Image
Image

Uhaba wa mafuta unaendelea kuathiri uchumi wa Nigeria


Uhaba wa mafuta ya petroli umezikumba sehemu mbalimbali za Nigeria kutokana na mgomo ulioitishwa na wasambazaji wa mafuta, na kusema watarudisha usamabazaji wa mafuta hadi serikali itakapowalipa malimbikizo ya madeni yanayofikia dola bilioni 1. Kwa sasa uhaba wa mafuta sio tu unakwamisha magari barabarani, bali pia umeanza kuathiri uchumi.

Uhaba wa Petroli, Dizeli na mafuta ya taa unawaathiri karibu wanigeria wote, hasa wale wenye kipato cha chini wanaotumia mafuta hayo. Lakini hata mashirika ya binafsi na ya umma pia yanaathiriwa kwa kuwa yanatumia petroli na dizeli kuendesha jenereta zao. Mashirika ya umeme ambayo pia yanategemea mafuta hayo kuzalisha umeme, sasa yamepunguza uzalishaji wa umeme na kufikia megawati 1,327 ambacho ni kiwango cha chini kabisa katika historia. Pamoja na kuwa wanigeria wengi wanatumia umeme unaotokana na majenereta binafsi, uhaba wa mafuta umewafanya nao pia washindwe kutumia majenereta yao.

Misururu mirefu ya magari na ya watu wakiwa na madumu ya mafuta imekuwa inaonekana katika sehemu mbalimbali za Nigeria. Baadhi ya safari za ndege za ndani zimekatishwa, na baadhi ya ndege za safari za kimataifa zinalazimika kutua katika nchi jirani ili kuongeza mafuta. Uhaba huo pia umefanya baadhi ya vituo vya Radio vya FM kutangaza kuwa vitasimamisha matangazo, baadhi ya matawi ya benki na mashirika ya simu pia yamesema yatasimamisha huduma zao.

Sababu ya upungufu wa mafuta nchini Nigeria imetajwa kuwa ni mgomo wa wafanyakazi wa mafuta wanaodai malimbikizo ya madeni. Msemaji wa shirika la mafuta la Nigeria Bw Ohi Olegbe amesema walikuwa na akiba ya siku 25, lakini uhaba uliopo umechochewa na mgomo huo. Amesema kutokana na mgomo chama cha madereva wa malori ya mafuta PTD wamegoma kusafirisha mafuta, na wanachama wa chama kikubwa cha wauza mafuta nchini Nigeria wamegoma kununua mafuta kutoka nje. Kutokana na hali hiyo biashara haramu ya mafuta katika mji wa Lagos imeanza kushamiri.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment