SIKU mbili baada ya kutunukiwa Nishani ya Amani na Utulivu katika
Ukanda wa Afrika Mashariki, Rais Jakaya Kikwete jana alikabidhiwa tuzo
nyingine ya kimataifa, ya Utawala Bora barani Afrika kwa mwaka 2015.
Tuzo hiyo aliyokabidhiwa jana ilipokolewa kwa niaba yake na Waziri wa
Katiba na Sheria, Dk Asha-Rose Migiro katika sherehe iliyofanyika Julai
25, mwaka huu nchini Afrika Kusini.
Rais Kikwete ametunukiwa tuzo hiyo na Bodi ya Uongozi ya Africa
Archiever’s Award kwa kutambua mchango wake katika maeneo ya uongozi na
utawala bora wakati wa uongozi wake wa miaka 10 wa Tanzania.
Hafla ya makabidhiano hayo ilifanyika jana Ikulu, Dar es Salaam na
kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali, wakiwemo Katibu Mkuu Kiongozi,
Balozi Ombeni Sefue, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju, Kaimu
Katibu Mkuu Ikulu, Susan Mlawi na Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu
na Utawala Bora, Tom Bahame Nyanduga.
Akizungumza kabla ya kukabidhi tuzo hiyo, Waziri Migiro alisema kwa
kupata tuzo hiyo, Rais Kikwete anaungana na viongozi wengine mashuhuri
Afrika ambao wamepata tuzo hiyo wakiwemo Rais wa zamani wa Ghana, Hayati
John Atta Mills, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Nkosazana
Dlamini Zuma na Askofu Desmond Tutu, kiongozi wa Kanisa la Anglikana
nchini Afrika Kusini ambaye pia ni mwanaharakati mashuhuri barani
Afrika.
Alisema Rais Kikwete alikuwa miongoni mwa Waafrika mashuhuri 1,202
ambao majina yao yalipendekezwa kwa ajili ya kutunukiwa tuzo hiyo kwa
mwaka huu, lakini Bodi iliyomtunukia Rais Kikwete tuzo hiyo imeridhishwa
zaidi na mchango wake mkubwa katika kujenga na kuleta utawala bora
katika miaka yake 10 ya uongozi wake.
Katika hafla hiyo, Rais alisema hakuweza kwenda kupokea tuzo hiyo
Afrika Kusini kwa sababu wakati huo alikuwa katika ziara rasmi ya
Kiserikali nchini Australia, lakini akaongeza kuwa amefurahi kutunukiwa
tuzo hiyo.
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)


0 comments:
Post a Comment