Image
Image

Yanga kufungua na Gor Mahia Kagame.

MABINGWA wa soka Tanzania Bara, Yanga watafungua dimba la michuano ya Kombe la Kagame dhidi ya Gor Mahia ya Kenya Julai 18 mwaka huu.
Michuano hiyo inayoshirikisha mabingwa wa soka kwa nchi za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, inatarajiwa kufanyika Dar es Salaam kuanzia Julai 18 mpaka Agosti 2 mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Katibu Mkuu wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa), Nicholas Musonye alisema maandalizi yote ya michuano hiyo yamekamilika na kwamba itashirikisha timu 13 zilizogawanywa kwenye makundi matatu. Wenyeji Tanzania watashirikisha timu mbili, ambazo ni mabingwa wa msimu wa mwaka 2013/2014 Azam na Yanga.
Yanga iliyotwaa ubingwa wa bara msimu wa mwaka 2014/2015 imepangwa kundi A pamoja na Gor Mahia ya Kenya, Telecom ya Djibouti, KMKM ya Zanzibar na Khartoum ya Sudan. Azam FC ipo kundi C pamoja na Malaika ya Sudan Kusini, Adama City ya Ethiopia na KCCA ya Uganda wakati kundi B lina timu za APR ya Rwanda, Shandy ya Sudan, AAB AFC ya Burundi na Hegaan FC ya Somalia.
“Tunashukuru sana kwa TFF (Shirikisho la Soka Tanzania) kuku bali kuwa wenyeji wetu na safari hii mashindano yatafanyika Dar es Salaam kila kitu kimekamilika, mechi zitaoneshwa moja kwa moja na kituo cha SuperSport na mechi itakayofungua mashindano ni Yanga na Gor Mahia,” alisema Musonye.
Kuhusu zawadi alisema zitakuwa dola za Marekani 60,000, ambapo mshindi wa kwanza atapata dola 30,000 wa pili dola 20,000 na wa tatu dola 10,000.
Rais wa Rwanda, Paul Kagame ndiye mdhamini mkuu wa michuano hiyo kwa muda mrefu, amekuwa akitoa fedha kwa ajili ya zawadi kwa timu tatu za juu.
Akifafanua kuhusu ushiriki wa timu kwenye michuano hiyo, Mwenyekiti wa Cecafa Leodegar Tenga alisema Baraza lake hutoa mialiko kwa vyama vya soka wanachama ambao ndio huchagua timu za kushiriki.
“Sisi kama Cecafa huwa tunatoa mialiko kwa wanachama wetu maana ndio tunaofanya nao kazi, wao ndio wanaamua timu ipi ishiriki… kuhusu timu kuleta timu B, hilo hatuwezi kulikubali kwani kuna mashindano ya watoto ambayo mwaka huu yatafanyika Uganda Desemba, kwa hiyo kama ni timu za watoto zishiriki huko, mashindano haya ni kwa ajili ya timu za wakubwa pekee na tumesisitiza hilo,” alisema.
Tenga alilazimika kutoa ufafanuzi huo baada ya kuibuka kwa minong’ono kwamba Azam inataka kushirikisha timu B kwenye michuano hiyo.
Taji hilo linashikiliwa na El Merreikh ya Sudan iliyoifunga APR kwa bao 1-0 katika fainali zilizofanyika kwenye uwanja wa Amahoro, Kigali Rwanda mwaka jana.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment