Image
Image

Mafanikio ya elimu yanapimwa kwa vigezo vipi?.


Katika siku za hivi karibuni, Serikali imekuwa ikijigamba kuwa imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuimarisha sekta ya elimu nchini.
Majigambo hayo yametolewa kwa nyakati tofauti na mamlaka mbalimbali za Serikali, akiwamo Rais Jakaya Kikwete aliyesema kuwa Serikali yake inajivunia maendeleo katika sekta ya elimu.
Hata jana, Bunge la bajeti linaloendelea mjini Dodoma lilielezwa kuwa sekta hiyo imefanikiwa kwa asilimia 81 na hivyo kushika nafasi ya kwanza ya utekelezaji wa awamu ya kwanza ya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Awali, Rais Kikwete katika hotuba yake aliyoitoa katika Uchaguzi Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), uliofanyika jijini Arusha Mei 28, alisema Serikali yake inajivunia mafanikio makubwa katika sekta ya elimu, licha ya kwamba bado zipo changamoto zinazopaswa kufanyiwa kazi.
Alielezea mafanikio hayo kuwa ni pamoja na uanzishwaji wa programu za walimu wa kozi za muda mfupi au walimu wa leseni, ongezeko la kiwango cha uandikishaji wanafunzi, ujenzi wa maabara na kuondoa utitiri wa vyombo vya kuhudumia madai ya walimu.
Pamoja na mafanikio haya, ni ukweli usio na shaka kuwa uanzishwaji wa programu za kozi za muda mfupi za ualimu, ni sababu mojawapo ya kushuka kwa kiwango cha elimu nchini. Hili limekuwa likilalamikiwa mara kwa mara na wadau wa elimu.
Kimsingi, Watanzania hawajasahau makovu waliyoyapata kutokana na walimu wa UPE na wale wa ‘vodafasta’.
Katika risala yao, walimu hao walipendekeza mambo tisa ambayo walitaka Serikali iyafanyie kazi ili kuboresha sekta ya elimu.
Baadhi ya mambo hayo waliyoyatoa kama wito kwa Rais Kikwete ni kufanyia mabadiliko ya mafao ya pensheni, uboreshwaji wa idara za ukaguzi wa shule na urejeshwaji wa posho za kufundishia.
Hata hivyo, wakati Rais Kikwete na mamlaka nyingine za Serikali zikieleza mafanikio hayo, Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii imesema hadi kufikia Machi, baadhi ya taasisi zilizopo chini ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi zilikuwa hazijapata hata fedha za maendeleo.
Kamati hiyo imeeleza pamoja na kuwapo kwa takwimu za mafanikio, wanafunzi bado wanakaa chini kwa kukosa madawati, bado kuna uhaba wa walimu, madarasa na vifaa vya kufundishia, huku karo katika shule binafsi zikiendelea kuwa juu.
Matatizo hayo ndiyo yaliyoifanya kambi rasmi  ya upinzani bungeni kuhoji aina ya uwekezaji uliofanyika katika sekta ya elimu hadi ikafikia mafanikio makubwa ya kujivunia kama inavyoelezwa na mamlaka hizo za Serikali.

Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment