Image
Image

Tumuunge Mkono MAKONDA katika kuwaondoa Ombaomba jijini Dar es Salaam.


JUZI Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alisisitiza nia yake ya kutaka kulifanya Jiji la Dar es Salaam kuwa bora katika suala la usafi, utulivu na amani kwa ujumla.
Alisema amejipanga kuanza na mambo matatu, la kwanza likiwa kuwaondoa ombaomba wa barabarani, kuwabana wamiliki wa majengo makubwa yaliyojengwa kinyume na taratibu pasipokuwa na sehemu za kuegesha magari na kuwaamuru wamiliki wa baa kutopiga muziki nje ya utaratibu wa vibali vyao.
Mikakati hiyo imekuwa baada ya ule wa awali wa kuwataka wakazi wa jiji hilo kuhakiki silaha zao ndani ya miezi mitatu, kabla ya kuanza msako, lengo likiwa ni kuhakikisha matukio ya uhalifu yanapungua na ikiwezekana yanatoweka Dar es Salaam.
Kwa hakika, tunaungana na juhudi zenye nia njema zinazofanywa na Mkuu wa Mkoa katika kuhakikisha Dar es Salaam inakuwa mahali salama pa kuishi. Tukianza na hili la ombaomba, ni ukweli usiofichika kwamba kwa muda mrefu wamegeuka kero katika jiji hilo ambalo ni sura ya nchi kutokana na kuwa na shughuli nyingi za kiuchumi na kiutawala.
Mbali ya kuchafua mazingira katika maeneo mbalimbali ya mji wanayoyageuza kuwa makazi, ikiwa ni pamoja na majengo na ofisi za umma katikati ya Jiji, vituo vya mabasi, kwenye makutano ya barabara na kadhalika, ombaomba wanatajwa pia kuwa mawakala wa wahalifu.
Wanatajwa kushirikiana kwa kiasi kikubwa na wahalifu nyakati za usiku, lakini pia ombaomba hao wanatumika katika biashara haramu, zikiwemo za kusambaza dawa za kulevya. Na wakati mwingine, baadhi ya vijana ambao mchana huonekana kama wenye shida za kweli na hivyo kustahili kusaidiwa angalau mkono uende kinywani, hugeuka vibaka hatari katika maeneo mengi ya katikati ya mji.
Hivyo basi, tunaamini hatua ya kuwaondoa watu wa aina hii ambao baadhi yao huelezwa hugeuka ma`pedeshee’, itasaidia harakati za kuliweka jiji katika hali ya usafi, lakini pia ni sehemu ya mkakati wa kupunguza matukio ya kihalifu.
Aidha, katika kuhakikisha Dar es Salaam inakuwa na utulivu na amani nyakati za usiku, suala la udhibiti wa kelele katika kumbi za starehe na kwenye baa, nalo lina uzito mkubwa, kwani ni moja ya kero kwa wakazi wa jiji hilo.
Wengi wa wamiliki wake hupiga muziki kwa sauti kubwa, tena kwa zaidi ya saa zilizowekwa kisheria, hivyo kuathiri kwa kiasi kikubwa wakazi katika maeneo husika, tena bila ya vibali vya kufanya hivyo.
Mbali ya kusababisha usumbufu kwa wakazi wa Jiji karibu siku zote za wiki, maeneo haya hugeuka pia maficho ya wahalifu. Hivyo, tunaamini ni sahihi wahusika wakibanwa ili wafanye shughuli zao ndani ya wakati unaokubalika kwa mujibu wa sheria.
Ndiyo maana tunasema kwa haya machache anayoanza nayo Mkuu wa Mkoa, ni vyema akaungwa mkono ili kumsaidia kurudisha hadhi ya Jiji la Dar es Salaam katika suala la usafi, amani na utulivu.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment