Dk Migiro alikutana na kimbuga cha upinzani ikiwa
ni siku moja baada ya Bunge la 10 kuigomea Serikali ilipotaka kuingiza
bungeni miswada mitatu iliyohusu Wizara ya Nishati na Madini wakisema
inahitaji muda mzuri.
Mapema jana, Dk Migiro aliwasilisha ndani ya Bunge
muswada huo akilitaka lijadili na kuupitisha ili kutoa nafasi ya
kuwalinda watu wa aina hiyo.
Akiwasilisha maoni ya upinzani bungeni, msemaji wa
kambi hiyo katika Wizara ya Katiba na Sheria, Tundu Lissu alisema
muswada huo hauna tija kwa muda huo kwani unatoa nafasi finyu kwa
wabunge kujadili jambo ambalo ni muhimu zaidi kwa wananchi.
Lissu ambaye pia ni mbunge wa Singida Mashariki
(Chadema), alisema uharaka wa muswada huo ni kiashiria tosha kwamba
Serikali inataka kuminya uhuru wa wabunge kupitia kwa kina sheria hiyo.
“Kanuni zinasema kuwa, sheria inaweza kupitishwa
kwa hati ya dharura ikiwa tu kuna mambo ambayo yanataka kutokea ambayo
ni pamoja na majanga au vita. Je, kuna uharaka kiasi gani wa kupitisha
muswada huu?” alihoji Lissu.
Mbunge huyo mbali na kutoa ufafanuzi katika
vifungu vingi katika muswada huo, lakini alisisitiza kuwa ukipitishwa
utakuwa umewanyima haki watu wa kada ya chini na kuwapa mwanya viongozi
wao.
Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika alipinga
vikali muswada huo pamoja na namna ulivyowasilishwa na akazua mgogoro
mkubwa baina yake na Mwanasheria Mkuu wa Serikali(AG), George Masaju.
Malumbano ya wawili hao yalianzia pale Mnyika
aliposema kuwa Serikali ni dhaifu katika suala zima la utungaji wa
sheria jambo ambalo pia liliamsha hasira za Spika.
Katika hoja zake, Mnyika alipinga jinsi muswada
ulivyokuwa ukitoa upenyo kwa watu kutoa taarifa kwa wakubwa wao badala
ya kuzipeleka kwa vyombo vingine.
“Mfano, muswada unaelekeza mtu kutoa taarifa kwa
kiongozi wake yaani akiwa mfanyakazi wa benki kuu anawezaje kutoa
taarifa za ufisadi wa gavana kwa gavana mwenyewe?” alihoji Mnyika.
AG Masaju alipinga kauli za kuwa Serikali inafanya
vitu dhaifu akisema siyo nia yao, bali wanafanya kazi ya kupeleka
miswada ili wabunge wenyewe ndiyo wafanye uamuzi.


0 comments:
Post a Comment