Image
Image

Magufuli mgombea urais asiyeogopa ushindani

KUANZIA leo zitakuwa zimebaki siku 11 kabla ya kuanza kwa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa tano wa Tanzania tangu baada ya kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini mwaka 1992.
Katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu, wananchi wa Tanzania bara wanapiga kura kumchagua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wabunge na madiwani. Wakati huo huo wananchi wa Zanzibar wakichagua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Wabunge wa Bunge la Muungano, Wawakilishi wa Baraza la Mapinduzi na Masheha ambao ni sawa na madiwani.
Baadhi ya vyama vya siasa vimeshafanya uteuzi wa wagombea wao kwa ngazi mbalimbali kuanzia ubunge, udiwani na urais, wakati vingine vikiwa katika siku za mwisho za kukamilisha uteuzi huo ili kuwahi siku ya mwisho iliyowekwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ya kupitisha uteuzi huo.
Kwa mujibu wa NEC, muda wa kuchukua fomu kwa wagombea wa urais itakamilika Agosti 20, mwaka huu na siku mbili baadaye kampeni za kusaka kura za Watanzania zaidi ya milioni 23 waliojiandikisha kwa ajili ya kupiga kura siku hiyo ya Oktoba ili kuchagua viongozi wanaowataka.
Chama Cha Mapinduzi (CCM) ni miongoni mwa vyama ambavyo vimefanya uteuzi wa mgombea urais ambao ulifanyika Julai 12, mwaka huu, kilimteua Waziri wa Ujenzi Dk John Pombe Magufuli kuongoza upeperushaji wa bendera ya kijani. Wiki iliyopita Dk Magufuli alikwenda Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuchukua fomu za kugombea ili kutimiza sheria za Uchaguzi ambapo aliandamana na Mgombea Mwenza Samia Suluhu Hassan ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Muungano.
Baada ya kuchukua fomu Dk Magufuli na Samia walirejea katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM Mtaa wa Lumumba ambako walipokewa na umati mkubwa wa wanaCCM wakiongozwa na Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Rais Jakaya Kikwete.
Wagomba hao walitumia fursa hiyo kutoa shukrani kwa maelfu wanachama waliowasindikiza ambapo Magufuli alionesha wazi kuwa amejiandaa vizuri pale aliposema haoni wa kumshinda na kwamba yupo tayari kuanza jukumu kubwa kuwatumikia Watanzania endapo watampatia ushindi katika uchaguzi wa Oktoba 25 mwaka huu. “Kujitokeza kwenu kwa wingi leo ni ushahidi mwingine kuwa CCM itaendelea kutawala.
Niwathibitishie kuwa shida za Watanzania nazijua, mategemeo ya Watanzania ninayo, na ipo misingi mizuri imewekwa chini ya Rais Kikwete,” anasema Magufuli. Anaendelea kusema,” nawaahidi nitakuwa mtumishi wenu sababu ninazijua shida za Watanzania. Watanzania wana tatizo la ajira, hawataki kero za ovyo kama kukimbizana na mama ntilie na bodaboda. Wanataka uchumi wao uwe mzuri, wanataka maisha mazuri zaidi.
Nitayasimamia, nawahakikishia sababu kero hizo nazijua. “Nimekuwa mbunge kwa miaka 20 na kushika nafasi za uwaziri katika wizara mbalimbali hivyo nimepata uzoefu kutoka kwa Rais Kikwete, Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa, Mzee Nyerere, na viongozi wengine. Niko tayari kukipokea kijiti kwa mikono miwili,” Magufuli anasema. “Nataka Mwenyekiti kukuhakikishia kuwa tutashinda, sioni wa kutushinda,” alisema Dk Magufuli mbele ya viongozi, wanachama, mashabiki na wapenzi wa CCM huku akirudia maneno ya “sioni wa kutushinda,” alisema mara tatu.
Alisema atakuwa mtumishi wa Watanzania wote bila kujali dini, kabila, itikadi kwa sababu maendeleo ni ya wote, lakini akawataka wadumishe umoja na amani, na kuwaahidi kuwa hatawaangusha. “Nitapeperusha bendera ya CCM kwa manufaa ya Watanzania wote ili kuwaletea maendeleo kwani maendeleo hayana chama, lakini nitafanya hivyo kupitia CCM kwa sababu naamini rais bora atatoka CCM....Nawaahidi kuwa nguvu zenu, jasho lenu, kuacha kazi zenu leo, na muda wenu mliotumia leo hapa, havitapotea bure.
Nasema hazitapotea bure. Nawaahidi Tanzania yenye neema. Ombi langu kwenu ni kuendelea kudumisha amani na umoja wetu bila ya kujali itikadi zetu, dini zetu wala kabila zetu,” alisema Dk Magufuli na kusisitiza kuwa atakuwa mtumishi wa Watanzania wote. Aliongeza: “Sitawaangusha. Wakati wa kampeni nitasema mengi zaidi, wakati huo nikiwa na Ilani ya Uchaguzi na yale ya pembeni. Lakini lengo langu kubwa ni Watanzania kuimarika kiuchumi zaidi na kuondoa kero zaidi. Wajumbe hawakukosea kuniteua sababu ninazijua shida za Watanzania.
CCM mbele kwa mbele, umoja ni ushindi.” Awali, Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Rais Kikwete alisema chama hicho sio chama cha mchezo na kuvionya vyama vya upinzani kuwa watakiona cha mtema kuni katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba. Alisema CCM itapata ushindi katika uchaguzi huo kwa kuwa imejipanga kwa hoja na imeleta maendeleo nchini, huku akieleza kuwa wapo watu wenye tamaa ya uongozi ambayo imekithiri.
“Sasa kazi ndio imeanza rasmi. Dodoma zile zilikuwa rasharasha. CCM sio chama cha mchezo. Watakiona cha mtema kuni. Kama ni mpira wa miguu, basi tumefunga mabao wakiwa wamesimama. Tumejiandaa vya kutosha na kushinda tutashinda. Uzoefu, maarifa na uwezo wa kushinda tunao,” alisema Rais Kikwete na kuongeza: “Nawataka wanaCCM kujipanga, msimdharau adui yeyote hata akiwa mdogo maadhali yuko upande wa pili shughulikeni naye.
Tumejipanga kwa hoja, tunazo hoja za kuzungumza. Nchi tulivu na maendeleo yanaonekana na duniani kote wanajua kuwa Tanzania inafanya vizuri. Tunao utawala bora, demokrasia na uhuru wa habari. “Hata duniani wanajua hilo na wanaona fahari kushirikiana na Tanzania. Lakini wapo watakaokuwa na tamaa tu, duniani wapo watu wameumbwa hivyo, wengine wanayo tamaa hadi imekithiri, imevuka mipaka,” alieleza Kikwete mbele ya maelfu ya viongozi, wanachama na mashabiki wa chama hicho tawala.
Lakini wakati kampeni zikitarajiwa kuanza siku 11 zijazo, Dk Magufuli licha ya kukiri kufahamu shida na matarajio ya Watanzania, lakini kwa Watanzania, Waziri huyo wa Ujenzi sio mtu wanayemtilia shaka kuhusu uwezo wake. Amejipambanua kama mtendaji mahiri, mchapakazi na kiongozi asiyetaka ubabaishaji ambaye kwa muda wote aliofahamika ndani ya Serikali amekuwa mtu mwadilifu na wa kupigiwa mfano.
Tangu alipoteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Ujenzi mwaka 2005 na aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, tangu wakati huo msomi huyu wa udaktari wa sayansi ya kemia, amekuwa mmoja wa mawaziri wachache katika Serikali ya Awamu ya Tatu na baadaye Awamu ya Nne, anayefahamika kwa Watanzania kwa uchapakazi.
Hakuna Mtanzania wa kawaida kuanzia Tunduru hadi Horohoro, Tarakea hadi Mugumu, Bukoba hadi Singida, Kigoma hadi Dar es Salaam, asiyefahamu Magufuli si tu kwa jina au kwa sura, bali hata kwa utendaji wake kazi ambayo ameifanya katika nyadhifa mbalimbali alizokabidhiwa.
Uteuzi wake Dodoma mwezi mmoja uliopita uliwakuna wengi hasa ikizingatiwa pia kwamba hakuwa mmoja wa wagombea wa CCM aliyetumia muda mwingi kujipigia chapuo kwamba ndiye anayefaa kuteuliwa kwa nafasi hiyo. Aliendesha kampeni za kimyakimya, za kistaarabu na zilizozingatia kanuni, sheria na maadili ya chama chake.
Ana sababu ya kuwavutia wengi kuchaguliwa kuwa mrithi wa Rais Kikwete kwa sababu ya uwezo alionao, uadilifu, uchapakazi na utendaji usiotiliwa shaka katika kuongoza. Watanzania hawatafanya kosa wakimchagua.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment