Image
Image

Cosafa imeipa fundisho Taifa Stars.


Matokeo mabaya ambayo timu yetu ya soka ya Taifa, Taifa Stars imeyapata kule Afrika Kusini ilikoshiriki mashindano ya Kombe la Cosafa  na kutolewa mapema kwa hakika yanasikitisha, pia yanaumiza.
Timu hiyo iliyoshiriki ikiwa mwalikwa pamoja na Black Stars ya Ghana, ilikwenda kwa matumaini ya  kuongeza chachu na ushindani kwenye mashindano hayo ya Kanda yanayoshirikisha nchi kutoka Kusini mwa Afrika zinazounda shirikisho la Cosafa.
Tunawapongeza Cosafa  kwa kuipa heshima kubwa nchi yetu na nafasi ya kupeleka timu ili kushiriki mashindano hayo, hata kama imeondolewa mapema, tena kwa aibu ya aina yake ya kufungwa mechi zote tatu.
Tunaamini, kutolewa kwa Stars baada ya kufungwa mabao manne bila kupata hata bao moja ni changamoto kubwa, hasa kwa benchi la ufundi la timu hiyo chini ya kocha Martin Ignatius au Mart Nooij na matokeo hayo yamethibisha kwamba soka ni mchezo mgumu unaochezwa uwanjani, wala si kwa maneno.
Tunasema imepata fundisho ambalo Nooij na vijana wake watalitumia kwenye mashindano mengine ambayo timu hiyo inashiriki mwaka huu.
Tunatambua kuwa Stars haikuwa mtalii kule Afrika Kusini, bali safari hiyo ilitosha kuwapa somo wachezaji wake na Watanzania kwa jumla kuhusu soka na jinsi inavyochezwa kwa sasa ulimwenguni.
Tunashawishika kuamini kuwa Nooij, kocha ambaye ana uzoefu mkubwa baada ya kuifundisha kwa mafanikio Mambas ya Msumbiji, atakuwa amejifunza kitu kutoka kwenye mashindano hayo, hata kama timu yake imeaibishwa kwa vipigo vitatu.
Tunasema, wachezaji wetu walioshiriki mashindano hayo watakuwa wamefunguka macho na kutambua wapi walikosea, wapi wanahitaji marekebisho, wanapojiandaa kuikabili Misri, timu ngumu na yenye ubora zaidi kuliko zilivyo Swaziland, Madagacar na Lesotho, ambazo zimeifunga Stars.
Kwa maana hiyo, tunaamini hakuna sababu ya kuanza kusaka mchawi na badala yake, Nooij na msaidizi wake, Salum Mayanga na Mkurugenzi wa Ufundi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Salum Madadi lazima wakae chini kuangalia wapi Stars ilikosea, idara ipi inahitaji marekebisho na kuyafanyia kazi haraka iwezekanavyo.
Pia, tunaamini kuwa benchi hilo la ufundi litaangalia kwa mfano, sehemu zote zilizopwaya, kwenye ulinzi, ushambuliaji au timu nzima, si kwa lengo la kuifumua.
Tunashauri wairekebishe wakati wa kujiandaa na mechi dhidi ya Misri kusaka tiketi ya kushiriki Fainali za Mataifa ya Afrika mwaka 2017 huko Gabon.
Tunasema, Nooij na wenzake wakubali kuwa kuteleza si kuanguka na badala yake watumie mashindano ya Cosafa kuandaa timu ya ushindani inayoweza kucheza na Misri mwezi ujao, ambayo itakuwa imejifunza kutokana na makosa kule Afrika Kusini.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment