Image
Image

Ziara ya Rais wa Vietnam ifungue milango ya fursa za Kiuchumi.

Ziara ya Rais wa Vietnam, Truong Tan Sang, nchini imebainisha kwamba Tanzania ina mambo mengi ya kuiga kutoka nchi hiyo na kwamba ikiyafanyia kazi, inaweza kupaa kiuchumi kwa kasi.
Nchi hiyo imepaa kwa kasi kubwa kiuchumi na moja ya sababu zilizoipaisha tunaambiwa kuwa ni kutumia malighafi ilizozichukua Tanzania zikiwamo mbegu za mpunga, korosho na samaki katika miaka ya sabini.
Siri hiyo ilifichuliwa juzi na Rais Dk. John Magufuli wakati wa mazungumzo na kiongozi huyo na kusema kuwa mbegu hizo ndizo zilizoifanya Vietnam kuwa kinara katika uzalishaji wa mazao hayo pamoja na ufugaji wa samaki.
Rais Magufuli amewataka Watanzania kuiga Vietnam katika uzalishaji wa mpunga, korosho na ufugaji wa samaki, ili kuchangia uchumi wa nchi na pato la taifa.
Alisema Watanzania wanatakiwa kuiga Vietnam yenye watu wanaokadiriwa kuwa milioni 91, ambao wamepiga hatua kubwa ya uzalishaji, hata uchumi wao umekua kwa asilimia 50 na kwamba imefanikiwa kupunguza umaskini kwa asilimia 50 na sasa imetoka katika uchumi wa chini hadi uchumi wa kati.
Kilichomshangaza Rais Magufuli ni Vietnam kuchukua rasilimali hizo kutoka nchini na zikaipaisha kiuchumi wakati Tanzania ikiendelea kusuasua kiuchumi. Kauli ya Rais Magufuli inaonyesha jinsi gani alivyoguswa na hali hiyo na bila shaka ameichukua kama changamoto ya kufanyia kazi haraka iwezekanavyo.
Jambo la msingi ni kwa Tanzania kutuma wataaamu wake kwenda Vietnam kujifunza jinsi walivyozitumia mbegu hizo kuendelea ili tutumie mbinu walizozitumia kuzalisha mazao hayo na samaki.
Kingine ambacho Tanzania inapaswa kufanya ni kuwavutia wawekezaji makini na  kutoka Vietnam waje kuwekeza katika sekta mbalimbali za uchumi kutokana na nchi hiyo kupiga hatua kubwa katika biashara.
Kwa kuona umuhimu huo, Serikali imesema imefungua milango ya uwekezaji kwa wafanyabiashara kutoka Vietnam kuja kuwekeza katika sekta mbalimbali zikiwamo utalii, mawasiliano, mafuta, gesi, kilimo, ufugaji, nishati na huduma za kijamii.
Kauli hiyo ilitolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, wakati wa  Mkutano uliowakutanisha wafanyabisahara wa Vietnam na Tanzania juzi, akisema kuwa kampuni za Vietnam zilizo tayari kuwekeza nchini zinakaribiswa kwa kuwaTanzania ina zaidi ya hekari milioni 43 za ardhi, na kati ya hizo, hekari milioni moja ni zenye rutuba na zinafaa kwa kilimo.
Tanzania imekuwa ikiwashawishi wawekezaji kuja nchini kuwekeza, lakini uwekezaji katika kilimo haujafanyika licha ya nchi yetu kuwa na ardhi kubwa inayofaa kwa kilimo.
Sababu kubwa ambayo inasababisha wawekezaji wasichangamkie kuwekeza katika sekta ya kilimo ni kutokana na sekta hiyo kuhitaji mtaji mkubwa tofauti na sekta nyingine ambazo wawekezaji wanakuja na kutengeneza faida kubwa baada ya muda mfupi.
Kwa kuwa Vietnam imeonyesha nia ya kushirikiana na Tanzania katika sekta mbalimbali, tunawashauri viongozi wetu waweke mkazo katika kuwashawishi wawekezaji kutoka Vietnam kuwekeza zaidi katika sekta ya kilimo kwa kuwa ndio uti wa mgongo wa Taifa hili wakati linajiandaa kwenda katika uchumi wa kati.
Ikumbukwe kwamba kilimo licha ya kuongeza chakula, lakini pia kinaweza kutoa ajira kwa Watanzania wengi ikiwa watapatikana wawekezaji makini. Tunaamini kuwa serikali ikiwa makini, ziara ya Rais Truong Tan Sang nchini itafungua fursa zaidi za kiuchumi kwa nchi yetu.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment