Tunatambua kwamba viongozi wa nchi wanachama wa
Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) walikutana Dar es Salaam, wiki mbili
zilizopita, kwa lengo la kujadili mgogoro wa Burundi. Tunatambua pia kwamba
siku waliyokutana ndiyo lilitokea jaribio la kumpindua Rais Pierre Nkurunziza,
hali ambayo ilivuruga hata ajenda na maazimio ya kikao.
Badala ya kutoka na maazimio mazito yenye lengo la
kuupatia ufumbuzi mgogoro ulioibuka kutokana na Rais wa nchi hiyo kutaka
kuwania muhula wa tatu wa uongozi kinyume cha Katiba yao, waliishia kulaani
jaribio la mapinduzi ambalo licha ya kushindikana, lilichochea maandamano
zaidi, mapambano zaidi kati ya askari na raia na mauaji zaidi.
Taarifa zilizopo zinaonyesha kwamba zaidi ya watu 20
wameuawa na wengine zaidi ya 431 kujeruhiwa huku mamia kwa maelfu ya raia wa
Burundi wakikimbia kuwa wakimbizi katika nchi za Rwanda, Jamhuri ya Kidemokrasi
ya Kongo na Tanzania.
Haya yote yanatokea kwa sababu ya kukiukwa kwa
Makubaliano ya Amani yaliyofikiwa mjini Arusha kwamba kiongozi mkuu wa nchi
hatakaa madarakani kwa zaidi ya vipindi viwili vya miaka mitano mitano.
Wananchi wanaotaka makubaliano hayo ya amani yaheshimiwe, baada ya rais huyo
kutawala vipindi viwili vya miaka mitano mitano, ndiyo wanaoandamana na baadhi
yao kuishia kupigwa risasi; wanajeruhiwa na kuuawa.
Madhara ya uamuzi huo ni kumiminika kwa wakimbizi
katika nchi jirani. Mazingira yamewafanya Warundi kuitoroka nchi yao wakiwa
hawana chakula, fedha, nguo, matandiko wala dawa na wakitembea usiku kucha kwa ajili
ya kusalimisha roho zao.
Kwa hiyo, Tanzania iliyoshiriki kikamilifu kurejesha
amani Burundi kufuatia machafuko ya mwaka 1994, inalazimika kuwapokea tena
wakimbizi ambao taarifa zinaonyesha wamefikia zaidi ya 100,000. Shirika la
Wakimbizi la Umoja wa Mataifa (UNHCR) ndilo linalopaswa kuwaangalia wakimbizi
hao, lakini maadamu wako nchini, huu ni mzigo mkubwa kwa Tanzania.
Kumekuwa na propaganda nyingi za kutaka kuonyesha
kwamba Burundi kuko shwari isipokuwa wakorofi wachache. Propaganda hizo ni
pamoja na mechi iliyoandaliwa Alhamisi iliyopita jijini Bujumbura ambayo ili
kuonyesha kwamba kuna amani ya kutosha na Rais alionekana akicheza mpira,
lakini Jumapili kiongozi wa chama cha upinzani cha Union for Peace and
Develoment, Zedi Feruzi na mlinzi wake waliuawa kwa risasi.
Katika nchi yenye amani hakuna mauaji ya kiholela;
katika nchi yenye utulivu raia hawakimbii na kwenda kuishi kama wakimbizi;
katika nchi inayojali haki, chama tawala hakiwezi kuunda vikundi vya kupiga
watu wanaopinga sera za Serikali. Vilevile, nchi inayojali utawala bora
haifungii wala kuvipiga mabomu vyombo vya habari vya binafsi na nchi inayojali
watu wake haiwezi kuwaacha watembee mwendo mrefu na kufia ugenini tena kwa
magonjwa yanayozuilika kama kipindupindu.
Tunaiomba jumuiya ya kimataifa iongeze juhudi za
kuwasaidia wakimbizi walioko nchini ambao wanakabiliwa na hali ngumu lakini
zaidi tunaomba ziongezwe juhudi kuupatia ufumbuzi mgogoro wa Burundi ili
isiendelee kuzalisha wakimbizi.


0 comments:
Post a Comment