Image
Image

Serikali isicheze na afya za Watanzania.


Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid jana aliwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya fedha ya wizara yake kwa mwaka 2015/16, akiomba kuidhinishiwa Sh813 bilioni.
Kati ya fedha hizo, Sh444.6 bilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo na Sh369.3 bilioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida. Kimsingi afya ni sekta mojawapo yenye changamoto lukuki hapa nchini. Ni sekta muhimu katika kuchangia ustawi wa Taifa.  Kumekuwa na changamoto kadhaa  katika sekta  ya Afya. Hata hivyo Serikali imefanya jitihada kubwa kukabiliana na changamoto hizo.
Baadhi ya  jitihada hizo ni  kupandisha viwango vya hospitali, kukarabati na kuongeza majengo, kuongezeka kwa wataalamu wa afya pamoja na huduma  za kitaaluma katika baadhi ya hospitali zetu.
Lakini pamoja na jitihada hizo mabadiliko hayo yamekuwa hayalingani na ongezeko la idadi ya watu pamoja na  sayansi na teknolojia.  Kwa mfano tatizo la uhaba wa dawa limeendelea kuvikumba vituo vyote vya  Serikali hapa Tanzania kiasi cha kuwa chanzo cha vifo vingi ambavyo  vinatibika.
Tatizo jingine katika sekta hiyo ni upungufu wa vifaa tiba. Vituo  vingi vya  tiba vimekabiliwa na upungufu huo na kusababisha wagonjwa kutopata tiba kwa ufasaha hivyo kuhatarisha afya zao. Si ajabu hospitali kukaa muda mrefu bila kipimo cha wingi wa damu, kipimo cha sukari na hata X-Ray.
Uhaba wa dawa umekuwa ni tatizo kubwa nchini na malalamiko mengi yametolewa. Kwa mfano mapitio ya kumbukumbu za Bunge ya 2008/09-2012/13 yanaonyesha takribani asilimia 35 ya wabunge ambao huchangia katika mjadala wa bajeti ya afya, hulalamika uhaba wa dawa vituoni na kuitaka Serikali kuongeza fedha.
Pia kuna tafiti kadhaa zimefanywa kuhusu tatizo la uhaba wa dawa kwenye hospitali na vituo vya afya. Kwa mfano utafiti uliofanywa na Taasisi ya Ifakara nchini (IHI), ulibaini kuwa  katika kipindi cha mwaka 2012 dawa muhimu zilizokuwepo katika vituo zilikuwa asilimia 41 tu.
Kwa mujibu wa utafiti huo, hali hiyo ilimaanisha kuwa kwa takribani asilimia 60 ya dawa muhimu hazikuweza kupatikana katika vituo vya huduma za afya. Katika utafiti huohuo, ilibainika kuwa dawa za antibiotics zilipatikanna kwa asilimia 57 tu, kitu ambacho ni hatari sana kwa magonjwa ya milipuko ambayo yamekuwa yakisababisha vifo.
Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Dk Antony Mbassa katika hotuba bungeni jana alizungumzia suala la uhaba wa dawa katika hospitali nyingi nchini, na  kufafanua kuwa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaonyesha kuwa upatikanaji wa dawa katika vituo vya Serikali ni asilimai 24 na vituo binafsi ni asilimia 47.
Kuna matatizo mengi katika sekta ya afya ambayo hatuwezi kuyaorodhesha yote hapa, lakini kubwa zaidi ni ufinyu wa bajeti kwa sekta hii muhimu. Mbali na ufinyu, hata hizo fedha kidogo zinazopelekwa, hazifiki zote. Hali hiyo inafanya suala la afya bora kuwa gumu na hivyo kujenga fikra kwamba iko siku itakuwa vigumu kumpata Mtanzania mwenye afya bora.
Kwa hali hiyo ni dhahiri kwamba kuna kila sababu kwa Serikali kuelekeza nguvu zake kwenye sekta ya afya. Bila kuwa na Watanzania wenye afya bora, ni nadra kuwa na taifa lenye nguvu kazi madhubuti. Wito wetu na kuitaka Serikali kutochezea sekta hii muhimu kwa ustawi wa Taifa.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment