Image
Image

Shule binafsi zatiwa kitanzia kuongeza ada kwa wanafunzi.

WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imepiga marufuku shule binafsi kuongeza gharama za uendeshaji wa shule, zikiwemo ada kwa mwaka wa masomo unaoanzia mwezi Januari mwaka ujao mpaka watakapopata maelekezo kutoka kwa Kamishna wa Elimu nchini.
Kwa shule ambazo tayari zimetangaza kuongeza gharama na ada kwa mwaka wa masomo wa 2016 bila kibali cha Kamishna wa Elimu, Wizara haitambui ongezeko hilo kwa kuwa ni batili na hivyo zimefutwa,” lilisema tangazo la Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ambalo gazeti hili lilipata nakala yake jana.
Wizara hiyo imesisitiza kuwa ada zote kwa shule zisizo za serikali zitabaki kama zilivyokuwa zimeidhinishwa na Kamishna wa Elimu. Shule zinazohusika na tangazo hilo la Serikali ni shule binafsi za awali, msingi na sekondari.
Waraka wa Elimu Namba Nne wa Mwaka 2008, uliweka viwango vya ada vinavyotozwa katika shule za msingi na sekondari za serikali na zile zisizo za serikali. Ada iliyowekwa kwa shule za kutwa zisizo za serikali ni Sh 150,000 na shule za bweni Sh 380,000 kwa mwaka kwa kila mwanafunzi.
Waraka huo pia ulielekeza kwamba ongezeko lolote la ada, lazima lipate kibali cha Kamishna wa Elimu kabla ya kuanza kutumika. Tangazo hilo linaeleza kuwa pamoja na katazo hilo la Serikali, imegundulika kuna baadhi ya shule zisizo za serikali, zimekuwa zikiongeza ada kila mwaka pasipo kupata kibali cha Kamishna wa Elimu.
“Utamaduni huu wa kuongeza ada kila ifikapo mwishoni mwa mwaka umekuwa ukisababisha usumbufu mkubwa kwa wazazi na walezi na hata baadhi yao kushindwa kuendelea kusomesha vijana wao katika baadhi ya shule,” lilisema tangazo hilo.
Kwa msimamo huo, wizara hiyo imezitaka shule zote za binafsi, kuwasilisha taarifa kwa Msajili wa Shule aliyepo Idara ya Ithibati ya Shule, kueleza kiasi cha ada na gharama kinachotozwa kwa sasa kabla ya mwaka wa masomo 2016.
Shule hizo pia zinatakiwa kuelezea kwa mara ya mwisho tarehe ambayo shule husika, ilipata kibali kutoka kwa Kamishna wa Elimu kutoza kiwango hicho cha ada. Taarifa hizo zinatakiwa kufika ndani ya wiki mbili kuanzia jana.
“Wathibiti ubora wa shule waliopo sehemu mbalimbali nchini wanaagizwa kulifuatilia suala hili kwa karibu ili kila shule itekeleze agizo hili na kutoa taarifa zilizoelekezwa katika tangazo hili. Hatua za kinidhamu zitachukuliwa kwa wamiliki ambao hawatatekeleza maagizo haya,” ilisema taarifa hiyo.
Pamoja na kukataza shule kutopandisha ada, Wizara hiyo imefafanua kuwa kwa sasa iko katika hatua za mwisho za utafiti na kuandaa mfumo wa kielektroniki wa kutambua gharama za kumsomesha mwanafunzi katika elimu msingi, ambayo ni elimu ya awali, msingi na sekondari.
Kutokana na hatua hiyo, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imewaomba wadau mbalimbali, watoe ushirikiano kwa timu za wataalamu wanaofanya kazi hii ili kusaidia katika kuukamilisha mfumo na hatimaye kuwa na ada elekezi katika maeneo mbalimbali.
Tamko hilo la wizara limetolewa wakati tayari shule nyingi za binafsi, zimeshatangaza kupandisha ada kwa mwaka ujao wa masomo kwa kisingizio cha kupanda kwa gharama za uendeshaji wa shule.
Ada kwa shule nyingi zisizo za Serikali zinatofautiana na ziko kati ya Sh 800,000 hadi Sh 5,000,000. Ada hizo ni nje ya michango ya majengo, mitihani, kitambulisho na matibabu, jambo ambalo limesababisha wazazi wenye uwezo wa kifedha ndio ambao wamekuwa wanasomesha watoto wao kwenye shule hizo.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment