Tume ya Taifa ya Uchaguzi
(NEC), wiki hii imetangaza ratiba ya Uchaguzi Mkuu wa rais, wabunge na madiwani
kwamba Agosti 21 itakuwa siku ya uteuzi wa wagombea hao.
Kwamba, baada ya NEC
kupitisha wagombea walioteuliwa, vyama hivyo vitaruhusiwa kuanza kampeni za
uchaguzi huo siku inayofuata, yaani, Agosti 22 ambazo zitafanyika kwa siku 64
hadi Oktoba 24, mwaka huu. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Uchaguzi Mkuu utafanyika Jumapili ya mwisho wa Oktoba ya mwaka wa
tano tangu ulipofanyika uchaguzi mkuu wa mwisho na kwa mwaka huu, Jumapili ya
mwisho ni Oktoba 25.
NEC imefanya vizuri
kuwafahamisha mapema wadau wa uchaguzi mkuu ambao ni vyama vya siasa lakini
hasa Watanzania kwa ujumla, ambao ndiyo wenye uamuzi wa mwisho wa nani awe
kiongozi wao katika ngazi fulani. Jambo jingine zuri ni kwamba, NEC imetoa
ratiba yake baada ya vyama vya siasa kutangaza ratiba zao za uteuzi wa
wagombea.
Lakini kwa ratiba hii NEC,
inajua changamoto zinazoikabili? Je, ina uhakika kwamba kazi ya uandikishaji
katika Daftari la Kudumu la Wapigakura itakamilika kabla ya kuanza kampeni za
wagombea?
Maswali haya mawili ni muhimu
kwa NEC. Kazi ya uandikishaji wapigakura ilianza Februari 23 mwaka huu katika
Mkoa wa Njombe na lengo lilikuwa kama kazi hiyo ingekamilika kwa wakati
Watanzania, waweze kushiriki kupiga Kura ya Maoni Katiba Inayopendekezwa Aprili
30.
Kazi hiyo ilishindikana na
hivyo Kura ya Maoni ikaahirishwa. Leo ikiwa ni miezi mitatu na siku kadhaa
tangu NEC ianze kazi ya uandikishaji kwa mfumo wa BVR, imekamilisha mkoa huo
mmoja tu wa Njombe kati ya 30 iliyopo. Hata mkoa huo mmoja bado kuna watu ambao
hawakufikiwa.
Pamoja na majigambo ya
viongozi wa Serikali kwamba kazi ile ingefanikishwa katika kipindi kifupi,
ukweli ni kwamba NEC ilikuwa na mashine za BVR 250 tu kati ya 8,000 zilizokuwa
zinahitajika kwa kazi hiyo kubwa. Mbaya zaidi ni kwamba NEC ilianza kazi hiyo
nyeti ikitegemea mashine za kuazima kutoka Kenya na Nigeria waliokuwa na
uchaguzi Machi 28.
Inasikitisha kuona kwamba
hadi sasa NEC imepata mashine zipatazo 4,500 kwa kazi hiyo muhimu. Tunaambiwa
imepeleka mashine hizo mikoa ya Iringa, Mbeya, Ruvuma, Mtwara na Lindi, Rukwa,
Kagera, Singida na Tabora.
Tunaambiwa kazi inakwenda
mchakamchaka lakini katika baadhi ya kata waandikishaji wapigakura wanadaiwa
kuondoa mashine kabla ya kuandikisha watu wote waliojitokeza; maeneo mengine
inadaiwa waliojiandikisha, kadi zao zinasomeka tofauti na vituo
walivyoandikishwa.
Tunaambiwa maeneo yenye watu
zaidi ya 3,000 waliandikishwa chini ya nusu yao huku baadhi ya vijiji, mashine
ziliendelea kutowatambua wenye sugu za vidole.
Wakati NEC inakabiliwa na
changamoto hizo, imetangaza kwamba kampeni za uchaguzi mkuu zitaanza Agosti 22,
ikiwa na maana kwamba hapo NEC itakuwa imekamilisha kazi yake, maana ikiwa
itakuwa bado uandikishaji huo unaweza kuharibika na kuzua sokomoko na taharuki
katika jamii.
Tunaishauri NEC ikamilishe
kazi hiyo mapema ili kampeni zikianza, wananchi wapate fursa ya kwenda
kuwasikiliza wagombea wanavyojinadi na kuuza sera badala ya kujiandikisha. Kazi
ikikamilika mapema, NEC pia itapata muda wa kuhakiki majina na vituo bila
usumbufu mkubwa.


0 comments:
Post a Comment