Image
Image

Chadema kuibuka na mambo matano

Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kitaamua mambo makuu matano katika vikao vyake vya juu vilivyoanza jana jijini Mwanza.
Miongoni mwa mambo hayo ni kutenguliwa kwa kitendawili cha nani atakayerithi nafasi ya katibu mkuu iliyokuwa ikishikiliwa na Dk Willibrod Slaa.
Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari ulioitishwa na uongozi wa Chadema kutoa ratiba ya vikao vya Sekretarieti, Kamati Kuu na Baraza Kuu vinavyofanyika jijini hapa, Mkuu wa Idara ya Habari wa Chadema, Tumaini Makene alisema alisema katibu mkuu wa chama anapatikana baada ya kupimwa kwa vigezo vya ni uadilifu, uwezo kiutendaji, uhodari wa kukabiliana na mikikimikiki ya kisiasa na kuchapa kazi kwa bidi bila hofu, upendeleo wala kuyumbishwa.
Alinukuu kifungu cha 7.7.13 cha katiba ya chama hicho akisema kinatoa mamlaka kwa mwenyekiti kupendekeza na kuwasilisha majina yasiyozidi mawili ya wanachama wanaofaa kushika wadhifa huo na mmoja wao atapitishwa na Baraza Kuu kwa kupigiwa kura.
“Hadi sasa, mwenye siri ya nani atakuwa Katibu Mkuu wa Chadema ni Mwenyekiti, Freeman Mbowe. Wengine wanapiga ramli kwa kubashiri,” alisema na kuongeza:
“Kama mambo yatakwenda yalivyopangwa, mwali (katibu mkuu), atajulikana usiku wa Jumamosi Machi 12 wakati wa kikao cha pili cha Kamati Kuu; na kutangazwa hadharani kwenye mkutano wa hadhara Jumapili Machi 13,” alisema Makene.
Makene alisema mambo mengine makuu yanayotarajiwa kujadiliwa na kuamuliwa ni mpango mkakati wa kisiasa wa miaka mitano kuanzia sasa hadi 2021 utakaohusisha namna chama hicho kitakavyokabiliana na vyama vingine katika uchaguzi wa 2020.
“Vikao vya Mwanza pia vitajadili na kupitisha bajeti ya chama kwa kipindi hicho pamoja na matumizi ya ruzuku katika kuimarisha shughuli za chama kuanzia ngazi ya msingi hadi Taifa,” alisema.
Alisema vikao hivyo, hasa kile cha Baraza Kuu ambacho kinafanyika nje ya Dar es Salaam kwa mara ya kwanza katika historia ya chama hicho, pia kitajadili na kupitisha marekebisho ya katiba, kanuni na miongozo ya mabaraza.
“Suala la utawala wa sheria chini ya Serikali ya Awamu ya Tano, matumizi ya vyombo vya dola dhidi ya wanachama na viongozi wa Chadema pamoja na mbinu za kuminya demokrasia pia vitajadiliwa na kuamuliwa hatua za kuchukua,” alisema.
Chanzo: Mwananchi
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment