HALMASHAURI ya Wilaya ya Longido mkoani Arusha,
imetakiwa kuandaa upya taarifa ya ukaguzi iliyoiwasilisha kwa Mkaguzi na
Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) mwaka 2013/14 na kuiwasilisha upya
katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Serikali za Mitaa (LAAC).
Akitoa maagizo hayo mwishoni mwa wiki jijini Dar es
Salaam, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Abdallah Chikota alisema taarifa ya
awali imeonesha dalili za ufisadi.
Alitaja baadhi ya dosari kwenye ripoti hiyo kuwa ni
uzembe wa kutojibu hoja 116 za ukaguzi, zinazohusu matumizi mabaya ya fedha za
Serikali.
Chikota alisema Kamati inatakiwa kufanyia kazi
taarifa iliyopitiwa na CAG, lakini taarifa iliyowasilishwa kwenye kamati hiyo
na halmashauri hiyo, haijafanyiwa kazi na CAG hivyo hawawezi kuendelea kuihoji Longindo.
“Tumeona kwenye taarifa yenu kuna harufu ya ufisadi,
tutawatembelea huko huko kukagua miradi yenu tuone uhalisia wake na fedha
zinazotajwa kutumika, kwa sababu inashangaza kuona mnataja fedha tu
zilizotumika kwenye miradi, bila kuonesha nyaraka zozote za uthibitisho wake,”
alisema Chikota.
Chikota alisema, kamati haiwezi kuendelea kupitia
kitabu cha taarifa zao na kuwataka wajibu kwanza hoja hizo za ukaguzi kisha
kuandika kitabu kipya na kukiwasilisha mbele ya kamati.
Akizungumzia baadhi ya hoja zisizo na vithibitisho,
Chikota alisema halmashauri hiyo inaonesha kutumia mafuta ya magari ya Sh mil
17, lakini fedha hizo hazikuidhinishwa, hivyo kuhitaji ufafanuzi wa kina.
Alisema, ili kudhihirisha kwamba halmashauri hiyo
ina ufisadi mkubwa, imetumia Sh mil 453 bila kutoa maelezo na kufanya malipo
mbalimbali ya Sh mil 50.4 ambayo hata hivyo, vocha zake hazikuonekana. Pia,
alisema kuwa ilikusanya Sh mil 97 ambazo hazikupelekwa benki.
0 comments:
Post a Comment