Image
Image

Kenya yaadhimisha sikukuu ya Madaraka.


Kenya jana imesherehekea sikukuu ya Madaraka,ambapo imeadhimisha miaka 52 tangu kujitawala yenyewe kutoka utawala wa kikoloni wa muingereza.
Sherehe hizo ziliandaliwa katika uwanja wa kitaifa wa Nyayo,ambapo zaidi ya watu 30,000 walihudhuria.
Sherehe hizo zilihudhuriwa na viongozi mbalimbali nchini Kenya wakiongozwa na Rais Uhuru Kenyatta, na Naibu Rais William Ruto.
Aidha Rais wa Uganda Yoweri Museveni na Naibu Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa,waziri wa mambo ya nje wa Ethiopia Balozi Berhane Gebre-Christos ,na Katibu Mkuu wa CCM Tanzania Abdulrahman Kinana pamoja na viongozi wengine walihudhuria sherehe hizo.
Vifijo,shangwe na nderemo zilitanda katika maadhimisho ya 52 ya sikukuu ya Madaraka katika uwanja wa kitaifa wa Nyayo,huku nyimbo za kizalendo zikihanikiza.
Wakenya kutoka matabaka mbalimbali pamoja na wageni walihudhuria sherehe hizi na angalau kupata fursa ya kusikiza hotuba ya rais.
Sikukuu ya madaraka inaadhimishwa kukumbuka siku ambayo Kenya ilipata idhini ya kujitawala kutoka kwa mkoloni.
Katika hotuba yake kwa taifa,Rais Uhuru Kenyatta alisema ulaji rushwa ndio tatizo kubwa linaloikabili Kenya kutokana na idadi kubwa ya maafisa wa umma wanaojikita katika jambo hilo.
Rais Kenyatta aliwahimiza wananchi kusimama kidete na kupinga ulaji rushwa.
Madaraka day 7 "Leo nawahimiza kila mmoja wenu kujitolea kupiga vita tamaduni ya ulaji rushwa,hongo na mambo yote maovu ambayo yanaenda kinyume na maslahi ya umma"
Rais Kenyatta pia aliahidi kwamba serikali yake itafanya ufuatiliaji na kuwachukulia hatua wote waliotajwa katika uchunguzi wa hivi karibuni kuhusiana na ulaji rushwa,suala lililowaathiri baadhi ya maafisa wakuu serikalini ikiwa ni pamoja na mawaziri.
Aidha Rais Kenyatta alisema serikali yake bado inazidi kupambana na wanamgambo wa Al Shabaab na kuzuia usajili wa vijana katika kundi hilo.Alisema kundi hilo kinawalaghai vijana katika misingi ya dini kwa mambo ya uongo.
Kenyatta alitoa wito kwa wananchi kutoa ripoti kuhusu mtu yeyote aliyejiunga na kikosi cha Al Shabaab,kwa sababu wote wanaojiunga na kikosi hicho ni maadui.
Madraka day 9 "Huyu ni adui ambaye ameharibiwa na kutiwa siasa chafu.Sisi sote twaelewa ya kwamba hakuna dini ambayo inamuamini Mwenyezi mungu inaweza kusema inaruhusiwa kuua au kukata mtu kichwa,hiyo ni lugha iliyowekwa na watu wachache kuharibu watoto wetu.Mimi nawaomba wakenya wote lazima tuwe macho"
Aidha Rais Kenyatta aliagiza kwamba asilimia 40 ya bidhaa na huduma zinazotumiwa na serikali lazima ziwe ni za kutoka nchini.
Alisema agizo hilo litaanza kutekelezwa katika mwaka ujao wa kifedha kuanzia mwezi Julai.
"Serikali yangu itahakikisha kwamba katika ujao wa kifedha tutaweka vikwazo vya bidhaa na huduma zote zinazotumiwa na serikali lazima ziwe ni kutoka hapa nchini"
Wakati huohuo Naibu Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa aliomba radhi kwa niaba ya serikali yake kwa wakenya kutokana na mashambulizi ya kibaguzi kwa waafrika yaliyotekelezwa na wananchi wa Afrika kusini nchini humo hivi majuzi.
"Kama mnavyojua hivi karibuni tulipitia wakati mgumu wakati baadhi ya waafrika kusini walipoanza kuwashambulia waafrika wenzao nchini Afrika Kusini.Nasimama hapa kuwaomba radhi kama alivyoomba Rais Jacob Zuma kwa viongozi wa Afrika.Nasimama hapa kuomba msamaha kwa yaliyotokea"
Mariphosa alisema tatizo hilo linashughulikiwa na wakenya pamoja na waafrika wote wanakaribishwa nchini Afrika Kusini wakati wowote.
Naye Rais wa Uganda Yoweri Museveni alisema kwamba kundi la Al shabaab limeshindwa na ndio maana linavamia watu wasio na hatia.
Aidha Museveni alitoa rambirambi zake kwa Kenya kutokana na shambulizi la Garissa lililopelekea vifo vya wanafunzi 145 na maafisa wawili wa polisi.
Siku ya Madaraka huadhimishwa kila mwaka tarehe 1 Juni nchini Kenya.Hii ni siku ambayo Kenya ilipata idhini ya kujitawala yenyewe mwka 1963,kabla ya kupata uhuru kamili na kuwa jamhuri mwaka huohuo mnamo tarehe 12 Desemba.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment