Image
Image

Tutatue changamoto hizi sekta ya kilimo.

HIVI karibuni Rais Jakaya Kikwete amekaririwa akisema sekta ya kilimo inakabiliwa na changamoto sita ambazo zinasababisha sekta hiyo kushindwa kupiga hatua nchini.
Kwa mujibu wa Rais Kikwete changamoto hizo ni matumizi ya jembe la mkono ambalo husababisha uzalishaji mdogo, kilimo kutegemea mvua kila mwaka, mabadiliko tabianchini, matumizi ya mbegu za asili na matumizi madogo ya mbolea.
Rais Kikwete alizitaja changamoto nyingine ni kukosa ujuzi na maarifa kwa wakulima walio wengi hivyo, kujikuta wakilima kilimo kisicho na tija kwao na Taifa.
Alisema mengi katika kukabiliana na changamoto hizo, ikiwa ni pamoja na Serikali kuongeza bajeti kila mwaka, ambapo bajeti ya mwaka 2005 walitenga sh. milioni 200, na mwaka jana ilikuwa zaidi ya sh. bilioni moja.
Pamoja na kuongeza bajeti ni lazima kwenda mbali zaidi kubaini sababu sa sekta ya kilimo kupewa kisogo au kutothaminiwa. Ni kweli matumizi ya jembe la mkono yamepitwa na wakati ni muda wa kuwekeza kwenye matrekta.
Ni muda wa kuhakikisha tunawekeza katika kilimo cha umwagiliaji badala ya kuangalia angani tukisubiri mvua ya Mwenyezi Mungu. Wakati umefika kutumia mbegu bora. Siku hizi kuna malalamiko ya wananchi kuuziwa mbegu feki.
Hali hii inawaathiri wakulima kifedha na kupoteza nguvu zao bure. Katika eneo hili Serikali inatakiwa kuwasaka na kuwakamata wanaowauzia wakulima mbegu ambazo hazifai. Mbegu ambazo hawezi kustawi.
Si hivyo tu, kuna kila sababu ya Serikali kuhakikisha mazao ya wakulima yanakuwa na thamani. Ilivyo sasa ni kama vile wakulima wamekataa tamaa ya kuendeleza kilimo kutokana na kupewa bei ndogo ya mazao yao.
Kuna kila sababu ya Serikali kuvunja ukimya na kupitia upya bei ya mazao ya wakulima. Haiwezekani wakulima wapinde migongo, watumie fedha zao kugharamikia mazao yao, lakini wanapouza wanakopwa au kulipwa bei ndogo.
Kwa maoni yetu changamoto kubwa ya kuimaliza ni kuhakikisha mazao ya wakulima yananunuliwa kwa bei nzuri. Kwa kufanya hivyo mazao yaliyotupwa kisogo, yatafufuliwa na kusaidia kuharakisha kukuza uchumi wa nchi.
Jambo nyingine ni wataalamu wa sekta hiyo kutimiza wajibu wao. Wakutane na wakulima na kuwashauri namna ya kulima kwa ufanisi. Wasiishie kukaa ofisini kwa sababu huko hakuna kilimo. Waendee vijijini.
Ni matarajio yetu kwamba umefika wakati muafaka kuzipatia ufumbuzi wa kweli changamoto zilizopo badala ya kuishia kuzijadili kwa kupapasa. Ni lazima kila mmoja kwa wakati wake atimize lengo ili kunyanyua sekta hiyo kwani kwa sasa imedumaa.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment