WAZIRI
MKUU Kassim Majaliwa amewataka wakurugenzi watendaji wateule 185 wa
majiji, manispaa, miji na halmashauri za wilaya waende wakafanye kazi
kwenye maeneo yao mapya waliyopangiwa kwa kuzingatia uadilifu,
uwajibikaji na uaminifu.
Waziri Mkuu ametoa wito huo leo (Jumanne,
Julai 12, 2016) wakati akizungumza na wateule hao kabla hawajatoa viapo
ya maadili katika hafla iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.
“Jukumu
mlilopewa na Mheshimiwa Rais ni nyeti na linahitaji utulivu na
kujituma. Kila mmoja wenu anatakiwa akafanye kazi kwa uadilifu,
uwajibikaji na uaminifu,” amesema Waziri Mkuu na kuongeza:
“Ninyi
ndiyo injini ya maendeleo katika Halmashauri zote hapa nchini na pia mna
dhamana ya kusimamia fedha za maendeleo katika halmashauri zenu.
Mtajikuta mna jukumu la kusimamia fedha za ndani pamoja na fedha
zinazotoka Serikali Kuu. Hakikisheni mnasimamia matumizi ya fedha hizi
ili kupata value for money.”
Waziri Mkuu aliwataka wawe makini wasije
wakajikuta wanaingia kwenye migogoro ya kifedha dhidi ya watendaji
wengine, migogoro ya kikazi na pia migogoro na wananchi wanaoenda
kuwaongoza.
“Mkifika huko ninawasihi mshirikiane na wadau wengine
ambao ni wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, kamati za ulinzi na usalama,
wakuu wa idara, watumishi wa idara mbalimbali zilizo chini yenu na
watendaji wa kata na vijiji”, alisema.
Alisema wanatakiwa wakasome
taarifa mbalimbali ili waelewe majukumu yao pamoja na mipaka yao,
waelewe maeneo yao ya utawala ni yapi lakini pia wajipange kusimamia na
kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwani imebeba ahadi zilizotolewa
na Rais pamoja na Makamu wa Rais wakati wa kampeni za uchaguzi.
Aliwaasa
pia wasiache kutafuta hotuba ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya
kuzindua Bunge la 11, aliyoitoa Novemba 20, mwaka jana na kuwataka
waisome na kufanyia kazi maeneo yote aliyoyaainisha kwa vile inatoa dira
ya utendaji katika maeneo yao.
Kwa upande wake, Makamu wa Rais, Mama
Samia Suluhu Hassan aliwataka wateule hao watambue dhamana waliyopewa
kuwa viongozi wa halmashauri na kwamba wanakwenda huko kuwa watumishi wa
umma na siyo watawala.
“Wewe ni mtumishi wa watu, na watu hao pia
wana wawakilishi wao ambao ni madiwani. Kwa hiyo fanyeni kazi kwa karibu
na madiwani, sikilizeni shida za wananchi na pangeni vipaumbele vya
kazi na pia msiache kujifunza. Soma wajibu wako kisheria na kikatiba ni
upi lakini pia jipe muda wa kujifunza,” alisisitiza.
“Wewe ni
kiongozi kwa hiyo tengeneza watu wako ili wakusaidie kutekeleza kile
ulichotumwa kufanya. Fanyeni kazi kwa bidii kwa sababu Tanzania inaenda
kwa spidi sana lakini pia mjihadhari na kashfa za matumizi mabaya ya
fedha. Msisahau kuwa fedha ni fedheha, ukiitumia fedha vibaya utapata
fedheha…” aliongeza.
Akiwahutubia wateule hao, Rais Dkt John Pombe
Magufuli aliwataka wawe ni watatuzi wa kero za wananchi badala ya kuwa
watengeneza kero na akasisitiza wawe mitume wazuri kwa wananchi.
“Kaondoeni
kero kwa wananchi wa hali ya chini, wako huko wanatozwa kodi ndogondogo
hata za kuuza mchicha tu. Mtu akivuna mpunga wa kula nyumbani kwake pia
anatozwa kodi, ni lazima kodi hizi mkazizuie kwa sababu tuliahidi
kupunguza kero kwa wananchi na siyo kuongeza kero kwao,” alisema.
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)


0 comments:
Post a Comment