Image
Image

Kidato cha sita watamba.

Wanafunzi 38,853 wamefaulu mitihani yao ya kidato cha sita kati ya watahiniwa 40,753 waliofanya mtihani huo mwaka huu, huku matokeo yakionyesha kuwa shule za Serikali na binafsi zimeenda sambamba.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Baraza la Mitihani la Taifa (Necta) jana, wanafunzi 35 walishindwa kufanya mitihani hiyo baada ya kuugua ghafla.

Akitangaza matokeo hayo mjini Zanzibar jana, katibu mtendaji wa Necta, Charles Msonde alisema kati ya wahitimu waliofaulu, wasichana ni 11,734, sawa na asilimia 98.56 na wavulana ni 27,119, sawa na asilimia 97 ya watahiniwa.

Kwa mujibu wa Msonde, Shule ya Sekondari ya Feza ya jijini Dar es Salaam iliongoza katika orodha ya shule 10 bora inayojumuisha pia shule za Runzewe (Geita), Feza Girls (Dar), Sumbawanga (Rukwa), Ivumwe (Geita), St Mary’s Mazinde Juu (Tanga), Vwawa (Mbeya), Kisimiri (Arusha), Namabengo (Ruvuma) na Scolastica (Kilimanjaro).

Orodha ya shule kumi zilizofanya vibaya inaongozwa na Shule ya Sekondari ya Meta ya Mbeya, iliyoshika mkia ikifuatiwa na Kwiro (Morogoro), Mtwara Tech (Mtwara), Iwalanje (Mbeya), Lugoba (Pwani), Kaliua (Tabora), Kilangalanga (Pwani), Lwangwa (Mbeya), Ilongero (Singida) na Bariadi ya Simiyu.

Msonde alisema kwamba kiwango cha ufaulu kwa matokeo ya kidato cha sita kimekuwa kikiongezeka kila mwaka kutokana na juhudi zinazoendelea kufanywa na Serikali katika kuboresha kiwango cha elimu kwa maendeleo ya Taifa na wananchi wake.

Alisema kwamba matokeo ya mtihani ya mwaka huu yanaonyesha kiwango cha ufaulu kimepanda kwa asilimia 0.61 kutoka asilimia 98.26 mwaka 2014 hadi asilimia 98.87 mwaka 2015.

Alisema kwamba katika shule kumi bora kitaifa, kuna shule tano za Serikali wakati katika orodha ya shule 20 bora, shule 13 za Serikali zimeongoza, zikifuatiwa na shule saba za binafsi.

Hata hivyo, alisema wanafunzi 35 walishindwa kufanya mitihani yao, wakiwamo 10 ambao walishindwa kumaliza mitihani baada ya kuugua na 25 waliougua kabla ya mitihani kuanza na kwamba Necta imeafiki wanafunzi hao warudie mitihani yao Mei mwakani.

“Kati ya wanafunzi hao watano wamefutiwa matokeo ya mitihani baada ya kuthibitika waliingia kwenye vyumba vya mtihani wakiwa na karatasi za kuwasaidia kujibu maswali ya mitihani wakati ni kinyume na sheria,” alisema Msonde.

“Watahiniwa waliofanya vizuri zaidi wamepatikana kwa kulinganisha wastani wa pointi kwenye masomo ya tahasusi pamoja na wastani wa alama za jumla walizopata katika masomo yao,” alisema Msonde.

Msonde alisema kwamba wanafunzi hao wameonyesha uwezo mkubwa katika masomo ya sayansi na kuingia katika kundi la wanafunzi wenye kipaji maalum wa mchepuo wakitoka katika mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment