Image
Image

Wanaosababisha sukari kupanda bei ni majipu yafaa watumbuliwe.

BAADA ya Rais John Magufuli kusitisha uingizaji wa sukari kutoka nje ya nchi ili kulinda na kufufua viwanda vya ndani, kumekuwa na malalamiko katika siku za hivi karibuni kwamba bidhaa hiyo imepanda bei ghafla.
Kabla ya agizo hilo, sukari ilikuwa inauzwa kati ya Sh 1,800 hadi Sh 2,200 lakini taarifa ambazo zimekuwa zikitolewa na wananchi zinaonesha kwamba bei ya sukari katika baadhi ya maeneo imepanda hadi kufikia Sh 2,600.
Dhana iliyokuwepo kutokana na kupanda kwa bei ya sukari ghafla baada ya zuio la Rais ilikuwa kwamba huenda viwanda vyetu bado havikidhi mahitaji ya soko la ndani. Lakini tunashukuru taarifa ya Bodi ya Sukari kuonesha kwamba upatikanaji wa sukari nchini ni wa kuridhisha na ipo akiba ya kutosheleza nchi nzima.
Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Sukari Tanzania, Henry Simwanza, amekaririwa na gazeti hili akisema kwamba pamoja na baadhi ya viwanda kusimamisha uzalishaji wa sukari kutokana na msimu kuisha, hali ya sukari nchini ni nzuri kwani ipo akiba zaidi ya tani 62,000.
Mkurugenzi huyo anasema bodi yao imegundua kwamba kuna wafanyabiashara wakubwa ambao kwa sababu wanazozijua wenyewe wameamua kuficha sukari ili kusababisha upungufu na hivyo kupandisha bei.
Sisi tunadhani huenda pia wanafanya hivyo ili kuikomoa serikali na hatimaye iwaruhusu kuendelea kuingiza tena sukari kutoka nje inayowapa faida maradufu. Bodi ya Sukari imeweka wazi kwamba wanaofanya hujuma hizo watakapobainika watachukuliwa hatua za kisheria.
Imewataka wafanyabiashara kuuza sukari kwa bei elekezi ambayo ni Sh 1,800 kwa kilo katika jiji la Dar es Salaam na mikoa ya jirani. Sukari ni moja ya bidhaa muhimu kwa familia nyingi kwa sababu inatumika katika kutayarishia vyakula vingi.
Yapo mazingira ambayo hali ikiwa mbaya kimapato, familia inaweza kupitisha siku kwa kunywa uji, na ili hilo lifanikiwe ni lazima iwepo sukari. Kama hata bei ya bidhaa hiyo familia haitamudu hali inakuwa mbaya zaidi.
Sukari pia ninawezesha akina mama kufanya biashara za maandazi na vitumbua na hivyo kujiongezea kipato. Sukari inapopanda bei inakwamisha pia biashara hizo kutokana na kipato kidogo cha wananchi walio wengi.
Ni kwa msingi huo, tunaunga mkono kwa dhati juhudi za Bodi katika kupambana na watu wanaosababisha bidhaa hii muhimu kupanda bei. Tunaiomba Bodi isiishie katika kutoa onyo pekee, bali kuanza uchunguzi wa kina na kuchukua hatua stahili kwa kila atakayebainika kuhujumu agizo la Rais.
Kama alivyosema Mkurugenzi wa Bodi, Simwanza, ni vyema kila mwananchi asaidie kuwafichua watu wanaoficha sukari ili kupandisha bei na kufifisha juhudi za serikali za kufufua viwanda vya sukari, hatua ambayo pia ni faida kwa wakulima.
Tunaamini kwamba juhudi hizi zikiungwa mkono ipasavyo, tunaweza kuzalisha sukari ya kutosha na hata kuuza nje ya nchi, hatua itakayokwenda sambamba na kupanua maradufu kilimo cha miwa nchini.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment