Image
Image

Ni muhimu wagombea urais kushiriki midahalo.


Taasisi ya CEO Roundtable imeandaa midahalo kwa ajili ya watu ambao wametangaza nia au kujitokeza kuwania urais kwa kupitia vyama tofauti, kwa kuanzia na CCM ambayo imeshaanza mchakato wa Uchaguzi Mkuu.
Mdahalo wa kwanza ulikuwa ufanyike Jumatatu wiki hii, lakini ukashindikana kutokana na waliojitokeza kuwania urais kupitia CCM na ambao walithibitisha kushiriki, hawakutokea wote na hivyo kusababisha usifanyike.
Waalikwa kwenye mdahalo huo wameshaeleza sababu za kutohudhuria kwao, hasa wakiegemea kukanganywa na kauli mbili tofauti zilizotoka kwa viongozi wao kuhusu msimamo wa chama na pia kubadilika kwa ratiba kulikosababisha waendelee na mipango mingine, hasa wakati huu ambao wanazunguka mikoani kutafuta wadhamini.
Ni sababu za msingi ambazo zinaeleweka. Inapotokea kiongozi mmoja anawakataza kushiriki midahalo hiyo kwa maelezo kuwa chama hakijapata mgombea urais, na saa 24 baadaye kiongozi mwingine akasema wahudhurie, ni lazima kauli hizo zitawachanganya na kusababisha waamue kuendelea na mipango mingine ili wasipoteze muda wakati huu muhimu kwao.
Lakini tunachotaka kueleza hapa si kufanyika au kutofanyika kwa mdahalo huo, bali umuhimu wa fursa hiyo katika kipindi hiki cha kuelekea kupiga kura kuamua maisha ya Watanzania yachukue sura gani kwa miaka mitano ijayo na kwa mtazamo mpana zaidi, kwa mustakabali wa maisha yao yote ya baadaye.
Kwa maana hiyo, uchaguzi wa Rais ni tukio muhimu kwa mustakabali wa Taifa hivyo ni lazima wananchi wafanye uamuzi sahihi wakati wa kupiga kura. Uamuzi sahihi utawezekana tu ikiwa wapigakura watapata fursa ya kutosha ya kuwasikia waomba urais, kuchambua hoja zao na kuwauliza maswali ili waone jinsi wanavyoweza kuzitetea hoja zao.
Moja ya njia za kuwawezesha kuonekana na kusikika ni kwa kushiriki katika midahalo ya wazi ambako watajieleza waziwazi, kuelezea vipaumbele vyao na kutetea hoja zao kabla ya wananchi kwenda kwenye sanduku la kura Oktoba 25.
Tunaamini kuwa wagombea wana wajibu wa kushiriki kwenye midahalo hii ili waeleze sera zao kwa jamii wanayotaka kuiongoza na baadaye kuulizwa maswali na kuyajibu ili waonyeshe ukomavu wao na jinsi walivyojipanga si tu kuliongoza Taifa hili, bali kulitoa katika hali fulani na kulipeleka kwenye hali nyingine.
Kwa vipindi viwili sasa, Tanzania haijashuhudia midahalo hii tangu wagombea wa mwaka 1995, Benjamin Mkapa, Augustine Mrema na Profesa Ibrahim Lipumba waliposhiriki mdahalo ambao uliwapa wananchi fursa nzuri ya kuwajua waliokuwa wanataka kuwaongoza na hatimaye kufanya uamuzi wakiwa na ufahamu tosha.
Hatuamini kuwa hali hii ya kuwanyima fursa wapigakura kuwajua vizuri wagombea wao wa urais, itajitokeza kwenye Uchaguzi Mkuu wa safari hii ambao umekuja wakati kuna mwamko mkubwa wa kisiasa na wananchi kukomaa zaidi kiasi kwamba kuna kila umuhimu kwao kuwasikia wagombea wao ili wafanye uamuzi sahihi. Mgombea ambaye hatataka kushiriki kwenye midahalo hii, ana ajenda ya siri na hivyo hafai kupewa uongozi wa nchi kwa kuwa hataki kulishirikisha ajenda yake.
Vyama visiwazuie makada wake kushiriki kwenye midahalo kwa kuwa vitakuwa vinawanyima wapigakura fursa ya kuwajua vizuri wagombea na pia kuwanyima haki ya kufanya uamuzi sahihi, huru na wa haki.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment