Image
Image

TFF isiingize siasa za uchaguzi kwenye soka.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetangaza kuwa litamualika Waziri wa Ujenzi, Dk John Pombe Magufuli kuwa mgeni rasmi kwenye ufunguzi wa michuano ya Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki inayoanza mwishoni mwa wiki.

Ikijua wazi kuwa inafanya makosa, TFF ilitoa mifano mingi ya kuonyesha kuwa uamuzi wa kumuita mwanasiasa kuwa mgeni rasmi kwenye ufunguzi wa mashindano hayo ni sahihi na kuwataka wananchi wasilielewe vibaya shirikisho kwa kitendo hicho.

Ni vizuri kuwa TFF imebaini kuwa inafanya makosa yaliyo dhahiri katika kipindi ambacho wanasiasa wanazidi kukomaa na hivyo kujua jambo gani linafanywa kwa hila na jambo gani kwa moyo mkunjufu.

Itakumbukwa kuwa kiongozi wa TFF aliwahi kwenda ofisini kwa mmoja wa wanachama wa CCM waliokuwa wakitajwa kuwania urais, kwa ajili ya kujitambulisha mara baada ya kuchaguliwa kiuongoza shirikisho hilo.

Picha ambayo ilitumwa na TFF kwenye mitandao mbalimbali, ilieleza kuwa kiongozi huyo alienda kumweleza mikakati ya shirikisho. Wengi walijiuliza kama ataenda kuwaeleza wagombea wote wa urais au huyo mmoja.

Kwa hiyo leo tunaposikia tena kuwa shirikisho hilo limemualika Dk Magufuli kuwa mgeni rasmi kwenye ufunguzi wa mashindano ya Kombe la Kagame, picha inakuja ile ile kuwa TFF inaingiza siasa kwenye mpira au kuna kiongozi anataka aitumie TFF kwa malengo binafsi ya kisiasa.

Tunapenda kupinga kitendo hicho cha TFF kuingiza siasa kwenye michezo na hasa kwenye kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu ambacho vyama vya michezo na taasisi nyingine zisizofungamana na upande wowote wa kisiasa zinatakiwa zijitenge kabisa na siasa na wanasiasa.

Tunajua kuwa Dk Magufuli ni waziri, lakini ukweli kwamba hadhi yake imebadilika baada ya kuteuliwa na CCM kuwa mgombea urais, inampotezea sifa hiyo ya kushiriki kwenye shughuli za kijamii zenye chembechembe za kampeni. Kwa sasa huwezi kumtofautisha Dk Magufuli na mgombea urais wa CCM. Dk Magufuli ni mgombea urais wa CCM na mgombea urais wa CCM ni Dk Magufuli.

Kwa hiyo hoja kwamba Dk Magufuli anaalikwa kwa kofia ya uwaziri ni kujaribu kutetea uozo ambao unaonekana dhahiri. Isitoshe, wakati huu hadhi yake ya kuwa mgombea urais kwa tiketi ya CCM ndiyo inakuja kwanza kuliko hata hicho cheo cha uwaziri na hivyo kumuita Dk Magufuli kushiriki kwenye shughuli za michezo ni kumpa jukwaa la kufanya kampeni hata kabla ya muda wake.

TFF ikumbuke kuwa wapenzi wa michezo ni watu wenye itikadi tofauti, mitazamo tofauti na wengine ambao hata ushabiki wa vyama haumo ndani yao. Wote hao wanatakiwa kuunganishwa na michezo na si kutenganishwa. Hivyo, mashabiki hao watakapokwenda uwanjani siku ya ufunguzi wanataka kuona burudani waliyoifuata ndiyo inatawala na si siasa ambazo huwachefua baadhi ya wapenzi wa michezo.

Vyama vya michezo havitakiwi kuwa chanzo cha kubagua au kutenganisha Watanzania, bali kuwaunganisha kwa kuwa moja ya kazi kuu za michezo ni kuunganisha watu badala ya kuwatenganisha.

Hatuoni kwamba itakuwa busara kwa TFF kuwa chanzo cha mapingamizi dhidi ya mgombea urais wa CCM itakapofikia muda huo. TFF na Baraza la Vyama vya Soka vya Nchi za Afrika Mashariki na Kati (Cecafa), ambalo linaendesha mashindano hayo, hawana budi kutafakari upya uamuzi huo na kuubatilisha ili usije kuwa chanzo cha misuguano kwenye Uchaguzi Mkuu.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment