Image
Image

Ujenzi wa Barabara ya Mwenge-Morocco unatazamiwa kukamilika ndani ya miezi 6.

UJENZI wa Barabara ya Bagamoyo kipande cha kutoka Mwenge hadi Morocco jijini Dar es Salaam,chenye urefu wa kilometa 4.3, kinatarajia kukamilika ujenzi wake ndani ya miezi sita.
Ujenzi wa barabara hiyo ulianza juzi, ikiwa ni siku moja baada ya Rais John Magufuli kuamuru fedha zilizotengwa kwa ajili ya sherehe za Uhuru, zikajenge barabara ya Bagamoyo kipande cha Mwenge-Morocco.
Taarifa iliyotolewa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kupitia Mtendaji Mkuu wake, Patrick Mfugale, ilisema mkandarasi ameshaanza kazi na anatarajia kuikamilisha ndani ya miezi sita.
“Ujenzi umeanza na utakamilika katika kipindi cha miezi sita,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo huku akiomba wananchi wanaofanya shughuli zao kando ya barabara hiyo kupisha ili mradi usikwame.
“Ili utekelezaji usikwame, tunaomba wananchi wanaofanya biashara kandokando ya barabara hiyo, waondoke mara moja, aidha wanaoegesha magari katika eneo la mradi kipindi hiki cha upanuzi waache mara moja,” ilieleza taarifa hiyo ya Mfugale.
Aidha, Mamlaka ya Usimamizi wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) imewataka watembea kwa miguu na wananchi, kutoa ushirikiano katika kipindi hiki cha upanuzi wa barabara hiyo ili kufanikisha ujenzi ndani ya muda uliopangwa.
Juzi gazeti hili lilishuhudia tingatinga mbili, mali ya kampuni ya ukandarasi ya Estim katika eneo la Mwenge zikisafisha eneo la barabara hiyo, ikiwa ni maandalizi ya upanuzi kama maagizo ya Rais yalivyosema.
Dk Magufuli aliamuru Sh bilioni 4 zilizopaswa kutumika kugharamia sherehe za sikukuu ya Uhuru, ambazo zingefanyika Desemba 9, mwaka huu, kutumika kufanya upanuzi wa barabara ya Mwenge hadi Morocco yenye kilometa 4.3 kwa kuongeza njia mbili za barabara za lami.
Tayari fedha hizo zimepelekwa Tanroads kwa ajili ya kutekeleza agizo hilo. Dk Magufuli alimwagiza Mfugale, walipokutana Ikulu Dar es Salaam mapema wiki hii, kuwa ujenzi wa barabara hiyo uanze haraka ili kukabiliana na adha ya msongamano wa magari katika barabara hiyo.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment