Image
Image

Ukawa waionya Serikali bajeti 2015/16.

Siku moja baada ya Waziri wa Fedha, Saada Mkuya kuwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka 2015/16, Waziri wa Fedha Kivuli, James Mbatia amesema watawasilisha bajeti yao ambayo kama Serikali itaipuuza, itawagharimu. Mkuya aliwasilisha Bajeti ya Serikali ambayo makadirio yake ni Sh22.4 trilioni.
Akizungumza kwa kifupi jana kwenye Viwanja vya Bunge mjini Dodoma, Mbatia ambaye hakutaka kuingia kwa undani akiahidi mambo yote Jumatatu, alisema kuwa watawasilisha bajeti ikiwa na vielelezo vyote, takwimu zilizofanyiwa kazi, bajeti ndogo lakini inayokidhi na kugusa maisha ya Mtanzania.
Alisema kuwa bajeti ya Serikali imejaa mbwembwe, lakini bajeti ya upinzani inalenga kwenye maeneo ya msingi, yanayomgusa Mtanzania na yenye kueleza maisha nafuu ya Mtanzania. “Tumeangalia tozo katika maeneo mbalimbali, tumeifanyia uchambuzi, inatekelezeka ni bajeti rahisi,” alisema Mbatia ambaye ataiwasilisha kuanzia saa 10:00 jioni.
Baada ya bajeti kusomwa juzi, wabunge walipewa siku tatu ili kupitia maeneo mbalimbali ya bajeti hiyo na kuwasilisha hoja zao kwa ajili ya kuipitisha.
Akizungumza baada ya Mkuya kumaliza kuwasilisha Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2015/16, Spika Anne Makinda ambaye hii ni bajeti yake ya mwisho kuisimamia akiwa Spika, alisema: “Wale mtakaoendelea na Bunge, muifanyie kazi bajeti hii, mhakikishe yote yaliyopendekezwa mnayafanyia kazi.”
“Halafu mje tuijadili hapa. Tutaanza kuijadili Jumatatu kwa siku saba mfululizo. Mje, hata kama mna homa ya uchaguzi, siku saba haziwezi kuwavurugia mipango yenu. Tunataka mje tuijadili, lakini bila matusi. Muungwana siku zote anashindana kwa hoja, mje na hoja zenu, lakini si matusi,” alisema Spika Makinda ambaye tayari ametangaza kutowania tena ubunge katika Jimbo la Njombe Kusini.
Kati ya waliotoa maoni yao ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe ambaye alisema bajeti hiyo haina nafuu kwa Mtanzania masikini. “Haya ni maneno matamu ya kuwahadaa Watanzania kwa kuweka vifungu vya kuwapa matumaini kwao,” alisema akisisitiza ni bajeti ya kampeni za Uchaguzi Mkuu.
Alisema kwamba kambi ya upinzani ilitoa maoni ya kutaka kuanzishwa kwa mafao kwa wazee wote tangu bajeti ya mwaka 2012/2013. Hata hivyo, licha ya kutajwa tena wanafanya maandalizi ya kuweza kutoa pensheni hiyo kwa wazee haitaweza kutekelezeka katika mwaka wa fedha 2015/16.
Alisema haitaweza kutekelezeka kwa sababu hakuna mpango wa kuileta sheria ya pensheni kwa wazee katika Bunge hili. “Hili ni changa la macho kwa wazee hakuna atakayelipwa pensheni katika mwaka ujao wa fedha,” alisema Mbowe ambaye pia ni Mbunge wa Hai (Chadema).
Alisema, katika bajeti hii kuwapo ongezeko la kodi na ushuru wa mafuta nchini wakati bei katika soko la dunia inapungua kila siku kutaongeza gharama za maisha. “Watu wanaweza kufurahi sasa miradi ya umeme vijijini itatekelezeka kwa kuwa fedha hiyo itaenda moja kwa moja Rea (Wakala wa Umeme Vijijini) lakini katika mwaka uliopita, ingawa fedha hizo ziliwekewa uzio, zilichotwa na kupelekwa katika matumizi mengine,” alisema.
Alisema tatizo kubwa la nchi liko katika utekelezaji wa mipango ya serikali. “Nusu ya mawaziri hawapo wakati bajeti yao inasomwa bungeni. Kwa nini wabunge wao hawapo bungeni, sisi wabunge wa kambi ya upinzani wote tulikuwa bungeni,” alisema.
TGNP waichana bajeti
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment