Jana,kulikuwa na habari inayosema‘Ukosefu wa fedha waathiri Hospitali ya Mkoa wa Dodoma’.
Kwa mujibu wa habari hiyo, kwa sasa hospitali hiyo inakabiliwa na
matatizo kadhaa na changamoto kubwa ya kifedha, hivyo kuifanya ishindwe
kukamilisha ujenzi wa baadhi ya miundombinu hospitalini hapo, yakiwemo
majengo.
Hayo yalielezwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,Chiku Gallawa, mwishoni
mwa wiki wakati akizindua bodi mpya ya hospitali hiyo yenye jumla ya
wajumbe 12.
Fedha zinazotolewa kwa hospitali hiyo, zimekuwa ni kidogo. Hata hizo
kidogo nazo zimekuwa zikichelewa kupelekwa hospitalini hapo, hali
inayoifanya hospitali kushindwa kununua mahitaji yake kwa wakati,
ikiwemo kushindwa kuwalipa kwa wakati wazabuni na kukamilisha majengo.
Yapo majengo kadhaa ambayo yalitakiwa kujengwa na mengine yapo katika
hatua mbalimbali. Tatizo lingine kubwa la hospitali hii ni upungufu wa
watumishi, ambapo Mkuu wa Mkoa anaeleza kuwa upungufu wa watumishi
uliopo, unafikia asilimia 79 na waliopo ni asilimia 21 tu.
Ni wazi kuwa hali ya namna hii, kwa hospitali ya rufaa ya mkoa,
haikubaliki. Upungufu huu wa watumishi ni mkubwa mno na unasababisha
utoaji wa huduma wa kila siku kwa wagonjwa wanaolazwa na wanaotibiwa na
kurejea nyumbani, kuwa mgumu mno.
Utoaji huduma za afya kwenye taasisi yenye upungufu wa kiasi hiki
huwa ni mzigo kwa watendaji na hata kwa wajumbe wa bodi. Tunaunga mkono
agizo la Gallawa la kuitaka bodi mpya ya hospitali hiyo, kuboresha
huduma za afya katika hospitali hiyo na kuzifanya ziendane na wakati
ulipo sasa.
Tunaomba wajumbe wa bodi kukaa na watendaji, kubuni mbinu mpya za
kupunguza matatizo yaliyopo na kupendekeza kwa serikali mikakati ya
kuboresha hospitali hii. Hospitali hii inatakiwa kuwa ya mfano kwa
hospitali zote za mikoa nchini kutokana na umuhimu wa mji wa Dodoma.
Mbali na matatizo ya fedha na watumishi, hapana budi changamoto
zingine za ukosefu wa magari na vitendea kazi nazo zitatuliwe. Wadau
kama vile kampuni za simu, mashirika ya hifadhi ya jamii, kampuni na
watu binafsi, hapana budi kuisaidia serikali kuboresha huduma za
hospitali hii.
Tunatambua wapo wadau waliowahi kuisaidia hospitali hii vitanda,
magodoro na mashuka. Lakini, misaada hiyo haitoshi, kwani hospitali hii
bado inahitaji vitanda, magodoro na mashuka mengi zaidi kwa ajili ya
kuhudumia wagonjwa wanaofika hapo.
Ni dhahiri hospitali ya Dodoma inatakiwa kusaidiwa haraka, kutokana
na kuhudumia watu wengi na pia kuwa kwenye mkoa wenye hekaheka nyingi za
kisiasa kwa karibu mwaka mzima.
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)


0 comments:
Post a Comment