MKUU wa Mkoa wa Katavi, Dk Ibrahim Msengi
amewasimamisha kazi maofisa waandamizi 11 wa Manispaa ya Mpanda akiwemo
Mkurugenzi Mtendaji wake, Suleiman Lukanga kwa ukiukwaji wa sheria za manunuzi
kwa kufanya ubadhirifu fedha zaidi ya Sh milioni 92.8.
Dk Msengi alieleza kuwa Lukanga na maofisa 11 wa
Manispaa ya Mpanda wanatuhumiwa kununua gari la kubeba taka ambapo kiasi cha Sh
milioni 92.8 zilitolewa kwa manunuzi hewa kwa kampuni hewa.
Wengine waliosimamishwa kazi ni Kaimu Mkurugenzi wa
Manispaa hiyo, Vincent Kayombo ambaye pia ni Ofisa Elimu (Msingi) wa Manispaa
ya Mpanda, Ofisa Manunuzi aliyetajwa kwa jina moja la Kakulima, Ofisa Mipango,
Ferdinard Filimbi, Mweka Hazina, Bosco Kapinga, Mhasibu Kibi Hamis Msaka na
wajumbe wanne wa Bodi ya Zabuni.
Dk Msengi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya
Ulinzi na Usalama wa Mkoa huo, ameamuru wakati uchunguzi kuhusu tuhuma hizo
ukiendelea, watuhumiwa wote 12 wasitoke nje ya Mji wa Mpanda na wahakikishe
wanalipa kiasi hicho cha fedha kwa kuwa ni fedha za umma.
“Maofisa hawa wa Manispaa na Mkurugenzi wao
wanatuhumiwa kufanya malipo hewa, ikiwa ni nusu ya fedha zilizotengwa kununua
gari hilo hakika wamefanya kwa makusudi …..
“Sasa naomba watupishe ili tufanye uchunguzi kwa
kuhusisha vyombo mbalimbali vya dola na wote wawe nje ya ofisi kuanzia sasa,
lakini wasitoke nje ya Mji wa Mpanda…..naagiza pia walipe kiasi hicho cha
fedha,” aliamuru.
Uamuzi huo umechukuliwa na mkuu huyo wa mkoa
kutokana na uchunguzi uliofanywa na tume tatu tofauti zilizoundwa kuchunguza
upotevu wa kiasi hicho cha fedha ambazo ni kati ya Sh milioni 200 zilizotolewa
na Tamisemi kwa ajili ya kununulia gari la taka katika Manispaa ya Mpanda.
Aidha, Dk Msengi ametoa onyo kwa mtumishi yeyote
aliyezoea kufanya ubadhirifu wa mali ya umma akisema wakae wakijua kuwa siku
zao zimetimia na kwamba tabia hiyo ovu haiwezi kufumbiwa macho.
Katika uchunguzi wa upotevu huo wa kiasi hicho cha
fedha uliofanywa na kamati tatu tofauti zilizoundwa na RC huyo zilibaini kuwa
Kampuni ya Bluecyon iliyoko Mbezi, Dar es Salaam ilizawadiwa zabuni ya kununua
gari hilo.
Uchunguzi wa Kamati hizo tatu zilizoongozwa na
Katibu Tawala Mkoa, Polisi Mkoa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa
(Takukuru) kuwa Bluecyon ilikuwa haijihusishi na biashara ya magari, bali ni
kampuni ya uchapishaji.
Akizungumza mjini Mpanda, Lukanga alisema, “Nilikuwa
kikazi kijijini baada ya kufika hapa mjini ndipo nimesikia agizo hilo la Mkuu
wa Mkoa kwamba amewasimamisha kazi watumishi 12 wa Manispaa ya Mpanda nikiwemo
na mimi niseme wazi kuwa agizo hilo tumelisikia.
“Hata kabla ya RC hajatoa taarifa hiyo jana tayari
nilikuwa nimeanza kulishughulikia tangu mwaka jana na tayari baadhi ya
watumishi wa Manispaa wamefikishwa mahakamani. Mgogoro unakuja baada ya mzabuni
huyo kushindwa kuleta gari hilo la kubebea taka….basi nilichukua hatua ikiwemo
kuvunja mkataba na mzabuni huyo na kuhakikisha fedha hizo zinarudi."
0 comments:
Post a Comment