Image
Image

Utumbuaji majipu wa Rais Magufuli waivutia TUCTA.

SHIRIKISHO la Vyama Huru vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) limeunga mkono kazi inayofanywa na Rais John Magufuli na Waziri Mkuu wake, Kassim Majaliwa kwa kuwa kinachofanywa na viongozi hao, ndicho ambacho wafanyakazi wamekuwa miaka yote wakitaka Serikali zilizotangulia, zifanye ili maslahi yao yawe mazuri.
Kaimu Katibu Mkuu wa Tucta, Hezron Kaaya alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari katika makao makuu ya Tucta, Dar es Salaam. Tangu ashike madaraka siku 28 zilizopita, Rais Magufuli amevutia wengi katika utendaji wake baada ya kuamua kushughulikia kwa haraka matatizo yanayogusa maisha ya Watanzania wengi.
Alianzia kwa ziara ya kushitukiza katika Hazina ya Taifa (Wizara ya Fedha), kabla ya kushitukiza kwa ziara ya Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na kisha kwa kupitia Waziri Mkuu Majaliwa akaibukia katika Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ambako uliibuliwa ufisadi wa makontena ulioleta hasara ya Sh bilioni 80.
Aidha, Dk Magufuli alipiga marufuku sherehe za Sikukuu ya Uhuru na maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani, na kupiga marufuku uchapishaji wa kadi za sikukuu za Krismasi na Mwaka Mpya kwa gharama za fedha za umma. Amezuia pia safari holela za watumishi wa umma nje ya nchi, akitaka zifanyike kwa kibali maalumu.
Awali pia aliagiza fedha zaidi ya Sh milioni 200 zilizokuwa zitumike kwa ajili ya mchapalo wa sherehe za uzinduzi wa Bunge la 11 mwishoni mwa mwezi uliopita, zitumike kwa ajili ya kununua vitanda vya wagonjwa katika Hospitali ya Muhimbili na fedha za Uhuru zitumike kupanua barabara ya Bagamoyo jijini Dar es Salaam katika kipande cha kutoka Morocco kwenda Mwenge.
Ni kutokana na utendaji huo, Tucta kupitia kwa Kaaya imesema mara zote wamekuwa wakiiambia Serikali kuwa ina uwezo wa kulipa wafanyakazi wake mishahara mizuri kama itakusanya mapato yake inavyotakiwa. “Bila shaka hatukueleweka.
Tulisema suala la ukusanyaji hafifu wa kodi, tulisema suala la wakwepaji wa kodi, wizi wa fedha za umma, misamaha ya kodi na ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma kwenye halmashauri zetu,” alisema Kaaya akizungumzia hatua kali alizoanza kuchukua Dk Magufuli katika kukusanya na kudhibiti mapato.
Kaaya alisema Tucta inaunga mkono kasi ya ‘kutumbua majipu’ na kuwataka Watanzania wote wenye nia njema na taifa hili kuunga mkono kazi hiyo kubwa ya Rais Magufuli ya kurejesha nchi mahali pake.
Hata hivyo, alikemea na kukataa mtindo ulioibuka hivi karibuni kwa watawala kutumia nafasi zao kuwakandamiza wafanyakazi kwa kisingizio cha kaulimbiu ya Rais Magufuli ya ‘Hapa Kazi Tu.’
Alisema kauli hiyo ya rais wote wanaikubali na wameona inavyofanya kazi, lakini wapo viongozi wachache wenye madaraka wanaotumia kaulimbiu hiyo, kujionesha kuwa wanakwenda sambamba na kasi ya Magufuli.
Alisema hivi karibuni kuna mkuu wa wilaya ambaye aliamuru maofisa wa ardhi watupwe rumande, amri anayoieleza haikuwa sahihi na ilikwenda kinyume cha sheria za kazi na haki nyingine za msingi za binadamu.
“Wale wafanyakazi hawakutenda kosa lolote la jinai. Sheria na taratibu za kazi ziko wazi kuhusu hatua za kinidhamu kwa wafanyakazi wanaokiuka maadili ya kazi. Tucta tunalaani kitendo hicho na wafanyakazi hao wana haki ya kumshitaki mkuu huyo wa wilaya na sisi tunawaunga mkono,” alisema Kaaya.
Pia katika kipindi hiki, kiongozi huyo wa Tucta alisema kumekuwa na kauli ya mkuu wa mkoa mmoja, akiwakataza maofisa wake kwenda likizo, eti kwa vile rais yuko kazini na hajakwenda likizo.
Alisema ieleweke kuwa likizo ni haki ya mfanyakazi na kama kuna mwajiri anataka kuzuia likizo hiyo, anapaswa kufanya majadiliano na mwajiriwa ili wakubaliane kulingana na taratibu za sheria zilizopo. Alisema kauli nyingine imeelekeza mashirika ya umma yasiyojiendesha kwa faida, yapunguze wafanyakazi.
“Tunapenda ieleweke kuwa kinachofanya mashirika ya umma yashindwe kujiendesha sio wingi wa wafanyakazi, bali ni uongozi mbovu wa mashirika hayo,” alisema na kuongeza kuwa uongozi mbovu unatokana na uteuzi wa wakuu wa mashirika hayo usiozingatia weledi, bali kujuana na urafiki.
‘Hapa Kazi Tu’ ni kaulimbiu ambayo Dk Magufuli aliitumia wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu na baada ya kuapishwa kuwa rais, amekuwa akionesha utekelezaji wa kauli hiyo kwa vitendo.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment