Image
Image

MSD ipeleke dawa za kutosha maduka ya hospitali za umma.



Bohari Kuu ya Dawa (MSD), imeanza kufungua maduka ya dawa katika hospitali za serikali kwenye mikoa mbalimbali. Hatua ya MSD ya kufungua maduka ya dawa katika hospitali za serikali lengo lake kubwa ni kurahisisha upatikanaji wa dawa kwa wagonjwa pamoja na kudhibiti vitendo vya wizi wa dawa katika hospitali za umma na kutumika katika maduka ya watu binafsi kwenye maeneo ya hospitali hizo.

Zimekuwapo tuhuma nyingi kwamba baadhi ya watumishi katika hospitali za umma wamekuwa wakiiba dawa na kuuzwa katika maduka ya dawa yaliyoko katika maeneo ya hospitali za serikali huku wagongwa waliolazwa wakikosa dawa. Hii ni kero kubwa na ya muda mrefu ambayo kila mmoja angependa kuona inakomeshwa.

Uamuzi wa MSD wa kufungua maduka yake ya dawa katika maeneo ya hospitali za umma ni utekelezaji wa agizo lililotolewa na Rais John Magufuli, baada ya kubaini kuwa maduka kadhaa ya dawa ya watu binafsi yaliyoko kwenye hospitali za umma yanatumika kuuza dawa zinazoibwa katika hospitali za serikali na kuwalazimisha wagonjwa kuzinunua dawa hizo katika maduka binafsi, tena kwa gharama kubwa.

Rais Magufuli aliizungumzia sana kero hiyo katika mikutano yake ya kampeni za Uchaguzi mkuu wa mwaka huu na kuahidi kwamba akichaguliwa ataikomesha.

Katika utekelezaji wa agizo la Rais Magufuli, MSD imeshafungua duka la dawa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), ambalo limeanza kufanya kazi rasmi huku ikijiandaa kufungua maduka zaidi katika hospitali nyingine za serikali nchini. MSD imesema iko mbioni kufungua maduka mengine mawili katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya na ya Mount Meru mkoani Arusha.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa MSD, Laurean Bwanakunu, baada ya kukamilisha duka la Muhimbili, watahamia katika mikoa hiyo miwili. Tunaipongeza MSD kwa kutekeleza haraka agizo la mkuu wa nchi, ambalo lengo lake ni kuhakikisha huduma za afya kwa Watanzania wengi ambao ni maskini zinaboreshwa ikiwamo kupata dawa za uhakika na kwa gharama nafuu.  Hata hivyo, tunashauri kwamba MSD isijikite kufungua maduka ya dawa tu, bali kuhakikisha kuwa dawa za kutosha zinapelekwa katika maduka hayo sambamba na vifaa tiba.

Hakutakuwa na maana kama yatafunguliwa maduka mengi ya dawa kwenye hospitali za serikali bila kuwapo dawa za kutosha pamoja na vifaa tiba kwa ajili ya wagonjwa.

Jambo la kutia moyo ni kuwa mahitaji ya dawa na vifaa tiba ni makubwa, hivyo MSD ikifungua maduka katika hospitali zote za serikali zitanunuliwa. 

Tunafahamu kuwa kutakuwapo na changamoto kadhaa katika utekelezaji wa agizo la Rais Magufuli, lakini tunaishauri MSD ihakikishe kwamba dawa, vifaa tiba vya kutosha vinapelekwa katika maduka hayo na kuuzwa kwa gharama nafuu ili wagonjwa wazimudu.

Bwanakunu anaelezea baadhi ya changamoto wakazokabiliana nazo kuwa kuna uwezekano wa kuchelewesha ukamilikaji kwa sababu kazi ya ukarabati wa maduka hayo inagharimu kiasi kikubwa cha fedha.

Ni matarajio yetu kuwa MSD italitekeleza agizo hilo kwa wakati mwafaka na kwa tija na ufanisi, lakini ihakikishe pia inapeleka dawa za kutosha kwenye maduka hayo. 

Tunatambua kuwa MSD inaidai serikali deni kubwa la muda mrefu, lakini kasi kubwa ya utekelezaji wa majukumu ambayo imeonyeshwa na serikali ya Magufuli, tunaamini deni hilo litalipwa.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment