Habari Kamili.
RAIS Dkt. John Pombe Magufuli amevunja Bodi ya Mamlaka ya Bandari (TPA) na kutengua uteuzi wa Mwenyekiti wa Bodi ya Bandari, Prof. Joseph Msambichaka pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Bandari, Bw. Awadhi Massawe.
Dkt. Magufuli pia ametengua uteuzi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dkt. Shaban Mwinjaka kuanzia leo (Jumatatu, Desemba 7, 2015), na kwamba atapangiwa kazi nyingine.
Akitangaza uamuzi huo mbele ya waandishi wa habari kwenye mkutano uliofanyika leo ofisini kwake Magogoni, jijini Dar es Salaam, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema hatua hizo zimechukuliwa kufuatia ziara mbili za kushtukiza alizozifanya katika mamlaka ya bandari Novemba 27 na Desemba 3, mwaka huu.
Waziri Mkuu amesema Rais Magufuli amevunja bodi hiyo na kutengua uteuzi wa viongozi hao kutokana na utendaji mbovu wa muda mrefu wa Mamlaka ya Bandari na kwa kitendo cha viongozi hao kutochukua hatua kwenye vyanzo.
Pia alisema Katibu Mkuu amesimamishwa kazi kwa sababu ya kutosimamia kwa makini mashirika mawili ya Bandari na Reli ambayo yako chini ya wizara yake ambako yeye mwenyewe alizuru Shirika la Reli (TRL) Desemba 3, 2015 na kukuta kuna ubadhirifu wa sh. bilioni 16.5/-.
“Tarehe 3 Desemba mwaka huu nilifanya ziara ya kushtukiza pale TRL nikakuta wametumia visivyo sh. bilioni 13.5/- walizopewa na Serikali. Pia nilikuta wamekopa sh. bilioni 3/- kutoka benki ya TIB lakini nazo wamezitumia nje ya utaratibu. Fedha hizi zilikuwa ni za kusaidia kuboresha miradi ya shirika lakini wao wamezitumia visivyo. Uchunguzi bado unaendelea,” alisema Waziri Mkuu.
0 comments:
Post a Comment