JANA Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Sadiki amekaririwa akisema
idadi ya wagonjwa wa kipindupindu katika mkoa huo imefikia 635 huku
akisema umekuwa tishio kwani tayari watu 10 wamepoteza maisha kutokana
na ugonjwa huo.
Akizungumza na waandishi mkoani humo, Sadiki alisema kati ya wagonjwa
hao, Wilaya ya Kinondoni inaongoza kwa kuwa na wagonjwa 523. Kutokana
na hali hiyo, alipiga marufuku uuzaji wa vyakula shule za sekondari na
msingi ili kuzuia ugonjwa huo.
Mkuu huyo wa mkoa alisema tangu kuanza kwa ugonjwa huo mwezi uliopita
kumekuwa na madhara makubwa tofauti na ilivyotarajiwa awali. Ni kweli
kabisa kwamba mlipuko wa ugonjwa huo ulipoanza hakuna aliyedhani
utaendelea kushika kasi hadi sasa.
Pia, ugonjwa huo umedumu kwa muda mrefu katika mkoa huo tofauti na
miaka mingine hali ambayo inazidi kuumiza vichwa vya wengi. Kinachoumiza
vichwa ni kwamba hakuna mvua zinazonyesha, lakini ugonjwa huo unazidi
kusimika mizizi.
Chanzo kikubwa tunaambiwa ni maji yasiyo salama. Hili nalo ni suala
ambalo halikutakiwa kuendelea katika mkoa huo kwa sababu ndipo roho ya
nchi ilipo. Kwa msingi huo tuliamini mitandao ya maji ilitakiwa iwe
katika mazingira bora tofauti na ilivyo sasa.
Haingiii akilini katika karne hii watu wapoteze maisha kwa kunywa
maji machafu. Pia, haiingii akilini ugonjwa kama huo usimike mizizi
katika eneo ambalo watu wanaamini kunaishi watu waliostarabika na wenye
upeo mpana wa mambo.
Kama Dar es Salaam inakuwa hivyo pembeni mwa nchi hali itakuwaje. Kwa
hili tunasema hapana. Ni lazima mtu mmoja mmoja awajibike katika kupiga
vita ugonjwa huo. Ni lazima uongozi wa mkoa useme hapana. Ni lazima
ukiri kuna tatizo au uzembe mahali.
Haiwezekani eneo ambalo wataalamu wapo kila kona halafu ugonjwa huo
uendelee kusambaa. Mungu aepushe mbali tatizo hilo liondoke mapema
vinginevyo hali si shwari. Mamlaka husika ni lazima ziwajibike. Tabia ya
kufungia maofisini haitamaliza tatizo. Ni lazima watendaji wajipanue.
Ni matarajio yetu uongozi utawajibika inavyotakiwa na kuhakikisha
mkoa unakuwa na uhakika wa maji safi na salama. Ni lazima viongozi
wahakikishe suala la usafi linatiliwa mkazo, vinginevyo mkoa huu
unakwenda kubaya. Mwenye masikio na asikie.
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)


0 comments:
Post a Comment