Image
Image

Ugawaji bure mashine za EFD umekuja wakati mwafaka uungwe mkono.

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA), imetangaza kuanza kutoa mashine za kielektroniki za kodi (EFDs) bure kwa wafanyabiashara stahiki 200,000. Kwa mujibu wa Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA, Dk Philip Mpango hatua hiyo itakuwa endelevu, huku ukilenga kutanua zaidi wigo wa kukusanya kodi.
Kabla ya uamuzi huo wa TRA, kwa takribani miaka miwili kuliibuka mvutano baina ya wafanyabiashara na TRA, ambapo wafanyabiashara waligoma kutumia mashine hizo wakitaka Serikali ishughulikie kwanza kero zao zikiwamo za bei ya mashine, utitiri wa kodi, ukwepaji kodi na urasimu.
Hawakuishia hapo, waliitisha pia mgomo nchi nzima, kabla ya kuanza mazungumzo ya mara kwa mara na Serikali, ambayo wakati mwingine hayakufikia ukingoni, hatua iliyofanya baadhi ya viongozi wa wafanyabiashara kukamatwa.
Hata hivyo, hayo yamebaki kuwa historia baada ya viongozi hao kufutiwa mashitaka.
Akizungumza juzi, Dk Mpango alisema uchambuzi wa wafanyabiashara wanaostahili kupewa mashine hizo, unaendelea nchi nzima kwa kuangalia ukubwa wa biashara ili wapewe mashine hizo.
Kutokana na kusudio jipya la TRA na serikali kwa ujumla la kugawa bure mashine za EFD, sisi wa HabariLeo tunatoa pongezi za dhati kwa uamuzi huu wa busara unaolenga kujenga mazingira rafiki zaidi ya ukusanyaji wa kodi, lakini pia kutanua wigo wa ulipaji kodi ambayo mapato yake serikali inayahitaji kwa udi na uvumba katika kuhakikisha ustawi wa nchi katika sekta mbalimbali unakua kwa kasi.
Aidha, tunaipongeza mamlaka kwa usikivu, kwani hivi karibuni Rais John Magufuli aliwapa `darasa’ TRA huku akielezea mshangao wake kwa mamlaka hiyo kushindwa kugawa bure mashine husika kwa wafanyabiashara. Alisema TRA walipaswa kubaki na kazi ya kukusanya mapato, huku akisema muda uliopotea na kodi ambayo haikukusanywa wakati wa mvutano na wafanyabiashara, ungetosha kununua mashine mpya na kuwagawia.
“Kama mnajua mashine hizi ni halali na ni zenu, wapeni bure kazi yenu iwe ni kukusanya kodi, ni hesabu rahisi sana isiyohitaji kwenda chuo kikuu, kwamba muda uliopotea na fedha hazifiki Sh bilioni 12 zingetosha kununua mashine na kazi iwe ni kukusanya kodi,” alisema Rais Magufuli.
Tunaamini kwa kuwa TRA wamekuwa wasikivu na kuamua kugawa bure mashine husika, bila shaka roho za wafanyabiashara sasa zitakuwa kwatu na kuisaidia serikali kukusanya mapato.
Hata hivyo, tunaisihi TRA kuharakisha mchakato wa uchambuzi wa wafanyabiashara zaidi wanaostahili kulipa kodi, ili wigo wa kukusanya kodi uwe mpaka, badala ya kubaki na wafanyabiashara wachache, wafanyakazi walioko katika sekta rasmi ambao hawana ujanja wa kukwepa kodi kwa kuwa hufyeka kupitia mishahara yao, na kadhalika.
Hili likiwezekana, tuna uhakika kasi ya ukusanyaji mapato itazidi kupaa, huku Watanzania wakiendelea kuona mabadiliko ya kasi katika huduma za kijamii na unafuu wa maisha hasa kwa kipindi hiki ambacho Rais Magufuli ameshikilia msimamo wa kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, ili fedha za mlipa kodi zirudi kumnufaisha mlipa kodi kwa njia mbalimbali.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment