Mshauri maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu uzuiaji wa mauaji ya halaiki
amesema ikiwa mzozo nchini Burundi hautakomeshwa huenda kukatokea vita
vya wenyewe kwa wenyewe.
Adama Dieng amewaambia waandishi wa habari kuwa anaitumia siku ya kwanza
ya kuwakumbuka wahanga wa mauaji ya halaiki hivi leo (Jumatano tarehe 9
Disemba) kuitaka serikali ya Burundi na upinzani kumaliza mapigano na
kujadili jinsi ya kupata suluhisho la kisiasa ili kuleta amani katika
nchi hiyo ya Afrika Mashariki.
Dieng amesema anatoa mwito kwa nchi jirani kama Rwanda na Tanzania
ambazo zimepokea idadi kubwa ya wakimbizi wanaotoroka mapigano hayo
kuisaidia Burundi.
Uamuzi wa Rais Pierre Nkurunziza kuwania muhula wa tatu na baadaye
kushinda uchaguzi uliokumbwa na utata umezua mapigano kwa miezi kadhaa
sasa, likiwemo jaribio la mapinduzi lililoshindwa. Zaidi ya watu 240
wameshauawa tangu mwezi Aprili na karibu 215,000 wametorokea nchi
jirani, kulingana na Umoja wa Mataifa.
Burundi ina historia ya mapigano kati ya makundi ya kikabila ya Wahutu
na Watusti. Nkurunziza aliingia madarakani mwaka 2005 wakati wa
kumalizika kwa mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yaliyosababisha vifo vya
watu 300,000 kati ya mwaka 1993 na 2006.
Umoja wa Mataifa wapata hofu
Mkuu wa Kamisheni ya Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa, Zeid Raad al-Hussein, amesema hali nchini Burundi ni hatari sana.
"Tunasikitishwa na maneno tu bila hatua yoyote na kuwepo mauaji
yanayoelekea kuwa ya kikabila, na hili ni jambo ambalo sisi na nchi
katika eneo hili tunalihofia sana," alisema Zeid Raad al-Hussein.
Zeid amesema mashambulizi dhidi ya raia yanaonekana kuongezeka na hii ina maana kuwa pande husika zina lengo la kuzua fujo.
Ikiwa kutakuwa na hali ya utulivu, amesema vijana wa chama kinachotawala
sharti waweke chini silaha na kikosi cha polisi cha upelelezi sharti
kidhibitiwe. Amesema ni kwa hatua hiyo tu ndipo makundi mengine yaliyo
na silaha yataacha silaha zao.
Umoja wa Ulaya wavunjwa moyo
Umoja wa Ulaya umesema huenda ukabana uhusiano wake na Burundi na
kusalia kutoa msaada tu baada ya mazungumzo kushindwa kupata suluhisho
la tatizo la kaki za kinadamu katika taifa hilo.
Taarifa iliyotolewa baada ya mazungumzo ya muda mrefu mjini Brussels
ilisema Umoja wa Ulaya ambao ni mfadhili mkubwa wa nchi hiyo ya Burundi
unazingatia hatua ambazo Burundi inachukua, lakini hatua hizo huenda sio
suluhisho.
Muungano huo umesema itakuwa bora ikiwa serikali itakubali kuzungumza na
upinzani. Mazungumzo ya siku ya Jumanne yalifanyika chini ya mkataba wa
Cotonou, ambao ni uhusiano wa kiuchumi na maendeleo wa mataifa 28 ya
Ulaya pamoja na mataifa ya Afrika, Caribbean na Pacific na ambao umeweka
masharti makali ya ushirikiano ikiwemo kuhakikisha haki za kibinadamu.
Mwezi uliopita Ubelgiji, ambayo ilikuwa mkoloni wa zamani wa Burundi,
iliwaambia raia wake kuondoka nchini humo huku Umoja wa Ulaya ukiziondoa
familia za wafanyakazi wake baada ya Umoja wa Mataifa kuonya kuwa
huenda Burundi ikatumbukia kwenye mauaji ya halaiki.
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)
0 comments:
Post a Comment