mkutano huo nusura uingie dosari, baada ya baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa kuonesha wasiwasi wao kuwa maadili hayo hayana maana, kwani tayari CCM kupitia kwa baadhi ya viongozi wao wameshaapa kuwa watashinda hata kwa goli la mkono.
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema kama maadili hayo yanataka vyama vyote kufuata sheria, inakuwaje Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye ajitape kuwa lazima chama chake kitashinda hata kwa goli la mkono na NEC yenyewe imekaa kimya.
“NEC mko kimya, IGP yuko kimya na msajili ya vyama vya siasa yuko kimya, hivi kweli hapo kuna haki itatendeka, je haya maadili ni mapambo? Alihoji Dk Slaa.
Dk Slaa pia alihoji inakuwaje wanaenda kujadili maadili wakati hata sasa mgawanyo wa majimbo haueleweki jambo ambalo limefanya kuwe na vurugu ndani ya vyama vya siasa. Alihoji tume inasubiri nini kutangaza majimbo hayo mapya.
Mwenyekiti wa Chama cha NLD, Dk Emmanuel Makaidi naye alisema maadili hayo hayana maana kama chama tawala kimeanza kutoa kauli ambazo zinaonesha kuwa wamejipanga kuvuruga uchaguzi, jambo ambalo linakatazwa na maadili hayo.
“Hapa tunafanya nini kama chama tawala kimeshaanza kutoa kauli hizo halafu mnataka mtuaminishe kuwa uchaguzi utakuwa huru na haki,” alisema Dk Makaidi.
NEC yajitenga
Hata hivyo Jaji Lubuva alisema maadili hayo yanahusika siku ya kwanza ya kampeni hadi siku ya kupiga kura na kutangaza matokeo.
Alisema tume yake haihusiki na kauli hizo kwani hawana mamlaka yanayowapa kulizungumzia mambo ambayo yako nje ya sheria ya uchaguzi.
“Kuna vyombo vingine vinavyoshughulika na nyinyi kabla ya kampeni, sisi tunahusika wakati wa kampeni tu, hivyo hayo mengine hayatuhusu,” alisema Jaji Lubuva.
Kuhusu majimbo mapya, Jaji Lubuva alisema bado wako kwenye mchakato wa kukamilisha kuunda majimbo hayo mapya na hivi karibuni watatangaza na kuwataka viongozi wa vyama vya siasa kuwa na subira.
IGP na maadili
Makamu Mwenyekiti wa CCM, Phillip Mangula pamoja na Dk Slaa, ndio waliotoa hoja ya kutaka IGP awemo kwenye maadili hayo ili kuepusha malalamiko kutoka kwa wanasiasa hao kuwa jeshi hilo linakwepa kushughulika na kesi za kisiasa.
Dk Slaa katika hoja yake alisema katika uchaguzi uliopita, walipata shida na polisi kwani kila walipokuwa wanapeleka kesi zinazotokana na kampeni, polisi walikwepa kuwa hawashughuliki na masuala ya kisiasa.
Mangula kwa upande wake alisema anaunga mkono hoja ya Dk Slaa kuwa IGP lazima naye awe sehemu ya maadili hayo, ili kuondoa malalamiko ya wanasiasa na ajue namna atakavyowajibika wakati wote wa kampeni za uchaguzi.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment