Nchi 5 za Afrika zimeiandikia barua Mahakama ya
Kimataifa ya Jinai (ICC) zikiitaka imruhusu Makamu wa Rais wa Kenya, William
Ruto kuwakilishwa mahakamani na mawakili wake ili apate fursa ya kutekeleza
majukumu yake ya kikatiba nchini mwake.
Nchi hizo ambazo ni Tanzania, Burundi, Rwanda, Uganda
na Eritrea pia zimeitaka ICC kubadilisha kifungu cha 63 cha mkataba wa Roma
kinachosisitiza kuweko mahakamani mshukiwa wakati wa kusilikizwa kwa kesi yake.
Habari za kuminika za karibu na mahakama hiyo ya kimataifa zinasema Umoja wa Afrika (AU) pia
umeandika rasmi barua kama hiyo kuhusiana na kesi ya William Ruto.
Makamu wa Rais wa Kenya alikuwa mjini Hague, kuanzia
Jumatatu iliyopita wakati kesi yake ilipoanza kusikizwa Septemba 10.
Hata hivyo alilazimika kurudi nyumbani siku ya Alhamisi baada ya Mwendesha Mashtaka wa
ICC, Bi. Fatou Bensouda kuomba kesi isitishwe kwa muda wa wiki moja ili kumpa
nafasi ya kupanga mashahidi.
Nchi za Afrika zimekosoa Mahakama ya ICC kutokana na
kile kinachotajwa kuwa ni ubaguzi wa kisheria.
Nchi nyingi barani humo
zinaamini kwamba ICC inatumiwa kisiasa na nchi za Magharibi ili kufikia malengo
fulani.


0 comments:
Post a Comment