Image
Image

Wanawake waaswa kushiriki kampeni za uchaguzi.

“KUNA umuhimu mkubwa kwa wanawake kushiriki kwenye mikutano ya kampeni za kisiasa ili waweze kufahamu sera za wagombea na kuchagua viongozi watakaosimamia ajenda ya haki na maendeleo ya wanawake,” anasema Fortunata Makafu.
Makafu ambaye ni Mwezeshaji kutoka shirika la Woman Wake Up (WOWAP) lenye makao makuu Mjini Dodoma ametoa kauli hiyo hivi karibuni wakati akizungumza na wanawake wa kata ya Lupeta wilaya ya Mpwapwa kwenye mafunzo ya kuwajengea uwezo wanawake juu ya kushiriki katika uchaguzi.
Makafu anasema ajenda za wanawake zinatekelezwa kwa kutegemea mfumo wa maisha katika eneo husika na unaweza kupikwa kwa kuangalia mgawanyo wa rasilimali kwa kuzingatia kijinsia, vipaumbele vya huduma za jamii, na ushiriki wa mwanamke katika shughuli mbalimbali za maendeleo na kwenye vyombo vya kutoa maamuzi. Makafu anasema wakati huu wa kuelekea uchaguzi mkuu wanawake wanatakiwa kushiriki kikamilifu kwenye mikutano ya kampeni ili kusikiliza sera za wagombea na hatimaye kumpigia kura kiongozi ambaye anafaa.
“Wanawake lazima mshiriki kwenye kampeni ili mfanye chaguo sahihi, usikubali kupokea rushwa, kiongozi anayetoa rushwa hataweza kukuletea maendeleo ni muhimu kuwaepuka viongozi wa nipe nikupe,” anasema Makafu. Anawataka wanawake kutambua kushiriki kwenye uchaguzi ni haki yao ya msingi hivyo wanapaswa kuitambua, kuithamini na kuitumia ipasavyo kwa kuzingatia na kusisitiza kwa kusema , “haki huwa haiombwi inuka uitafute.”
Makafu anasena wanawake wengine bado wana mawazo kuwa hawafai kuongoza lakini inabidi ifike mahali waijue thamani yao katika kuleta mabadiliko na kushiriki kikamilifu katika shughuli za siasa kwa kupiga na kupigiwa kura. “Msikubali kununuliwa kwani kura yako ina thamani kubwa sana kama utaitumia vizuri kwa manufaa ya jamii,” Makafu anasisitiza.
Mwezeshaji Nuhu Suleiman anasema anawataka wanawake kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye uchaguzi na watumie vizuri kura zao kwa kuchagua viongozi ambao wataleta mabadiliko. Anasema ushiriki wa wanawake kwenye mikutano ya kampeni bado hafifu kutokana na changamoto kubwa ambazo wanawake wamekuwa wakikabiliana nazo kama vile kunyimwa ruhusu na waume zao, kuzidiwa na kazi nyingi za nyumbani na uelewa mdogo wa umuhimu wa kushiriki katika kampeni za kisiasa.
Anasema wanawake wanatakiwa kuachana na dhana potofu kuwa siasa ni shughuli ya wanaume na kusisitiza kuwa wanawake wanapaswa kushiriki kikamilifu kuchagua viongozi bora kwa kuwa wana mahitaji mengi zaidi ya wanaume hasa huduma mbalimbali hasa za afya.
Suleiman anasema vipaumbele vinatofautiana; wakati wanaume wanapoona kipaumbele chao ni barabara kwa vile wanaendesha pikipiki, gari au baiskeli, wanawake wanaona kipaumbele chao ni zahanati, maji na shule kwa kuwa wanapenda kuona watoto wao wakipata huduma nzuri ya afya, maji safi na salama na elimu bora kwa watoto.
Hata hivyo anawataka wanawake wa Mpwapwa kutambua haki zao na wajibu wao wa kidemokrasia katika kushiriki uchaguzi mkuu ujao ili wachague viongozi watakaoweza kusimamia ajenda zao na kuwaunga mkono wagombea wanawake ambao wana sifa za kuongoza.
Anasema tangu nchi ipate uhuru Tanzania imekuwa ikikabiliwa na maadui watatu umasikini, ujinga na maradhi na maadui hao wataweza kuondolewa iwapo watapatikana viongozi wenye uwezo wa kuongoza na kuendeleza mazuri yaliyofanywa na viongozi wengine.
Pamoja na hayo anasema uoga ni adui mkubwa wa maendeleo ya mwanamke. Pia anasema asilimia 51 ya Watanzania ni wanawake lakini ushiriki wao katika kugombea nafasi mbalimbali za uongozi bado ni mdogo. Anasema wanawake wanatakiwa kushiriki kwenye uchaguzi na kuchagua wale walio tayari kutekeleza ajenda za wanawake. Anawataka kuona umuhimu wa kushiriki kwenye mikutano ya kampeni ili kusikiliza sera za wagombea na kuwauliza maswali pamoja na kuona umuhimu wa kujitokeza kupiga kura.
‘Wanawake ni sehemu kubwa ya jamii na wanahitaji kufanya mabadiliko ya kimfumo, pia wamekuwa wakikabiliwa na changamoto za kiuchumi wengi hawana fursa za kiuchumi ni vizuri ukachagua mgombea ambaye yuko tayari kuleta mabadiliko,” anasema. Anawahimiza wanawake wasikubali kununuliwa na viongozi wanaotafuta madaraka kwa kutumia fedha kwa kuwa mgombea anayetoa rushwa hata kuwa na deni endapo atachaguliwa hivyo atatumia madaraka kutafuta fedha badala ya kuwahudumia wananchi.
“Msikubali kununuliwa kwa kopo la pombe, khanga, kitenge au fulana, mtalipa yoye hayo kwa kipindi cha miaka mitano kwa kukosa maendeleo.... kwa kuwa kiongozi atakayeinga madarakani kwa kutumia fedha ataendelea na mambo binafsi na hamtakuwa na uwezo wa kumhoji maana uongozi wake ni wa kununua,” anasema.... Anasema ni wajibu wa kila mpiga kura kwenda kwenye mkutano ili kuwasikiliza wagombea na kuwapima.
“Ni lazima mshiriki kwenye mikutano yote ya vyama vya siasa bila kubagua kwani huwezi kufahamu kiongozi mzuri ni yupi kama utakuwa hujamsikiliza,” anasema. Anasema kampeni ni harakati za wagombea kuwashawishi wapiga kura kuwaletea maendeleo ‘nitoe rai mshiriki kampeni kwa kila mgombea aliyeteuliwa ili kuangalia ni nani analeta maendeleo bila kujali mwanachama wa chama chako au sio, lakini kama mwananchi ili kutimiza haki ya msingi ya kila mgombea ili mwisho wa siku ufanye maamuzi sahihi’’ anasema.
“Ni muhimu sana kujitokeza pale tume itatangaza tarehe ya kampeni ili kusikiliza sera za wagombea wote, ”anasisitiza. Mratibu wa mradi huo, Nasra Suleiman anasema mafunzo hayo yanatolewa kupitia mradi wa Fahamu Ongea Sikilizwa, awamu ya pili, yanalenga wanawake walio kwenye makundi mbalimbali wakiwemo walemavu na vijana kwa lengo la kuwajengea uwezo juu ya kushiriki katika uchaguzi.
Anasema mradi huo una lengo kuu la kuhakikisha kunakuwa na usawa na uwazi katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu ili wananchi waliopo pembezoni hasa wanawake na vijana waweze kushiriki kikamilifu kama wapiga kura, wagombea wa nafasi mbalimbali .
Pia kuwahamasisha na kukuongeza uelewa wa wananchi kushiriki kikamilifu katika uchaguzi kama wapiga kura, watazamaji, waangalizi na wagombea.” Tunataka kuimarisha uwezo wa wanawake ili washiriki kikamilifu kwenye mchakato mzima wa uchaguzi.
Anasema wamechagua wanawake kupata mafunzo hayo kwani ni kundi lililo pembeni na mfumo uliokuwepo umewanyima nafasi za ushiriki kwenye uongozi na hata wanawake viongozi ni wachache. JU
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment