Image
Image

Sababu kuu ya Kili Stars kukatwa Chalenji 2015 hii hapa.

Kama hukuona jinsi timu ya Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars) ilivyoaga kwenye michuano ya Chalenji mwaka huu, ukihadithiwa utaona wachezaji walifanya masihara ilhali timu ilikuwa na matokeo mazuri mwanzo-mwisho.

Kutolewa kwa Stars kunaandika rekodi mpya kwa Stars kushiriki michuano hiyo kwa mara ya tatu mfululizo bila kutwaa kombe hilo. Mara ya mwisho Stars kutwaa kombe hilo ilikuwa 2010 wakati michuano hiyo ilipofanyika jijini Dar es Salaam. 

Mwaka 2011 Uganda walikuwa mabingwa na walitetea ubingwa wao mwaka uliofuata, yaani 2012, kabla ya Kenya kuwapiku 2013 Kenya. Michuano hiyo haikufanyika mwaka jana kutokana na hali mbaya ya kifedha iliyokuwa inawakabili waandaji.

DHARAU
Kili Stars imeshindwa kufanya vyema mwaka huu katika michuano hiyo kutokana na wachezaji wa timu hiyo kuamini kuwa timu hiyo ni bora kuliko timu zote na tayari walikuwa wamejijengea fikra kuwa hakuna wa 'kuwagusa mpaka fainali'. 

Fikra hizo zilikuwa ni nzuri, lakini walihitaji kujituma na kufanya kazi bila ya kuangalia wanacheza na timu kibonde au timu ngumu. Stars ilitolewa dhidi ya Ethiopia ambayo ilikuwa ikicheza soka lisiloeleweka kimfumo.

PENGO LA AISHI MANULA
Kukosekana kwa Aishi Manula (alikuwa na rekodi ya kadi za njano) kwenye kikosi cha Stars katika mechi yao iliyowang'oa ya robo-fainali dhidi ya Ethiopia, kuliigharimu timu hiyo ya Bara kwani kipa Said Mohamed 'Nduda' alionekana kukosa uzoefu kwenye michuano hii, ikiwa ni mechi yake vya kwanza kwenye kikosi hicho mwaka huu.

Presha ilionekana kuwa kubwa kwake hasa wakati wa penalti, akifungwa mikwaju yote minne iliyopigwa na nyota wanne wa Ethiopia.

Bila shaka, kipa mzoefu wa michuano ya kimataifa, Ally Mustafa 'Barthez' aliyekuwa benchi Jumatatu 
angekuwa chaguo zuri kwenye hatua ya matuta kutokana na ukweli kwamba Nduda tayari alikuwa na 
presha ya kufungwa goli ndani ya dakika 90 za mchezo.

WASHAMBULIAJI BUTU
Kocha wa Kili Stars, Abdallah 'King' Kibadeni alikuwa akiwatumia zaidi washambuliaji John Bocco, Elias
Maguli na Malimi Busungu kwenye eneo la kati la ushambuliaji, lakini kocha huyo anadai mastraika hao walikosa nafasi nyingi ukilinganisha na matokeo waliyokuwa wakipata.

Nipashe iliyopiga kambi jijini hapa mwanzo-mwisho kufuatlkia michuano hiyo mwaka huu, ilishuhudia nafasi mbili hadi tatu zikipotezwa 'kizembe' na  mastraika Maguli na Bocco katika kila mechi waliyocheza. 

VURUGU ZILIWATOA MCHEZO
Penalti iliyosababishwa na beki wa pembeni kulia Shomary Kapombe na kuzaa bao la kusawazisha la Ethiopia katika dakika ya 56 ilionekana kuwatoa mchezoni nyota wengi wa Stars.

Wengi wao walionekana kukosa imani na mwamuzi kiasi cha kuanzisha vurugu zilizosimamisha mchezo kwa dakika tatu huku baadhi ya wachezaji akiwamo nahodha Bocco wakionywa kwa kadi za njano.

Vurugu zilipomalizika wachezaji wengi wa Stars walionekana kupunguza kasi na kukata tamaa ya kusaka ushindi.

KUVIMBA KICHWA
Tatizo kubwa la Stars ya Chalenji 2015 lilikuwa wachezaji wake kujiamini kupita kiasi, walijua fika wangeitoa Ethiopia na kwenye michezo yote miwili dhidi ya timu hiyo (hatua ya makundi na robo-fainali)
walionekana kutopania ushindi. 

Mabeki wa pembeni Mohamed Hussein 'Tshabalala' na Hassan Kessy walionekana kupoteza muda bila sababu kuntu katika mechi ya robo-fainali. Pia wachezaji walikuwa wakiweka 'njonjo' nyingi wakati timu ilikuwa ikihitaji zaidi mabao kuliko maonyesho ya jinsi ya kuuchezea mpira.

KELELE ZA MASHABIKI 
Kelele za mashabiki wa Ethiopia ambao walijitokeza kuishangilia timu hiyo pia zilionekana kuchangia kuivuruga Stars. Licha ya kuwa na nyota wengi wenye uzoefu wa mechi za kiimataifa, tmu hiyo ilikuwa inacheza kwa presha, hasa baada ya wenyeji kusawazisha.

Hali hiyo pamoja na vurugu na uamuzi ya mwamuzi kutoa penalti ambayo nyota wengi wa Stars waliona ilikuwa na utata, vilichangia kwa kiasi kikubwa kuivuruga timu yao kumalizia dakika 36 za mwisho ambazo ilishindwa kutengeneza mashambulizi ya maana.

Wachezaji na hata benchi la ufundi la Stars lilikuwa linamsakama refa kwa madai kwamba alichezesha mechi kwa maagizo ya waandaaji kuhakikisha wenyeji Ethiopia inasonga mbele ili kuchangamsha michuano.

Jambo pekee la kujivunia ni kwamba Stars imeaga mashindano ikiwa haijapoteza mchezo hata mmoja ndani ya dakika 90. Kwenye hatua ya makundi timu hiyo ilipata ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Somalia, 
kisha ikaifunga Rwanda 2-1 na kutoa sare ya 1-1 dhidi ya Ethiopia kabla ya kung'olewa kwa matuta 4-3 dhidi ya wenyeji hao baada ya sare ya 1-1 tena ndani ya dakika 90.

'SUB' 3 DAKIKA 360
Ni straika Malimi Busungu na kiungo Jonas Mkude pekee ambao walitokea benchi la Stars kwenye michezo yote minne. Stars ndiyo timu iliyofanya mabadiliko 'kiduchu' zaidi kwenye michuano hiyo mwaka huu licha ya kanuni za mashindano kuruhusu kubadili wachezaji watatu katika kila mchezo.

Kibadeni alimwingiza Busungu kwenye mchezo dhidi ya Somalia kuziba nafasi ya winga Simon Msuva. Kwenye mchezo dhidi ya Rwanda pia alimtoa kiungo Himid Mao na kumuingiza Jonas Mkude wakati kwenye mchezo wa tatu wa makundi kocha huyo hakufanya mabadiliko yoyote. 

Katika mechi ya robo-fainali, kocha huyo wa zamani wa Simba na Ashanti United, alimtoa winga Deus Kaseke na kumwingiza Busungu.

MAGOLI NANE
Stars imefanikiwa kufunga jumla ya mabao nane kwenye michuano hiyo ikiwa ni wastani wa kufunga mabao mawili katika kila mchezo huku ikiruhusu nyavu zake kutikiswa mara tatu.

Mabao ya timu hiyo yalifungwa na John Bocco (3), Elias Maguli (2), Simon Msuva (2) na Said Ndemla aliyetupia moja.

PASI ZA MWISHO
Katika mechi zote nne mastraika wa Stars walitengenezewa jumla ya mabao sita huku mabao mawili yakitokana penalti na lingine mpira wa adhabu.

Winga Msuva ameongoza kwa kutoa krosi tatu zilizozaa mabao, wakati beki wa pembeni kushoto Tshabalala alitoa krosi mbili zilizozaa mabao huku Maguli akipiga pasi moja iliyozaa bao.

NIDHAMU
Nidhamu ya nje ya uwanja kwa wachezaji wa Stars ilikuwa ni nzuri kwani muda wote walikuwa kambini na walikuwa wakifuata kwa muda kile walichotakiwa kukifanya.

Wachezaji wa Stars walipata jumla ya kadi nane za njano kwenye mechi zote nne walizocheza. Katika mechi ya kwanza dhidi ya Somalia hakukuwa na kadi yoyote, mchezo dhidi ya Rwanda, Kapombe alionywa kwa kadi, mchezo wa tatu dhidi ya Ethiopia, kipa Manula, beki Kessy, kiungo Mao na winga Msuva 
walionywa kwa kadi za njano. 
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment