Image
Image

Wananchi wajenge tabia ya kudai risiti wanaponunua vitu.

WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, juzi alisoma bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha wa 2016/17, ambayo ni ya Sh trilioni 29.54.
Bajeti hii ni ya kwanza tangu, Rais John Magufuli, aingie madarakani baada ya kushinda uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba, mwaka jana.
Rais Magufuli ameanza kazi ya kutimiza ahadi zake na kutekeleza ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Bajeti ya mwaka wa fedha 2016/17 inaonyesha kuwa mapato yatokanayo na kodi yatakua kiasi cha Sh. trilioni 15.11 sawa na asilimia 13.8 ya Pato la Taifa.
Mapato ambayo hayatatokana na kodi yanatazamiwa kufikia kiasi cha Sh. trilioni 2.69.
Dk. Mpango alisema makisio ya makusanyo yanayotokana na kodi ni makubwa kutokana na serikali kuamini kuwa Mamlaka ya Kodi Tanzania (TRA) ina uwezo wa kukusanya fedha nyingi.
Serikali imepania kwa kiasi kikubwa kuziba mianya yote, ambayo imekuwa ikichangia ipoteze mapato mengi.
Katika kuhakikisha kuwa serikali inaongeza nguvu katika kukusanya mapato ya ndani imeandaa mikakati ya kubana wakwepa kodi.
Serikali imepanga kubana wafanyabiashara wanaokwepa kodi kwa kugawa mashine za risiti za TRA (EFD).
Imepanga kugawa mashine hizi kwa wafanyabiashara wakubwa na wale wa kati ili kudhibiti ukwepaji kodi.
Serikali imeonya kuwa wale wote watakaokwepa kutumia mashine hizi watachukuliwa hatua kali za kisheria.
Wananchi wana mchango mkubwa katika jambo hili la kuhakikisha wafanyabiashara wanatumia mashine hizi za risiti za TRA.
Kwa miaka mingi, wananchi wa Tanzania wamekuwa wakihudumiwa bila ya kujali suala la kupewa risiti.
Tabia hiyo kwa kiasi kikubwa imechangia kwa kiasi kikubwa kwa serikali kupoteza mapato mengi.
Wananchi wanapaswa kuhakikisha kuwa wanabadili tabia ya kuchukulia mambo ya kirahisi wakati huo huo kutaka serikali ilete maisha bora kwa kila mtanzania.
Tunapongeza uamuzi wa serikali kugawa bure mashine za EFD, kwani kumesaidia kuondoa manung’uniko waliokuwa wanadai kuwa ni aghali.
Malalamiko hayo yalisababisha kuzuka kwa mvutano mkubwa kati ya wafanyabiashara na serikali.
Kwa kitendo cha serikali kutoa mashine hizo, ina maana hakuna tena kisingizio bali jambo hili linatakiwa utekelezaji tu.
Msaada mkubwa katika kufanikisha jambo hili utatoka kwa wananchi, ambao wanapaswa kuhakikisha kila wanaponunua vitu basi wanadai risiti.
Aidha, utaratibu huu wa utoaji risiti unamfanya mwananchi anaponunua bidhaa na akapewa risiti kuwa na uhakika kuwa kodi iliyolipwa inafika serikalini na kinyume cha hapo kodi hiyo anabaki nayo mfanyabishara.
Pamoja na nia hii njema ya kuleta uwazi na kurahisisha ukusanyaji wa mapato ya serikali katika zoezi hili wengi wameitikia wito huo wa serikali kwa kununua mashine za risiti.
Zoezi hili lina nia nzuri kwa wafanyabishara kwa kurahishisha utunzaji wa kumbukumbu za kibiashara na hivyo, kupunguza au kuondoa kabisa misiguano wakati wa ukokotoaji wa kodi na kuleta uwazi kwa mfanyabishara bila kuonewa au mapato ya serikali kupotea.
Mfanyabiashara au mwananchi yeyote anapolipa kodi sahihi inaleta manufaa katika maendeleo ya nchi kwa mfano ujenzi wa miundo mbinu, kugharimia elimu, huduma za afya, usalama wa raia na mali.
Kuna faida nyingi za kutumia mashine hizi kwa mfano imempungumzia mfanyabiashara huyu alilazimika kuchapisha vitabu vya risiti kwani kwa kutumia mashine hizi anaondokana na uchapishaji wa vitabu ambavyo ni vingi na utunzaji wa nakala zake unaleta usumbufu.
Pia zina uwezo mkubwa wa kutunza kumbukumbu za mauzo, manunuzi na mali za biashara bila kufutika kwa muda usiopungua miaka mitano.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment