Image
Image

Wananchi chambueni ahadi, nyingi hazitekelezeki.


Kuanzia mapema mwezi huu, makada mbalimbali wa Chama Cha Mapinduzi (CCM wamekuwa wakichukua fomu, kwenye makao makuu ya chama hicho mjini Dodoma, za kuomba udhamini wa wanachama wao waweze kugombea urais.
Baadhi yao walichukua fomu hizo, baada ya kwanza kuandaa mikutano mikubwa katika kumbi mbalimbali au viwanja vya mpira, na kutangaza nia huku wengine wakichukua kimyakimya bila ya kujinadi japo baadaye walizungumza na vyombo vya habari. Orodha ya waliochukua fomu kupitia CCM ni ndefu na ni jambo lenye afya katika demokrasia.
Tunawapongeza wagombea wote. Masikitiko yetu; kwanza, ni kuona baadhi ya wagombea hao wakiwabeza wenzao, kuonyesha kwamba hawana uwezo, hakuna anayefaa kuliko wao. Pili, ni kauli zao za kuiponda hata Serikali hii ya awamu ya nne iliyoundwa na chama chao.
Tatu, ni ahadi nyingi zinazotolewa na wagombea hao juu ya mambo watakayotekeleza ikiwa watateuliwa kugombea na kushinda urais katika uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu.
Tunawatahadharisha wananchi wawe macho. Mfano, baadhi ya wagombea wamedai watajenga reli kuunganisha mikoa, kujenga viwanda ili uchumi wa nchi uendeshwe na viwanda, kupambana na mafisadi waliolelewa na kukingiwa kifua na serikali, kuendesha nchi bila kutegemea hata senti kutoka nchi wahisani na kuteua baraza dogo la mawaziri.
Wengine wamedai watarejesha Azimio la Arusha, kila nyumba itakuwa na mabomba mawili; moja la kuingiza maji na jingine kuingiza gesi, kuifikisha nchi kuwa ya uchumi wa kati, kuigeuza Tanzania kuwa nchi mpya – nchi ya asali na maziwa, na kutekeleza yaliyomo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Ahadi hizo – wananchi wasipojiuliza swali watatekeleza vipi – ni tamu masikioni na ndiyo maana kila mtangazania alishangiliwa sana na umati mkubwa wa wafuasi wake waliofurika kumsikiliza, wakiwamo baadhi ya viongozi mashuhuri wastaafu. Hata hivyo, baadhi ya wananchi wamekuwa wakiwashangilia watangazania kwa vile wanatoka maeneo yao lakini si uhalisia wa ahadi.
Hebu wananchi jiulizeni, ikiwa kwa miaka 54 ya uhuru, watu wanahangaika na maji na wakipatiwa ni ya visima, ni miujiza gani itafanyika kwa miaka mitano kila nyumba, hata za mbavu za mbwa, kuwa na mabomba ya maji na gesi? Vipi watajenga viwanda vipya wakati sera ya Serikali ni kutokujihusisha na biashara?
Baadhi ya wagombea hao wamezeekea katika utumishi serikalini, wameshuhudia na kuhusika kukingia kifua mafisadi, leo wanaposema watapambana na wala rushwa, watafanya miujiza gani kuondoa kansa hiyo?
Jiulizeni, kati ya watangaza nia hao, ni nani amethubutu bungeni kupigia kelele ufisadi kupitia ununuzi wa rada, Richmond na Escrow? Ni wizara gani haijawahi kukumbwa na dosari za udhibiti wa fedha kama inavyoainishwa na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali? Watu walifikia kuiba hata fedha za safari wakidai ni za safari za rais wakati ni uongo! Kwanini baadhi yao walifukuzwa uwaziri?
Hatuna nia ya kuwapinga wagombea hao, lakini wawe wakweli, ahadi walizotoa nyingi hazitekelezeki. Hata Serikali ya Awamu ya Nne iliingia madarakani na ahadi nyingi tamu kwenye masikio ya wapigakura, lakini hadi leo kila eneo wanalalamika ahadi ya rais haijatekelezwa na sababu kubwa hazikuwamo kwenye Ilani ya Uchaguzi. Hivyo, tunawatahadharisha wananchi kwamba wote wanaoshangilia ahadi ambazo hazimo kwenye ilani watachagua rais kanyaboya.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment