Image
Image

Kupunguza utegemezi kuendane na hali halisi.


Bajeti ya Serikali ya mwaka 2015/16 itaanza kujadiliwa wiki ijayo baada ya kusomwa bungeni mwishoni mwa wiki na Waziri wa Fedha, Saada Mkuya na baadaye Spika Anne Makinda kutoa siku za wabunge kuisoma kabla ya kuanza kuijadili.
Bajeti hiyo ni ya Sh22.49 trilioni na imelenga kupunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa fedha za nchi wahisani na wafadhili. Kwa mujibu wa hotuba hiyo ya bajeti, Serikali imepania kupunguza utegemezi huo hadi kufikia asilimia 8.
Pia, kwa maana hiyo, mkakati mkubwa utakuwa ni katika kusimamia makusanyo ya kodi na mapato mengine, hali kadhalika kukopa fedha kutoka taasisi mbalimbali kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
Uamuzi huo wa kupunguza utegemezi wa wahisani na wafadhili unatokana na Serikali kuona kuwa fedha hizo hazina uhakika, hasa wakati nchi hizo zinaposhinikiza Serikali kutekeleza jambo fulani kama walipozuia fedha wakati wakishinikiza suala la sakata la uchotwaji fedha kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow na lile la Epa.
Uamuzi huo umekuja wakati kukiwa na changamoto kubwa ya makusanyo ya mapato kutokana na Serikali kushindwa kufikia malengo yake, kushindwa kupata vyanzo vipya vya kodi na kushindwa kudhibiti wakwepa kodi.
Kwa mujibu wa bajeti hiyo, Serikali inatarajia kukusanya Sh12,363 bilioni kutoka kwenye mapato ya kodi na Sh1,112.7 bilioni kutoka kwenye mapato yasiyotokana na kodi.
Kwa tarakimu hizo tu ni dhahiri kuwa kuna kazi kubwa ya kukusanya fedha kufikia takriban nusu ya kiwango cha bajeti ili Serikali iweze kutekeleza sehemu kubwa ya miradi ya maendeleo na shughuli nyingine.
Kwa mujibu wa mjadala wa bajeti za wizara mbalimbali, Serikali haikuweza kupeleka fedha kwenye miradi mingi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha wa 2014/15, jambo lililolalamikiwa sana na wabunge wakisema maendeleo hayawezi kuja kwa shughuli za maendeleo kupata asilimia 30 tu ya fedha zilizopangwa.
Wasiwasi wetu ni kwamba hali itajirudia tena mwaka mpya wa fedha kwa Serikali kushindwa kukusanya fedha na hivyo kuzorotesha utekelezwaji wa miradi ya maendeleo, jambo ambalo kwa njia fulani litazidisha ugumu wa maisha kwa wananchi.
Ni vizuri kuondokana na utegemezi wa fedha kutoka kwa nchi wahisani, lakini uamuzi huo ni lazima uendane na hali halisi ya humu ndani na dhamiria ya kweli ya kuongeza juhudi za kukusanya mapato yanayotokana na yasiyotokana na kodi.
Kwa mfano, ingeanza kwanza mikakati ya kukusanya mapato kama ilivyoelezwa kwenye hotuba ya bajeti ambayo ni pamoja na kuwa na mikataba ya kiutendaji na Mamlaka ya Mapato (TRA) kuhakikisha watendaji wanafikia malengo na baada ya kuona mafanikio yake ndipo uamuzi wa pili wa kupunguza kiwango fulani cha utegemezi na hali kuendelea hivyo hadi pale tunapoona tumepunguza kwa kiasi kikubwa.
Juhudi za kupunguza matumizi yasiyo ya lazima pia zinatakiwa zifanyike kwa upana wake katika kuhakikisha kile kinachopatikana kinatumiwa vizuri na kwa shughuli zilizokusudiwa.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment