WAKATI leo ni siku ya mwisho kwa watia nia wa urais kupitia CCM,
makada 33 kati ya 42 wamerejesha fomu huku kila mgombea akizungumzia
tatizo la rushwa namna atakavyopambana nalo.
Makada waliorejesha fomu jana ni pamoja na Edward Lowassa, Mwigulu
Nchemba, Lazaro Nyalandu na Dk Hassy Kitine. Hadi sasa wanachama tisa
ambao wanatakiwa kurejesha fomu hizo hawajarudisha na mwisho wake ni saa
10 kamili jioni.
Wagombea hao ni Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January
Makamba, Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja, Godwin Mwapongo, Balozi
Patrick Chokala na Peter Nyalile.
Wengine ni Ritha Ngowi, Helena Elinewinga, Anthony Chalamila na
Sonoko Banda. Hata hivyo, Katibu wa Sekretarieti Oganaizesheni ya CCM,
Mohamed Seif Khatib alisema hakuna adhabu kwa mtu ambaye atashindwa
kurudisha fomu hizo.
Lowassa
Miongoni mwa wanachama waliorudisha fomu jana ni Waziri Mkuu wa
zamani, Edward Lowassa. Aliporudisha fomu hizo jana alisema amedhaminiwa
na wanachama wapatao 879,000 na kutaka wote wanaomtuhumu kwa ufisadi
kuacha mara moja.
Alisema ikiwa atateuliwa kuwa mgombea urais na kuwa rais atahakikisha
anatumia rasilimali zote kwa faida za Watanzania. Alisema kwa bahati
mbaya watu ambao wanakosa hoja, wamekuwa wakiwatuhumu wenzao kwa vitu
ambavyo havina ukweli wowote.
“Nataka nitumie nafasi hii kwa wale wote ambao wamekuwa wakinituhumu
kwa miaka kadhaa sasa na kunihusisha na suala zima la rushwa, kuwaambia
waache mara moja kwani hakuna hata chembe ya ukweli wa maneno hayo,”
alisema.
Alisema kwa yeyote mwenye ushahidi wa tuhuma hizo autoe. “Aseme
nimechukua rushwa lini, kwa nani, kwa lipi na kwa kiasi gani,”
alisisitiza huku akisema ni majungu na sasa yametosha na ikiwa
atateuliwa, ataongoza nchi kwa haki.
Alisema ana shauku kuunganisha uwezo wa kila Mtanzania katika
kupambana na umaskini wa nchi, umaskini wa watu siyo amri ya Mwenyezi
Mungu kwani kwa pamoja raslimali, maarifa na ufanisi zaidi vitatokomeza
umaskini.
Hata hivyo, waandishi wa habari hawakupewa nafasi ya kumuuliza maswali kutokana na muda aliokuwa ametengewa kuisha.
Dk Asha-Rose Migiro
Mwanachama mwingine aliyerudisha fomu jana ni Dk Asha-Rose Migiro
ambaye alisema hayuko tayari kuzungumza na waandishi wa habari.
Eldefonce Bilohe
Pia mkulima kutoka Kigoma, Elfonce Bilohe naye alirejesha fomu
akikishukuru chama kwa demokrasia iliyoionesha. Bilohe alisema hayo
wakati akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kurudisha fomu.
Alisema yeye ni mkulima lakini amepata nafasi ya kushiriki katika
kinyang’anyiro hicho, kitendo ambacho kweli kimeonesha kuwa ni chama cha
wakulima na wafanyakazi.
Aizungumzia zoezi la kutafuta wadhamini, amesema limeenda vizuri na
amekabidhi idadi ya wadhamini waliohitajika kutoka katika mikoa 15 kama
chama kilivyotaka. Alisema alikutana na changamoto ya kuombwa rushwa.
“Changamoto kubwa ambayo nimekutana nayo katika kuwapata wadhamini ni
baadhi ya watu kuniomba kitu kidogo kama maji ya kunywa,” alisema.
Waziri Nyalandu
Mwingine wa CCM aliyerudisha fomu jana ni Waziri wa Maliasili na
Utalii, Lazaro Nyalandu. Akizungumza na waandishi wa habari alisema ana
imani na Watanzania na yupo tayari kuhakikisha CCM inashika dola mwaka
2015.
Alisema kila alipokuwa akipita ameona watu wakiwa na mapenzi makubwa
na chama chao na hiyo ni ishara kuwa bado wana imani na chama chao.
Akizungumzia kuhusu umoja uliopo katika Taifa alisema kuwa ni lazima
kuhakikisha tunu hiyo inalindwa na kuenziwa na kusisitiza kuwa ni lazima
kupiga vita ubaguzi wa aina yoyote.
Luhaga Mpina
Kwa upande wake mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina alisema ametembelea
mikoa 17 na kusema zoezi lililenda vizuri. Alitoa ushauri kwa CCM kuweka
mdahalo kwa wagombea wote wa nafasi ya urais ili kujua nini ambacho
watakifanya kwa Watanzania.
Alisema kuwa hana presha na wagombea 42 ambao wamekwishachukua fomu
na anaamini kuwa atashinda. Alisema anaamini jina lake litakuwepo katika
tatu bora kwa wale watakaoteuliwa na chama.
Malick Malupu
Mwanachama mwingine aliyerudisha fomu ni Malick Malupu, mwanafunzi wa
shahada ya uzamili ya utumishi wa umma Chuo Kikuu cha Mzumbe alirudisha
fomu aliwataka wagombea wenzake kuwa makini na wapambe wao kwani
wanaweza kusababisha mtafaruku au mgongano baina yao. Alisema kama kuna
mtu anamuabudu mgombea aachane na chama.
“Ukiona mtu anakatwa jina lake akalalamika ujue ameingia kwa hujuma au kwa njia ya ubatili pamoja na kutoa rushwa,” alisema.
Dk Hamisi Kingwangala
Mbunge wa Nzega, Dk Hamisi Kingwangala naye alirudisha fomu na kusema
amefanikiwa kupata wadhamini kama ilivyo agizo la chama. Alisema
atahakikisha anashughulikia suala la rushwa na ufujaji wa fedha za umma.
Dk Kitine na kesi za rushwa Wakati akirudisha fomu hizo za kuwania
kuteuliwa kuwa Rais wa Tanzania, Dk Kitine alisema rushwa ni sehemu
ndogo ya ufisadi na kupambana na vitu hivyo kunategemea ushirikiano.
“Rushwa imetapakaa sana na sababu kubwa ya kuamua kuchukua fomu ni
pamoja na kuhakikisha nikiwa kiongozi napambana na kukomesha rushwa na
ufisadi katika nchi,” alisema. Alisema atahakikisha wahusika wa vitendo
hivyo wanakamatwa na kufikishwa mahakamani.
Alisema atapeleka bungeni sheria hiyo ili ipitishwe kwani itakomesha
kabisa vitendo hivyo kwa kuwa vitawabana wahusika na itatosha kuwa na
ushahidi wa kimazingira yaliyosibu mpaka mhusika kupelekwa mahakamani na
itatosha mtu kupatikana na hatia.
Alisema jaji au hakimu hawatapewa uhuru wa kuamua adhabu ya kesi za
rushwa. ‘‘Tutatengeneza sheria na hatutampa uhuru Jaji au Hakimu kuamua
kesi hizo. Hakimu atakuwa na maagizo kutokana na sheria husika, yeye
hana uhuru wa kutoa adhabu anayoitaka yeye adhabu itakuwa kwenye
sheria,” alisema.
Alisema kwenye sheria hiyo mtoa rushwa na mpokea rushwa wote
watashtakiwa na watahukumiwa wa makosa waliyofanya. Dk Kitine alisema
rushwa imekuwa chanzo cha matatizo yote yaliyo katika nchi hii.Alisema
wakati akitafuta wadhamini alipata ushirikiano mkubwa kutoka kwa
wananchi.
Mwigulu kuibadilisha Takukuru
Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba wakati anarudisha jana fomu na
kusema atapambana na rushwa ambayo imekuwa ikipoteza haki za masikini.
Alisema katika awamu zilizopita wamejitahidi kupambana na rushwa kwa
kuanzisha Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), lakini
alisema atabadilisha sheria namba 11/2007 kwani inaleta rushwa juu ya
rushwa kuna kipindi kirefu ambacho kimekuwa kikitumia kabla ya mtu
kushtakiwa.
“Sheria itabadilika na rushwa itakuwa ni janga maalumu na kuondokana
na uchunguzi juu ya uchunguzi. Tutaipa mamlaka taasisi inayofanya jukumu
la kukamata na kuondokana na uwezekano wa kutoa mwanya wale
wanaokamatwa na kuondokana na uwekezano wa mtu kutumia hela za rushwa
kumaliza kesi za rushwa,” alisema.
Pamoja na rushwa, mgombea huyo aliahidi kupunguza tatizo la ajira kwa
kiasi kikubwa iwapo nia yake ya kuingiza nchi kwenye uchumi wa kati
itafanikiwa.
Mwigulu alisema uchumi wa viwanda utachochea kwa kiasi kikubwa
kuongezeka kwa viwanda vya usindikaji ikiwemo wa mafuta ya alizeti na
viwanda vingine.
“Kukiwa na soko la uhakika mazao na kukiwa na viwanda kwenye maeneo
hayo na vijana wengi watakwenda hapo na kutengeneza ajira kwa wakati
moja,” alisema.
Pia alisema uwepo wa viwanda kutapelekea kuzalishwa kwa bidhaa nyingi
na kutachochea sekta binafsi kutengeneza mazingira mazuri ya biashara
kwa kuondokana na mfumo wa kodi unaokatisha tamaa, rushwa na ukiritimba
vijana wengi watakuwa na cha kufanya.
Akizungumzia mabadiliko ya katiba, alisema hakuna haja ya kugombana
kwani katiba si Biblia au Kurani ambazo hazifanyiwi mabadiliko, lakini
katiba inaweza kufanyiwa mabadiliko.
Alisema hata kuna nchi ziliwahi kuharibikiwa zikiwa na katiba, lakini
katiba halisi inakaa moyoni. “Twende kwenye taratibu za kisheria
tumalizie suala hili na si kwenda kwenye taratibu za kifujo kwenye
sheria hapo tutamaliza tofauti na tafsiri nzuri na kupata kile
tunachokipata,” alisema
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)


0 comments:
Post a Comment