KOCHA wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Charles Mkwasa
amesema licha ya timu yake kupata matokeo ambayo sio mazuri sana dhidi
ya Nigeria Super Eagles, kikosi chake kimeonesha mwanga katika mechi
hizo za kufuzu kwa fainali za Afcon 2017.
Taifa Stars juzi iliikaribisha Super Eagles na kutoka nayo suluhu
katika mchezo wa kufuzu kucheza fainali za Mataifa ya Afrika uliofanyika
kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Fainali hizo za Mataifa ya
Afrika mwaka 2017 zitafanyika nchini Gabon.
Mkwasa akizungumza na waandishi wa habari baada ya mchezo huo,
aliwapongeza wachezaji wake kwa kucheza kama alivyowaelekeza na
kufanikiwa kuibana Nigeria katika mchezo huo.
“Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa matokeo haya, kwa kweli nimeridhika na
kiwango kilichooneshwa na wachezaji wa timu yangu kwani wamecheza kama
nilivyowaelekeza,” alisema Mkwasa. Alisema walichopungukiwa wachezaji
wake ni uzoefu wa kimataifa ukilinganisha na Nigeria, ambao asilimia
kubwa ya wachezaji wake wanacheza soka Ulaya.
Mkwasa aliipongeza Nigeria kwa kucheza vizuri kwani uzoefu wao kwa
kiasi kikubwa ndio walichangia Taifa Stars kucheza kwa kiwango kile
walichocheza hadi kusababisha kuondoka na pointi moja.
Alisema Taifa Stars ilicheza mchezo wa kujituma zaidi na kila
mchezaji alitekeleza jukumu lake kama alivyokabidhiwa. Alisema kikosi
chake kilicheza kwa tahadhari na kwa kujituma sana ili kutopoteza mchezo
huo wa nyumbani mbele ya mashabiki wao waliofika kuishuhudia timu yao
iliyocheza na timu yenye uwezo mkubwa.
Mkwasa alisema watajipanga vizuri zaidi ili kuhakikisha wanaibuka na
ushindi katika mechi zao zijazo dhidi ya Chad, Misri (marudio) na
Nigeria (marudio) na kuhakikisha wanafuzu kucheza fainali hizo za
Afrika.
Kwa upande wake kocha wa Super Eagles, Sunday Oliseh alisema kuwa,
timu yake ilionekana kucheza vizuri katika vipindi vyote ukiondoa makosa
madogo madogo waliyoku wa wakiyafanya wachezaji wake.
Alisema timu yake bado mpya na wanaijenga na ni matumaini yake kuwa, wataendelea kufanya vizuri siku zinavyozidi kwenda.
Aliitetea timu yake kuwa ilikuja siku mbili kabla ya mchezo na hilo
liliwafanya kuwa wachovu licha ya wakati fulani kuonekana wakishambulia
kwa nguvu na wakati mwingine wakipunguza kasi yao, ambapo alisema
matokeo hayo ni sehemu ya mchezo.
Alisema wanatarajia kufanya vizuri zaidi katika michezo ijayo kwani
watakuwa na muda zaidi wa kufanya marekebisho ili kuhakikisha wana fuzu
kwa fainali hizo. Stars katika mchezo wake wa kwanza dhidi ya Misri
ilichapwa 3-0 huku Nigeria wenyewe waliifunga Chad 2-0 katika mchezo wao
wa awali.
Taifa Stars mchezo wake ujao watacheza ugenini dhidi ya Chad Machi
25, 2016 kabla ya kurudiana kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam Machi
28, huku Nigeria watakuwa na kibarua kigumu watakapocheza na mabingwa wa
kihistoria wa Afrika Misri wakiwa nyumbani Machi 23 mwakani.
Kimsimamo, Stars iliyokuwa inashika mkia imepanda na kuipiku Chad iliyokuwa katika nafasi ya tatu.
Msimamo Kundi G kabla ya mechi ya jana:
P W D L GF GA GD Pts
Nigeria 2 1 1 0 2 0 2 4
Misri 1 1 0 0 3 0 3 3
Tanzania 2 0 1 1 0 3 -3 1
Chad 1 0 0 1 0 2 -2 0


0 comments:
Post a Comment