Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk. Agnes Kijazi, alisema mvua hizo kubwa
zitakuwa na athari mbalimbali ukiwamo mlipuko wa magonjwa na uharibifu
wa miundombinu.
Mamlaka hiyo inaeleza kwamba mvua hizo zinatarajia kuanza wiki ya
kwanza ya mwezi huo na kuendelea hadi Novemba mwaka huu, ingawa baadhi
ya maeneo yatakuwa na mvua za wastani.
Awali zilitolewa taarifa kwamba zingenyesha mvua za el-nino, lakini
taarifa za utabiri za hivi karibuni zinabainisha kwamba hatari hiyo
haipo tena.
Taarifa za mamlaka hiyo kuhusiana na kuwapo kwa mvua kubwa za vuli
zinapaswa kuchukuliwa kwa uzito mkubwa ikiwamo kuchukua tahadhari
mapema.
Hata hivyo, kutokana na sababu zisizoeleweka, baadhi ya wananchi
wamekuwa wabishi na wakipuuza tahadhari inayotolewa na mamlaka hiyo
kuhusiana na uwezekano wa kutokea kwa maafa.
Hii sio mara ya kwanza kwa mamlaka hiyo kutoa tahadhari za namna
hiyo, lakini tatizo kubwa kwa baadhi ya wananchi viongozi kwa ujumla
wake wanakuwa wagumu kuchukua tahadhari zinapotolewa taarifa za
uwezekano wa kutokea kwa majanga.
Kutokana na kutotiliwa maanani kwa tahadhari hizo, kila mara
wananchi wamekuwa wakipatwa na maafa na baada ya hapo kutolewa matamko
balimbali na viongozi, lakini baadaye utekelezaji wa maagizo
hushindikana.
Mvua kubwa zimekuwa zikisababisha mafuriko na kuwaathiri wananchi
kadhaa hususani wanaoishi katika maeneo hatarishi kwa kubomoa nyumba zao
na kukosa makazi huku wengine wakipoteza maisha.
Katika miaka ya hivi karibuni, wananchi katika maeneo kadhaa nchini
wamejikuta wakikosa makazi na wengine kupoteza maisha hususani wakati
wa mvua za masika.
Kwaka 2011 kwa mfano, mvua kubwa za masika zilisababisha vifo vya
watu zaidi ya 40 jijini Dar es Salaam na wengine takribani 500 walikosa
makazi, baada ya nyumba zao kujaa maji na kulazimika kuhifadhiwa na
serikali katika kambi za muda zilizowekwa kwenye shule.
Wengi wao ni wale waliokaidi kuhama katika makazi yao yaliyoko
kwenye mabonde, licha ya TMA na mamlaka nyingine za serikali kutoa
tahadhari na kuwataka wahame.
Pamoja na serikali kuwahifadhi na kuwapatia misaada ya kibinadamu,
pia iliwapatia viwanja katika maeneo ya Mabwepande, wilayani Kinondoni
kwa ajili ya makazi mapya, zipo taarifa kuwa baadhi ya waliopewa viwanja
hivyo, waliamua kurejea katika maeneo ya mabondeni bila sababu za
msingi.
Aidha, wapo baadhi ya wakazi katika Wilaya ya Ilala, ambao
wanaendelea kukaidi kuhama wakidai kuwa wanasubiri kulipwa fidia licha
ya halmashauri kuwaamuru waondoke kutokana na eneo lao kutokuwa salama
zinaponyesha mvua kubwa.
Mvua za masika za mwaka huu pia zilisababisha vifo vya watu zaidi
ya 12 jijini Dar es Salaam na wengine kulazimika kuhama maeneo yao
kutokana na nyumba zao kujaa maji.
Kutokana na ukaidi huo, serikali hususani mkoani Dar es Salaam
imeshasema kuwa haitatoa msaada tena kwa waliokaidi kuhama ikiwa maeneo
yao yatakumbwa tena na mafuriko ya mvua.
Tunawashauri wakazi wa maeneo yote hatarishi nchini kuitikia
tahadhari iliyotolewa na TMA kwa kuhama maeneo yao ili kuepukana na
uwezekano wa kupoteza mali zao, kukumbwa na magonjwa ya mlipuko kikiwamo
kipindupindu na hata vifo.
Tunazikumbusha pia mamlaka kadhaa zikiwamo halmashauri kuboresha
miundombinu kama barabara na madaraja kabla ya mvua hizo kuanza.


0 comments:
Post a Comment