Image
Image

Wanachama feki wa Chadema wachafua hali ya hewa*Polisi yafyatua mabomu ya machozi.

SIKU moja baada ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa kudai mgombea urais wa chama hicho/Ukawa, Edward Lowassa hafai kuwania nafasi hiyo Vijana ambao inaaminiwa kuwa siwa na chama halali wa Chadema wameibuka jijini Dar es Salaam huku wakitishiana kwa mapanga.
Ilidaiwa kuwa walichukua hatua hiyo kutokana kupishana kauli kwa kutoridhishwa na kitendo cha Dk. Slaa kuachia ngazi ndani ya chama hicho ambacho alikitumikia kwa nguvu zake zote,lakini wachache ndiyo wanafaidi matunda yake.
Kutokana na hali hiyo, hali ya usalama ilikuwa si shwari katika ofisi za makao makuu ya Chadema zilizopo Mtaa wa Ufipa, Kinondoni, ambapo walinzi wa chama ilibidi kutoa silaha, yakiwemo mapanga ili kujilinda dhidi ya wapenzi hao wa. Dk Slaa.
Wapenzi hao FEKI wa Dk. Slaa waliandamana wakishinikiza chama hicho kumrudisha madarakani huku wakitoa amri ya kutaka kiachane na mgombea wake wa urais, Lowassa kwani baada ya kuingia Chadema kumekuwa na mpasuko mkubwa.
Tafrani hiyo ilitokea saa sita mchana baada ya kundi la watu waliojitambulisha kama wapenzi na wanachama wa Chadema kukusanyika eneo la Kinondoni Morocco wakiimba nyimbo za “tunamtaka Babu, hatumtaki Mamvi” (wakimaanisha wanamtaka Slaa na hawamtaki Lowassa).
Ilidaiwa kuwa vijana hao walitoka maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam na idadi yao inazidi 100. 
Vijana hao walikuwa wamevaa mavazi ya chama hicho huku wakiwa na mabango pamoja na bendera za Chadema.
Pia,vijana hao wa kiume na kike wakati wakisubiriana na kutafuta namna ya kupeleka malalamiko yao kwenye chama walisikika wakiimba nyimbo huku wakihamasishana kwa maneno ya “Peoples Power”.
Kutokana na hali hiyo Jeshi la Polisi liliingilia kati na kuzuia maandamano hayo kwa kufyatua mabomu ya machozi na baada ya purukushani ya muda mfupi, liliwakamata vijana waliohusika katika mkusanyiko huo kwani ilikuwa ni kinyume cha sheria.
Pamoja na askari kufika hawakusikiliza agizo la Polisi na badala yake waliamua kwenda Makao Makuu ya Chadema kueleza malalamiko yao kwamba Dk. Slaa ameonewa na chama kinatakiwa kimrudishe katika nafasi yake vinginevyo hawataelewa chochote.
Mwandishi wa gazeti hili ambaye alifuatilia sakata hilo hadi ofisi za Chadema, alikuta vijana wa chama hicho wakianza kuingia na kujaa kwa wingi katika nje ya ofisi za chama.
Mmoja wa vijana hao alisikika akiwaambia wenzake kuwa wamepewa taarifa kuwa kundi hilo linaloandamana limetumwa kwenda kufanya fujo na kwamba wao wanatakiwa kujiandaa na kukilinda chama kwa gharama yoyote.
Dakika chache baada ya kundi la Morocco kufika Mtaa wa Ufipa yalipo Makao Makuu ya Chadema, vijana walinzi walianza kutoa silaha kama mapanga na kuwatisha vijana hao.
Kulikuwa na kubadilishana lugha kwa dakika chache baina ya pande hizo mbili lakini baada ya muda mfupi mawe yalianza kurushwa huku watu kutoka Morocco wakikimbia na kuondoka eneo hilo.
Kutokana na hali tete eneo hilo, eneo la Kinondoni hususan Mtaa wa Ufipa na Togo walionekana askari Polisi na wenye maduka na nyumba walianza kuingiwa na taharuki.
Baada ya vijana hao kuondoka Makao Makuu ya Chadema,walinzi wa chama hicho walianza kuzunguka katika mitaa ya jirani na ofisi zao na kukamata mtu yeyote waliyekuwa hawamfahamu.
Kutokana na hali hiyo, gazeti hili liliwasiliana jana na Jeshi la Polisi Kinondoni na kujulishwa kuwa linawashikilia vijana 10 wanaosadikiwa kuhusika na maandamano yaliyofanyika katika eneo la Morocco jijini Dar es Salaam ili kuwahoji.
Akizungumza na gazeti hili jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura alisema vijana hao wanaendelea kuhojiwa ili kujua ni kwa namna gani wameshiriki maandamano hayo. 
Wambura alisema mahojiano hayo yanaweza kuchukua wiki moja au zaidi.
Kamanda Wambura alisema baada ya vijana hao kuandamana walitawanywa na Jeshi la Polisi kwa kutumia mabomu ya machozi ambapo baadhi walitupa mabango waliyokuwa nayo barabarani na kukimbia lakini wengine walikamatwa na kufikishwa Kituo cha Polisi Oysterbay.
Alisema baadhi walishikiliwa katika ofisi za Makao Makuu ya Chadema zilizopo eneo la Kijitonyama, wengine Ofisi za Mtengaji Kata maeneo ya Biafra na wengiene eneo hilo la Morocco na jumla ya vijana hao ni 10.
Ilivyokuwa
Baadhi ya wafuasi wa Chadema waliandamana kupinga hatua ya Dk. Slaa kustaafu siasa kutokana na ujio wa Lowassa kwenye chama hicho. Wafuasi hao waliokuwa na mabango mbalimbali yaliyokuwa na picha za Dk. Slaa yenye jumbe tofauti tofauti waliandamana jana maeneo ya Morocco, Mwenge.
Wakati wa maandamano hayo wafuasi hao walikuwa wakiimba nyimbo mbalimbali ikiwemo ya kuwa”hatumtaki Lowassa…hatumtaki Lowassa”.
Mashuhuda
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili baadhi ya mashuhuda walioshuhudia tukio hilo walisema wao walishangaa kuona watu waliokuwa wamebeba mabango wakipita huku wakiimba barabarani ambapo baada ya kuwauliza ni nini kinaendelea hawakupewa jibu lolote.
Rashid Said alisema wakati maandamano hayo yakiendelea walitokea askari waliokuwa na gari aina ya Defender tatu na kuanza kupiga mabomu ya machozi hali iliyowasababishia wafuasi hao kutawanyika.
Alisema baadhi wafuasi hao walitawanyika na wengine kukimbia lakini baadhi yao walikamatwa.
Said alisema baada ya muda mfupi alishuhudia wengine wakiachiwa baada ya ndugu zao kwenda kuulizia katika kituo hicho chanzo cha kukamatwa kwa ndugu zao.

Gazeti hili lilishuhudia baadhi ya wafuasi walioachiwa wakitembea kando ya barabara huku wakilalamika kuwa kwa nini wakamatwe wakati wameandamana kutafuta haki yao.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment