Taasisi ya vyombo vya habari kusini mwa Afrika
tawi la Tanzania (MISA-TAN) na Baraza la Habari tanzania (MCT) imezikumbusha
serikali za Afrika Mashariki kuendeleza haki na uhuru wa vyombo habari ikiwa ni
utekelezaji wa tamko la ulimwengu la haki za binadamu na kulinda misingi ya
utawala wa sheria wa kidemokrasia kwenye ukanda huo.
Aidha vyombo hivyo vimesema kwamba ni wajibu wa
serikali hizo kuhakikisha kwamba kila mtu anao uhuru wa kutoa maoni au
kujieleza pamoja na kupata habari bila ya kuingiliwa.
Mwenyekiti wa MISA-TAN, Mohammed Tibainyendera na
Meneja Maadili na Usuluhishi wa MCT Allan Lawa wakizungumza kwenye uzinduzi wa
Tamko la Mount Meru juu ya uhuru wa vyombo habari, pia wamehimiza umuhimu wa
uboreshaji wa maslahi ya waandishi wa habari pamoja na kuwahakikishia mazingira
bora na salama katika utekelezaji wa majukumu yao kila siku.
Rais wa chama cha wanasheria Tanganyika (TLS)
Francis Stolla akizungumza mara baada ya kuzindua tamko hilo la wanahabari
ameahidi kufanya kazi na waandishi wa habari ikiwa ni pamoja na kutoa msaada wa
kisheria bila malipo.
Tamko hilo la Mount Meru ambalo lilitolewa siku
ya uhuru wa vyombo vya habari duniani kwa mwaka huu mkoani Arusha pamoja na
mambo mengine limelaani vikali ongezeko la kuwashambulia kuumizwa na kuuawa kwa
waandishi wa habari katika ukanda wa Afrika Mashariki.


0 comments:
Post a Comment